
vii
Jukumu la mwalimu katika kutimiza malengo haya
Ili kutimiza malengo haya, mwalimu ana wajibu muhimu. Mwalimu azingatie
mazingira ya shule na kutoa mifano halisi ya vitu au watu wanaopatikana katika
mazingira ya shule. Kuna mazingira ya mjini na ya mashambani.
Mwalimu ana wajibu wa kujitayarisha mapema kabla ya somo kwa kuhakikisha
ana vifaa vya kutumia darasani ili kufanikisha somo. Vifaa hivi viwe vinapatikana
kwa urahisi au kwa bei rahisi iwapo ni vya kununuliwa.
Mwalimu anapaswa kutumia mwongozo huu na kitabu cha wanafunzi na
rasilimali nyingine yoyote itakayofanikisha kipindi chake. Mwalimu asitumie
mwongozo huu kisisisi bali awe mbunifu kulingana na uwezo wa wanafunzi wake
na vifaa vinavyopatikana.
Mwalimu aanze kwa kufundisha dhana sahili kabla ya kufundisha zile
changamano zaidi. Lazima azingatie uwezo wa wanafunzi wake.
Mwalimu anapaswa kuwashirikisha wanafunzi wake kadiri iwezekanavyo
katika somo la Kiswahili. Kwa kuwashirikisha, watakuza stadi zao za kusikiliza,
kuongea, kusoma na kuandika.
Mifano anayotoa darasani, iwe rahisi,sahihi, ya hali ya kila siku na inayoeleweka
kwa wanafunzi kuhusu mazingira yao na kuihusisha na masuala ibuka kama vile:
uadilifu, haki za watoto, Ukimwi, jinsia na teknolojia. Jukumu kubwa la mwalimu
ni kuwahamasisha wanafunzi kuongea, kusoma na kuandika lugha ya Kiswahili
kwa ufasaha. Hili ni jukumu ambalo mwalimu yeyote wa Kiswahili hawezi
kuepuka.
Lazima mwalimu awe kielelezo kwa wanafunzi wake kwa sababu wanafunzi
hupenda sana kuiga. Awe ni mtu anayeipenda lugha ya Kiswahili na kuionea
fahari ili awatie ari wanafunzi wake kuipenda lugha ya Kiswahili.
Mwalimu mwema ni yule anayejaribu kuwa katika kiwango cha wanafunzi.
Kama ni kuimba, wote wanaimba, kama ni kuigiza naye anaigiza. Mwalimu
sharti awe mchangamfu ili awachangamshe wanafunzi wake. Asifunze mambo
au mada kidhahania tu. Ataje matukio halisi maishani mwa wanafunzi huku
akiwahusisha katika kila hatua darasani. Mwongozo huu ni kama dira kwa
mwalimu katika kutekeleza mambo haya.
Mwalimu ajaribu kutumia rekodi za redio pamoja na video ili kuwavutia
wanafunzi mbali na kuendeleza stadi za kusikiliza na matamshi bora. Mwalimu
awahusishe wanafunzi katika kuchora picha, kuigiza darasani, kuimba na
kuwahusisha katika mijadala ili somo la Kiswahili liwe hai. Mwalimu anaweza
kuwaalika shuleni watu waliobobea katika Kiswahili ili kuwahamasisha wanafunzi
kuipenda na kuionea fahari lugha ya Kiswahili.