Eliana Binti Mfalme
na Hadithi Nyingine
Yahya Mutuku
Eliana Binti Mfalme na Hadithi Nyingine
Kimechapishwa na Queenex Publishers Limited
S.L.P 56049-00200, Nairobi,Kenya.
Simu: 0727 794 498, 0715 808 200
Baruapepe: info@queenexpublishers.co.ke
queenexbooks@gmail.com
Tovuti: www.queenexpublishers.co.ke
© Yahya Mutuku, 2021
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili,
kupigisha chapa, kutafsiri au kutoa kitabu hiki kwa
jinsi yoyote ile bila idhini kwa maandishi ya Queenex
Publishers Limited.
ISBN: 978-9966-141-41-5
Chapa ya kwanza 2021
1
Eliana Binti Mfalme
2
Hapo zamani palikuwa na mfalme mmoja.Aliitwa
Mfalme Makame.Aliongoza nchi iliyoitwa Upendo.
Ilikuwa nchi yenye amani. Raia wote walimpenda
mfalme sana.
Mfalme alikuwa na binti mrembo ajabu.Binti huyo
aliitwa Eliana. Eliana alikuwa msichana mzuri.
Mfalme alimpenda sana Eliana.
3
Eliana alikuwa na marafiki wengi. Walikuwa
wasichana. Marafiki hao walimwonea wivu.
Hawakupendezwa na urembo wake. Walipanga
njama ya kumwumiza.
Eliana alikuwa na kasuku. Baba yake alimpa
kasuku huyo zamani. Kasuku alimpenda sana
Eliana.Alipenda kukaa na Eliana kwenye bustani.
Usiku,Eliana alimfungia kasuku wake katika tundu
lake.
Siku moja, marafiki za Eliana walimtembelea.
Walitaka kucheza naye. Eliana alitoka kwenda
kucheza.Alimwacha kasuku wake. Kasuku alitaka
kumfuata ila Eliana alimshauri kasuku kubaki.
Eliana na marafiki zake walifika mahali msituni
penye mto. Ulikuwa ni mto wenye maji mengi.
Maji yalikuwa safi sana. Ndani ya mto kulikuwa
na samaki.Walikuwa samaki wa kila aina.
“Sikiliza Eliana. Tutacheza mchezo hapa mtoni.
Ni lazima ucheze nasi. Ukikataa, tutaamini kuwa
wewe ni mwoga. Binti wa mfalme hafai kuwa
mwoga, wasichana walimwambia.
Ulikuwa mchezo wa kuvua samaki. Kila msichana
alikuwa na kikapu. Kila mmoja alitakiwa kuvua
4
samaki hamsini. Walikubaliana wavue samaki
wakifumba macho.
5
Kumbe wasichana hao walikuwa wajanja!
Hawakufumba macho. Eliana alitii ushauri wao.
Alivua samaki wadogo wanaoitwa dagaa.
Alishindwa kujaza kikapu chake.
Wasichana hao waliamua kumuadhibu Eliana.
Walimfungia kwenye mti kisha wakaondoka.
Eliana alishindwa kujitoa mahali pale. Walitaka
Eliana aliwe na wanyama wa mwituni.
Wasichana waovu walitembea haraka. Hakuna
mtu aliyewaona kwenye kasri wakimwita
Eliana. Walikubaliana wakiulizwa wangesema
hawakumwona. Walimwonea Eliana wivu kwa
kuwa alikuwa binti mrembo sana.
Eliana alianza kulia. Alilia sana. Hakuna mtu
angemsikia.Alijuta kumwacha kasuku wake.Alilia
akimwita kasuku wake.Ghafla,Eliana alisikia sauti.
Ilikuwa sauti nzuri sana. Ni sauti aliyoikumbuka.
Hakujua ilitoka wapi.
Ewe wangu Eliana,
Ni raki wa maana,
Mwengine raki sina,
Wewe ni yangu hazina.
6
Ilikuwa ni sauti ya kasuku wa Eliana. Eliana
alisubiri.
Baada ya muda mfupi kasuku wa Eliana alitokea.
Aliruka na kutua begani pa Eliana. Alimfungua
kamba alizofungwa mikono na miguu. Macho ya
Eliana yalikuwa mekundu.Alikuwa amelia sana.
7
“Acha kulia Eliana.Adui zako wamekuacha hapa
mtoni. Ni lazima urudi nyumbani. Baba na mama
wanakungoja. Nitakuonesha njia ya kurudi,
kasuku alimtia nguvu.
Kufikia jioni, Eliana alifika nyumbani. Alikuwa
ameumia mguu. Damu ilimtoka kwenye kidole.
Mfalme na malkia walikuwa na wasiwasi.
Eliana alilia alipowaona. Walimkimbilia Eliana.
Walimkumbatia kwa upendo.
8
“Mwanangu, ulienda wapi? Mbona ukatoka hapa
bila ruhusa yetu? Huko ulikoenda ulienda na
nani?” mama yake alimuuliza. Eliana alikuwa binti
mpenda ukweli. Hakuwadanganya. Aliwaeleza
yote yaliyotokea.
Siku iliyofuata,mfalme aliita baraza lake la wazee.
Wale wasichana waovu waliletwa kwa mfalme.
Waliogopa. Walitetemeka sana. Walipomwona
Eliana walianza kulia. Walimwinamia wakiomba
msamaha.
Mfalme Makame alikasirika sana. Malkia naye
alikuwa na hasira kama mkizi. Eliana alishangaa.
Kumbe wasichana hao walikuwa waovu! Ilikuwa
lazima waadhibiwe. Mfalme hakutaka kuwaona
tena.
“Baba, mama, ninaomba wasiadhibiwe. Adui
mpende. Ninaomba tuwasamehe. Hata hivyo,
wao si marafiki zangu tena. Nitajitafutia marafiki
wengine wazuri, Eliana alisema.
Mfalme alimpenda sana binti yake. Aliwaamuru
walinzi kuwa wasichana hao waovu wasikanyage
pale kwenye kasri tena. Alijua wangejaribu tena
kumdhuru Eliana.
9
Eliana aliwapata marafiki wengine wazuri.
Walikuwa vijana wenye nidhamu. Mfalme
hakuwakataza kumtembelea Eliana muda wowote
waliotaka.Walipenda kucheza na kasuku.
Mfalme alimtengenezea kasuku tundu zuri. Eliana
alimpenda zaidi na kumtunza vizuri.Wote waliishi
maisha ya raha mustarehe.
10
Jibu maswali yanayofuata.
1. Mbona marafiki za Eliana walimwonea Eliana
wivu?
2. Eliana na marafiki zake walienda kucheza
mchezo upi mtoni?
3. Tundu ni nini?
4. Mwimbie rafiki yako wimbo ambao kasuku
alimwimbia Eliana.
5. Hadithi hii inakufunza nini?
11
Mvulana Shujaa
12
Hapo zamani za kale paliondokea mvulana
aliyeitwa Fumo. Fumo alikuwa yatima. Fumo
aliishi katika kijiji kilichoitwa Ziwani. Wanakijiji
wa Ziwani walipenda sana ufugaji.
Fumo alikuwa mvulana mdogo lakini mwenye
nguvu nyingi. Kila mmoja alimpenda kwa kuwa
alikuwa na tabia nzuri.
13
Wanakijiji waliwapeleka ng’ombe na mbuzi
kwenye msitu wa Majimaji kula nyasi. Kulikuwa
na nyasi nyingi kwenye msitu huo wa Majimaji.
Siku moja, nyoka mkubwa aliyeitwa Mlavyote
aliingia katika msitu wa Majimaji. Alipenda sana
kula ng’ombe na mbuzi. Alianza kuwakamata
ng’ombe na mbuzi na kuwala.
Fumo alikuwa ameajiriwa kazi ya kulima shamba
na mama mmoja pale kijijini. Alisikia yote
yaliyosemwa kuhusu nyoka huyo hatari.Alitamani
kusikia mambo mengi zaidi.
Wanakijiji walikuwa na huzuni.Wazee waliogopa
sana.Watoto nao walilia waliposikia jina Mlavyote.
Vijana walianza kutafuta sehemu nyingine ya
kulisha mifugo.
Wanaume wa kijiji cha Ziwani walikutana.
Walikuwa na silaha kama vile mikuki, mishale,
nyuta, marungu na mawe. Walienda msituni
kumtafuta Mlavyote.
Walipomwona Mlavyote,walijitayarisha kupigana
naye. Mlavyote aliwakaribia. Alipopanua kinywa,
alitoa moto mkubwa. Wanaume walipouona
moto, waliogopa.Walikimbia kuelekea kijijini.
14
Wanakijiji walianza kujitayarisha kuhama kijijini.
Walitaka kwenda kutafuta mahali pengine pa
kuishi. Jambo hilo halikumfurahisha Fumo.
Fumo alienda nyumbani kwa kiongozi wa kijiji
Mzee Kalikwela. Alimwambia hapakuwa na
haja ya watu kuhama. Alisema alikuwa tayari
kupambana na Mlavyote.
15
“Ukinipa ruhusa ya kupigana na Mlavyote,
nitashukuru. Hakuna haja ya kutoka hapa kijijini.
Je, ni sehemu ipi bora yenye ardhi nzuri kushinda
Ziwani?” Fumo aliuliza.
“Haya basi, kama unajiamini, njoo hapa mbele
yangu, Mzee Kalikwela alimwita Fumo na
kumbariki.
16
Baadaye, Mzee Kalikwela aliwatangazia watu
wasihame. Alitaka wasubiri wajue iwapo Fumo
angemuua Mlavyote. Fumo alitafuta mtungi
mkubwa mno. Aliuweka kichwani na kuubeba.
Alitoka kijijini kila mmoja akimtazama. Watu
wengi walisema kuwa alikuwa anaenda kuliwa
na Mlavyote.
Fumo alipokaribia alipoishi Mlavyote, alianza
kuimba wimbo huu;
Mlavyote mla vyote, mfalume wa msitu,
Ulaye mifugo wote, mbuzi ng’ombe pia watu,
Ujumbe nimeulete, ewe mwenye nguvu chatu.
Mlavyote alipoisikia sauti nzuri ya wimbo aliipenda.
Kwa muda mrefu alitamani kusikiliza wimbo.
Alitoka alipojificha na kutambaa hadi alipokuwa
Fumo. Fumo aliendelea na wimbo wake mzuri:
Ingiya kwenye mtungi, ulaye vyote shujaa,
Ndo uke penye wengi, kijiji nakotokea,
Huko utakula vingi, mifugo na watu pia.
Mlavyote alishangazwa na ushujaa wa Fumo. Pia
alipenda wimbo wake na sauti yake nzuri.Aliingia
katika mtungi huo kisha akatulia. Fumo aliufunika
mtungi kabisa kisha akauweka kichwani na
kuanza safari ya kurejea kijijini.
17
Fumo alipokaribia kijiji cha Ziwani, Mlavyote
alisikia kelele za watu.Aliamini maneno ya Fumo
akijua angekula watu na mifugo.Fumo alitayarisha
moto mkubwa mno.Mlavyote alisubiri.Alikuwa na
furaha kuwa kila siku angemla ng’ombe au mtu.
18
Moto ulipokuwa tayari, Fumo aliuinua mtungi na
kuuweka juu ya mafiga.Aliongeza kuni nyingi kavu
nao moto mkubwa ukawaka. Mlavyote alishtuka.
Mtungi ulishika moto. Ngozi yake ilichomwa.
Alijigongesha kwenye mtungi lakini wapi! Moto
ulikuwa ukimuunguza kwelikweli.
19
Fumo alipofunua mtungi, moshi mwingi mweusi
ulitoka. Aliupiga mtungi kwa shoka ukapasuka.
Vipande vya Mlavyote vilivyoungua vilitawanyika
kila mahali. Huo ndio ulikuwa mwisho wa
Mlavyote.
Mzee Kalikwela aliita mkutano wa baraza la
wazee. Kila mmoja alipendekeza Fumo awe
kiongozi wa mashujaa. Fumo aliteuliwa kuwa
kiongozi wa mashujaa wote wa kijiji.
Fumo alipendwa kutokana na tabia zake nzuri.
Akiwa kiongozi, aliwaheshimu wadogo kwa
wakubwa. Watoto walizaliwa wakaitwa Fumo
kwa kuwa lilikuwa ni jina zuri.
Fumo alioa mke mzuri aliyeitwaTriza.Walijaaliwa
watoto wengi wazuri wa kike na kiume. Waliishi
kijijini Ziwani kwa raha mustarehe.
20
Jibu maswali yanayofuata.
1. Wanakijiji wa Ziwani walipenda kuwafuga
wanyama gani?
2. Msitu ambao wanakijiji waliwapeleka mifugo
wao ulikuwa unaitwaje?
3. Kwa nini wanakijiji waliishi kwa woga?
4. Unafikiri ni kwa nini Mzee Kalikwela alimwita
Fumo na kumbariki?
5. Hadithi hii inakufunza nini? Mweleze mzazi au
mlezi wako.
21
Sungura Amuua Fisi
Mwovu
22
Hapo zamani za kale paliondokea fisi mlafi
sana. Alianza kwa kula wanyama waliokufa
lakini baadaye akaacha. Aliingiwa na tamaa
akawakamata wanyama wakiwa hai na kuwala.
Wanyama waliogopa sana. Kila siku fisi aliwaua
wanyama na kuwala. Kwa sababu ya kula nyama
kila siku, fisi alinona sana kama nguruwe.
23
“Jamani tutasaidiwa na nani? Dada na kaka zangu
wote wameliwa. Huyu fisi ni mnyama mwovu
sana, paa alisema kwa huzuni.
Siku hiyo hiyo, sungura alikutana na fisi. Alikuwa
amebeba kikapu kikubwa kizuri. Sungura
alipomwona fisi, hakutoroka. Fisi alishangazwa
na ushujaa wa sungura.
24
“Mbona huniogopi?Wataka nikubadilishe kitoweo
sasa? Nimewala wanyama wengi. Ni wewe
umebaki na leo nitakuua na kula nyama zako,
fisi alimtisha sungura.
“Hakika fisi, sikuogopi. Nimekuwa nikikutafuta
kwa kuwa ninajua una nguvu. Pia wewe unapenda
kula nyama tamu.Je,una habari kuwa paa wanane
wamekamatwa na mwindaji?” sungura aliuliza.
“Sina habari hata! Paa wanane! Walikamatwa
lini?Wako wapi unipeleke nikawale?Wajua kati ya
wanyama wote niliokula nyama zao, ninaipenda
sana nyama ya paa. Ni tamu kupindukia, fisi
alisema huku mate yakimdondoka.
“Mwindaji aliwakamata pangoni. Amewafungia
katika mtego ng’ambo ya mto.Nimetoka huko leo
asubuhi. Ndiyo maana ninatembea nikikutafuta.
Je, utakubali kufuatana nami?” sungura aliuliza.
“Twende basi. Twende tukale nyama. Pongezi
sungura.Wewe ni rafiki unayenijali. Ikiwa ni kweli,
hakika sitakuua lakini ikiwa ni uongo, lazima leo
nikuue, fisi alisema kwa uchangamfu.
“Sawa, lakini ujue kila kitu kina sheria zake.
Mwindaji akikuona atakutambua mara moja. Ni
lazima ufanane na paa ili mwindaji akuruhusu
uingie katika mtego, sungura alimwambia fisi.
25
“Basi nifanye nini sungura? Je, mbona wewe
hufanani na paa? Unataka kunifanya nikose
nyama ya paa leo?” fisi aliuliza kwa hasira.
26
“La hasha fisi.Ninalo vazi nitakalokuvisha ufanane
na paa. Nimelificha huko mbali karibu na mtego.
Tatizo ni kuwa huna pembe. Ni lazima nikutafutie
pembe sasa hivi, sungura alijibu.
Sungura aliingia kichakani. Alitafuta vijiti
vyembamba akavichonga vizuri kwa kisu.
Vilionekana kama pembe ndefu.Alirudi alipokuwa
fisi.Fisi alipoona vijiti vilivyochongwa,alifurahi sana.
Alitamani sungura afanye haraka ili wasichelewe
kufika kwenye mtego. Alidhani mwanadamu
angeondoka na paa wote.
Sungura alichukua nyundo iliyokuwa kikapuni.
Alishika kijiti kimoja akaanza kukipigilia kichwani
pa fisi. Fisi alihisi maumivu mengi. Kijiti kiliingia
kichwani na damu ikamtoka kwa wingi.
“Fisi, tambua kuwa hakuna kizuri kisicho na
magumu kupata.Ni lazima uvumilie ikiwa unataka
kuwala paa. Geuka nikupigilie upembe huu wa
pili, sungura alisema huku akishika nyundo.
Sungura alipigilia kijiti cha pili.Alipigilia kwa nguvu
zake zote. Kijiti kiliingia kichwani sawasawa. Fisi
alikuwa na maumivu mengi. Haja ndogo ilimtoka.
Haja kubwa ilifuatia kutokana na maumivu.
27
“Mvumilivu hula mbivu rafiki yangu. Tayari una
pembe nzuri kichwani. Hebu jitazame kwenye
kioo hapa, sungura alisema. Alitoa kioo kidogo
katika kikapu akampa fisi.
Fisi alipojitazama kwa kioo, alifurahi. Alikuwa na
pembe ndefu kichwani. Alijipangusa damu kisha
wakaanza safari ya kwenda kwenye mtego.
28
Fisi alivuja damu nyingi sana.Kila walipopiga hatua,
aliishiwa nguvu. Sungura alimpa fisi matumaini.
Fisi alipokumbuka nyama alijikaza.
Hatimaye walifika. Mbele yao palikuwa na mtego
mkubwa. Fisi alimwona paa mmoja mkubwa sana
nje ya mtego.Alimeza mate. Hata hivyo, hakuwa
na nguvu za kuendelea kutembea.
29
“Ningoje nikakuchukulie lile vazi nililokuahidi,
sungura alisema na kumwacha fisi akilala kwa
maumivu. Aliporudi, aliandamana na paa kumi.
Kila paa alikuwa na fimbo mkononi.
Fisi alijaribu kuinuka akimbie akashindwa. Paa
walimpiga kwa pamoja hadi akafa.
Huo ndio uliokuwa mwisho wa fisi mlafi. Paa
walikuwa na furaha nyingi. Aliyekuwa akiwaua
naye alikufa.
“Wewe ni mnyama mdogo lakini una akili nyingi.
Tutakufanya mfalme wetu.Tunataka uwe kiongozi
wetu, paa kiongozi alimwambia sungura kwa
furaha.
Paa walimfanya sungura kiongozi wao. Sungura
aliwaongoza paa vyema. Aliendelea kutumia
hekima kuwaongoza wanyama hao msituni.
30
Jibu maswali yanayofuata.
1. Mbona wanyama wengi walimwogopa fisi?
2. Unafikiri ni kwa nini sungura alimwambia fisi
kuwa ni lazima afanane na paa?
3. Kwa nini fisi alipenda sana nyama ya paa?
4. Kwa nini paa walimpiga fisi hadi wakamuua?
5. Hadithi hii imekufunza nini? Mweleze rafiki
yako.
31
Kalu na Mbwa wake
Bosko
32
Jina langu ni Rashid Kalu. Mimi ni mvulana.
Nina umri wa miaka minane. Ninasomea shule
ya msingi ya Hekima. Mimi ni mwanafunzi wa
Gredi ya Tatu. Ninawapenda sana wanyama wa
nyumbani. Ninapenda kuwapa matunzo mazuri.
Mbwa wangu anaitwa Bosko. Baba yangu
aliniletea Bosko kama zawadi.
33
Huyu ndiye Bosko. Ni mbwa mkubwa sana. Mimi
ninampenda sana. Bosko ni mbwa mwenye nguvu.
Mimi humlisha nyama na mifupa kila siku.
Huwa ninamwosha Bosko kila siku kwa maji
safi na sabuni. Pia ninakisafisha kibanda chake.
Wanyama wanahitaji mazingira safi ili wasipate
maradhi.
34
Usiku mmoja majambazi walikuja nyumbani.Bosko
alibweka sana. Wezi walifyatua risasi. Sikusikia
Bosko akibweka tena. Wezi walituibia. Waliiba
runinga, redio na tarakilishi kisha wakatoroka.
Asubuhi ilipofika, nilimtafuta Bosko kila mahali.
Hatimaye nilimpata akiwa amejificha. Alikuwa
ndani ya ghala.Alikuwa ameumia. Sikio lake moja
lilivuja damu. Nilimtibu Bosko kwa dawa mara
moja.
Bosko alianza kunusa mchangani. Alitoa sauti za
ajabu. Nilijua alitaka kunionesha kitu. Alikimbia
akinusa mchanga. Niliamua kumfuata. Baba
na mama walikuwa wameenda sokoni. Nilizidi
kumfuata Bosko.
Bosko alizidi kwenda. Tulivuka mito na milima.
Nilipochoka, alifanya kelele zaidi. Nilijikaza na
kumfuata.Hatimaye nilichoka.Jasho jingi lilinitoka.
Nililala chini ya mti. Bosko alikuja kulala karibu
nami.
Bosko aliutumia mguu wake kuniamsha.Alinifanyia
ishara nimfuate. Tuliondoka na kuzidi kwenda.
Nilielewa Bosko alichotaka. Alikuwa akinipeleka
walipokuwa majambazi.
35
Tulifika mahali palipokuwa na mawe mengi.Bosko
alipanda juu ya mawe upesi.Alisimama karibu na
pango kubwa.Nilifika mahali alipokuwa.Alibweka
akichungulia ndani ya pango.Mle pangoni mlikuwa
na giza jingi. Mwangaza wa jua haukuingia ndani.
Macho yangu yalishindwa kuona ndani nikiwa nje.
36
Niliingia ndani ya pango.Nilikuwa nimebeba tochi
mfukoni.Pango lilikuwa kubwa mno. Nilienda hadi
huko ndani. Bosko alibaki nje akilinda.
Niliona vitu vingi ndani. Kulikuwa na vitu vya
elektroniki. Niliona simu, runinga, redio, jokofu na
vitu vingine vingi. Kulikuwa na magunia mengi.
Nilipoangalia ndani, niliona zilikuwa dawa za
kulevya.
Ghafla majambazi walinikuta pangoni.Walinifunga
kwa kamba. Nililia nikimwita Bosko. Nilihofia
kuwa majambazi wangempiga risasi. Niliwafikiria
baba na mama. Nilikuwa na huzuni. Hawakujua
kule nilikuwa.
Usiku ulifika haraka. Nilizidi kuogopa. Upepo
ulivuma kwa nguvu.Giza lilikuwa kila mahali.Wezi
waliwasha moto.Walikuwa na furaha.Walifurahia
mali waliyoiba.
Wezi walichoma nyama. Hawakunipa hata
kipande. Walikunywa pombe nyingi. Walilewa
sana.Wote walilala.Usiku,nilisikia kitu kikitembea
karibu nami. Kumbe alikuwa ni Bosko!
Bosko aliziuma zile kamba.Alizikatakata.Alikuwa
na meno makali sana. Kwanza, niliketi na kula
zile nyama. Zilikuwa tamu sana. Nilimpa Bosko
nyama naye akazila haraka.Alitafuna mifupa pia.
37
Nilikula nikashiba ndi! Bosko alishiba pia. Sote
tulishiba.
38
Niliona chupa ya dawa. Ilikuwa dawa ya usingizi.
Niliwawekea wezi puani. Waliendelea kulala
kabisa. Nilimwongoza Bosko tukatoka. Tulianza
safari usiku huo.
Tochi niliyoibeba ilinisaidia sana. Tulisikia
mngurumo wa lori.Tulijificha na kusubiri. Tuliona
lori la mizigo. Lilienda polepole. Mimi na Bosko
tulipanda lorini. Tulishikwa na usingizi. Tulilala
fofofo!
Alfajiri tuliamka.Tulishuka polepole. Lori lilikuwa
mjini.Niliongoza.Bosko alinifuata.Tulifika stesheni
ya polisi. Niliwaeleza askari kila kitu. Walitaka
nikawaoneshe penye pango la wezi.
Tulitumia gari la polisi. Niliwaelekeza nilivyoweza.
Tulipofika msituni, tuliacha gari. Bosko aliongoza.
Alienda haraka.Hatimaye tulifika.Askari waliingia
ndani pangoni.Wengine walibaki nje.
Wezi hawakuwa wameamka.Walikuwa usingizini.
Walilemewa na ile dawa ya usingizi. Wote
walifungwa pingu. Waliwekwa garini na sote
tukaondoka. Nilikuwa na furaha kwa kuwa wezi
wote walishikwa.
39
Vitu vyote ndani ya pango vilichukuliwa. Polisi
mmoja aliamua kunipeleka nyumbani. Aliwapata
wazazi wangu. Walikuwa na huzuni. Walifurahi
kuniona.Tulipata vitu vyetu, tena vikiwa salama.
Wezi walipelekwa mahakamani. Walihukumiwa
kifungo gerezani. Ama kweli, siku za mwizi ni
arubaini.
40
Jibu maswali yanayofuata.
1. Wezi waliiba bidhaa zipi nyumbani kwa akina
Kalu?
2. Kalu alimpata Bosko akiwa amejificha wapi?
3. Unafikiri ni kwa nini Bosko alikuwa ananusanusa
chini?
4. Maneno‘alinona kama nguruwe’ yanamaanisha
nini?
5. Iwapo ungekuwa Kalu, ungefanya nini?
41
Kalu na Nungunungu
42
Huyu ni Mzee Babusa. Mzee Babusa anatembea
polepole.Yeye ni babu yake Kalu. Kalu ni mjukuu
wake. Mzee Babusa yuko safarini. Anaenda
kumtembelea Kalu na wazazi wake.
Mzee Babusa anaipenda familia ya Kalu.
Anampenda Kalu na wazazi wake.Wanapendana
kama chanda na pete.
43
Mzee Babusa amefika kijijini. Kalu anamkimbilia
babu na kumkumbatia kwa furaha.
“Shikamoo babu, Kalu anamwamkua.
“Marahaba mjukuu wangu Kalu. U hali gani?”
“Njema babu, ila kuna shida shambani kwetu.
Baba amesema ukija nikupeleke huko mara moja,
Kalu anaeleza.
44
Kalu na babu wanafika shambani. Shamba la kina
Kalu ni kubwa sana. Baba yake Kalu anapalilia
mihindi. Mama yake Kalu amesimama karibu
na mgomba. Wote hawana furaha. Mihogo
imeharibiwa na nungunungu.
Ni asubuhi na mapema. Baba yake Kalu yuko
shambani. Amevalia bwelasuti. Miguuni ana
mabuti. Mkononi ameshika kwanja. Anamngoja
nungunungu. Amemwona karibu na kwekwe. Ni
lazima amuue.
Anataka kumpiga nungunungu kwa kwanja.
Nungunungu amemwona. Haogopi. Anamrushia
mwiba na kumchoma mkono. Baba yake Kalu
anapiga kelele na kukimbia.Nungunungu anafukua
muhogo na kuendelea kula.
Mama yake Kalu yupo shambani. Amemwona
nungunungu. Anataka mbwa, Bosko amkamate
nungunungu.Nungunungu anaachilia miba mitatu.
Bosko ameumia. Mguu wake wa mbele unavuja
damu. Nungunungu anaendelea kula mihogo.
Kalu anataka kumfukuza nungunungu. Kalu
amekwea mtini. Ana mawe na fyata mkononi.
Anampiga jiwe kwa fyata lakini hampati.
Kalu ametumia mawe yote. Nungunungu
amekataa kuondoka.
45
Babu yake Kalu ametengeneza mtego mkubwa.
Ameutengeneza kwa vijiti vingi. Amemtuma
Kalu kuupeleka shambani. Nungunungu akiingia
mtegoni hataweza kutoka nje.
46
Kalu na babu wamefika shambani.Wameuendea
mtego. Mtego umeharibiwa na nungunungu.
Hauwezi kunasa chochote. Babu anashangaa.
Kalu anashangaa zaidi.
Babu amejificha shambani. Ana uta na mishale
mingi. Anamwona nungunungu. Anavuta uta na
kuachilia mshale.Anamwona nungunungu akiruka
juu na kuanguka.Anadhani amemuua nungunungu.
“Kalu…Kalu…Kalu...njoo umwone nungunungu,
babu anaita. Kalu anafika. Wote wanaenda
alipoanguka nungunungu. Hawamwoni. Mshale
wa babu umekatika na kuharibika. Nungunungu
ametoroka.
“Babu, mwalimu wetu husema umoja ni nguvu.
Hebu tufikirie. Tufikirie njia bora ya kumshika
nungunungu.Watu wawili ni bora kuliko mmoja,
Kalu anaeleza.
Babu na Kalu wamefika msituni. Wamechuma
majani na mizizi.Wametengeneza dawa ya mizizi.
Ni dawa aliyoitumia babu alipokuwa kijana.
Ni dawa ya kumwangamiza nungunungu.Kalu
anafukua mahali penye muhogo.Anaupaka dawa
hiyo.Anafukia mchanga na kuondoka.
47
Anaenda penye bwawa. Anachota maji kwa
kibuyu.Anayaweka karibu na mihogo.
Babu analeta mtego mwingine.Anauweka katikati
ya mihogo.Wanaondoka shambani.
Nungunungu amemaliza kula mihogo. Ameshiba
sana. Hana nguvu. Hawezi kutembea.Anahisi kiu.
Anayanywa maji yote. Hajijui. Ameona nyumba
ya vijiti vingi.Ameingia ndani na kulala.
48
Kalu na babu wamefika shambani. Wamevalia
ngozi za chui.Ngozi ni kinga yao.Wamefika penye
mtego. Wamemwona nungunungu. Nungunungu
amekwama mtegoni.
49
Nungunungu ana hasira. Amewaona Kalu na
babu. Ameachilia miba kwa hasira. Lo! Miba
mitano imempata babu. Mingine imempata Kalu.
Imemchoma ngozi ila haijawaumiza.
Babu na Kalu wanaenda nyumbani kwa Fundi
Kololo. Kalu na babu wamefika. Wanazungumza
na Fundi Kololo.Wamebeba ule mtego. Ndani ya
mtego kuna nungunungu.
“Fundi, wewe ni mfugaji wa nungunungu.
Tumekuletea mmoja. Amekuwa msumbufu.
Amekula mihogo yetu yote, babu anaeleza.Kololo
ana furaha.Anauchukua mtego na kuuweka chini.
“Asanteni sana. Serikali imenipa ruhusa ya kufuga
wanyama kama hawa. Mkipata wengine nileteeni.
Wanasumbua lakini msiwaue. Kuua wanyama si
kuzuri. Wanyama ni utajiri wa nchi yetu, Fundi
Kololo aliwaambia.
Kalu na babu wanaelekea nyumbani.Wote wana
furaha.Nungunungu hatawasumbua tena.Mihogo
ya baba na mama itakuwa mingi. Kalu na baba
watakunywa chai kwa mihogo asubuhi.
50
Jibu maswali yanayofuata.
1. Kwa nini wazazi wake Kalu hawakuwa na
furaha wakiwa shambani?
2. Unafikiri ni kwa nini Kalu na babu yake walivalia
ngozi ya chui?
3. Kwa nini Kalu na babu yake walimpeleka
nungunungu kwa Fundi Kololo?
4. Unafikiri ni kwa nini si vizuri kuwaua
wanyamapori?
5. Hadithi hii imekufunza nini? Mweleze mzazi au
mlezi wako.
51
Katana Mchafu
52
Ilikuwa ni siku ya Jumamosi saa tatu asubuhi.
Katana hakutaka kuamka. Alikuwa mvulana
mvivu sana.
Maria aliingia chumbani. Alimwamsha Katana
lakini akakataa katakata kuamka. Katana
alipenda sana usingizi.
53
Baada ya muda mfupi, Katana aliamka. Alienda
sebuleni na kupata mkate kwa chai. Alianza
kula bila kunawa mikono. Alikula mkate mzima
akabakisha kipande kidogo sana.
Maria alikuwa nje akifua nguo. Maria aliachiwa
kazi ya kufua. Katana aliachiwa kazi ya kufagia.
Katana hakutaka kufanya kazi.
54
Katana alienda kwenye ghala. Alifungua na
kuingia ndani. Alikuwa na furaha sana. Alipata
ndizi za mama zilikuwa zimeiva. Alichukua ndizi
kumi. Aliona muwa mrefu na kuuchukua. Katana
alikula ndizi akitupa maganda ovyo. Alipomaliza,
hapo palijaa maganda mengi.
Maria alimshauri aokote. Katana alikataa
kuyaokota. Aliposhiba alichukua mpira wake.
Alienda kucheza uwanjani. Baada ya kucheza,
Katana alirudi kula muwa.Alichafua mahali pote
pakajaa maganda. Aliondoka akarejea uwanjani.
Alicheza mchana kutwa. Alijichafua sana. Kufikia
jioni alichoka sana.
Katana alianza kurudi nyumbani. Ilikuwa ni jioni.
Jua lilikuwa limetua. Giza lilianza kuingia. Nyota
zilionekana angani. Pia mwezi ulionekana angani.
Katana alitembea haraka.Alikuwa na woga.
“Maria kwa nini hukufagia? Wataka baba na
mama wakasirike?” Katana aliuliza.
“Haikuwa kazi yangu kufagia. Mimi nilifua sare
zetu. Wewe uliketi kula. Umechafua kila mahali.
Mama na baba wakija watakuadhibu, Maria
alijibu.
55
Lango lilifunguliwa. Baba na mama waliingia
katika nyumba. Walikuwa wamechoka. Mama
alienda jikoni. Alitaka kupika chakula haraka.
Katana hakuwa karibu. Alikuwa katika chumba
chake cha kulala. Alidanganya kuwa alikuwa
anasoma.Hakutaka kuwa karibu na wazazi wake.
Alinuka jasho.
56
Baba alikaa sebuleni.Mama alikuwa jikoni akipika.
Maria alikuwa sebuleni akisoma hadithi.
Mama alimaliza kupika na kupakua chakula.
Alikileta mezani. Katana aliitwa. Alikaa mbali na
wazazi.Aliketi karibu na Maria.Alinuka vibaya.
“Katana, ulifanya kazi tuliyokuachia?” baba
aliuliza. Katana hakujibu.Alinyamaza ji!
57
“Hakufanya kazi yoyote, alienda kucheza, Maria
alimwambia baba.
“Katana, leo ulioga?” Mama alimuuliza. Katana
alinyamaza.Alitazama chini kwa aibu.
“Nilimwambia aoge akakataa, Maria alisema
bila woga.
Baada ya chakula cha jioni, kila mmoja alienda
kulala. Katana alilala fofofo! Alikoroma kama
chura wakati wa mvua. Alienda haja ndogo
kitandani. Godoro lilichafuka. Shiti ilichafuka.
Blanketi lilichafuka.
“Uuuuuui! Uuuuuui! Mama wee! Mama njoo…
Baba njoo…. Maria njoo… Ninaumwa mama,
ilikuwa sauti ya Katana. Alikuwa akilia sana.
Alipiga yowe asaidiwe.
Baba aliamka. Mama aliamka. Maria aliamka.
Walisikia sauti ya Katana. Walitoka mbio.
Walienda chumbani mwa Katana. Hawakujua
ni nini kilichotokea. Walidhani Katana alikuwa
akiota ndoto mbaya.
Baba aliufungua mlango. Mama aliwasha taa.
Walimpata Katana ameshatoka kitandani.
Alikuwa sakafuni.Aliruka kama mcheza ngoma.
58
“Mama yangu wee…” Katana aliendelea kulia.
Mama alimwangalia. Aliona siafu mgongoni.
Baba alitazama chini. Aliona siafu wengi. Maria
aliangalia chini. Siafu walikuwa kila mahali.
“Nitoe baba…Nitoe wote mama.Maria,toa wote
kabisa, Katana alisema. Walimtoa siafu wote.
Katana alilia kwa maumivu mengi.
59
Walimtoa Katana chumbani. Waliwaona siafu
sebuleni. Waliwaona siafu jikoni. Chumba cha
Maria kilikuwa na siafu. Na chumba cha wazazi
je? Pia kilikuwa na siafu. Nyumba yote ilikuwa na
siafu.
Mama alitoka. Alitaka kwenda jikoni. Ghafla
aliteleza akaanguka. Aliteguka mguu wake wa
kulia. Alikanyaga ganda la ndizi. Baba alimsaidia
kusimama. Mguu wa mama uliuma sana.
Baba aliingia jikoni. Alichota jivu jingi. Aliweka
jivu kila mahali. Aliweka kote nje. Aliweka katika
vyumba. Hakuna mmoja alirudi kulala. Ilikaribia
alfajiri.
Asubuhi ilifika. Katana alikamata ufagio. Alifagia
nje ya nyumba.Alifagia maganda ya ndizi.Alifagia
maganda ya muwa.Alitupa maganda kwenye jaa.
Katana alioga akawa safi. Nguo zake zilikuwa
safi. Alianza kuupenda usafi. Hakutaka kuumwa
na siafu tena. Baba alimpenda. Mama alimpenda.
Maria alimpenda. Kila mmoja alimpenda.
60
Jibu maswali yanayofuata.
1. Unafikiri ni kwa nini Katana hakutaka kuamka?
2. Kwa nini Katana alijifungia katika chumba
chake cha kulala?
3. Unafikiri ni kwa nini siafu waliivamia familia ya
Katana?
4. Ni kwa nini mama yake Katana aliteleza na
kuanguka?
5. Ikiwa Katana angekuwa rafiki yako, ungempa
ushauri upi? Kwa nini?
61
Kizito
62
Sote tulikuwa darasani. Mwalimu wa somo la
Kiswahili, Bi Upendo aliingia.Alikuwa na mvulana
mgeni. Mvulana huyo alivalia sare mpya na
nadhifu. Usafi wake ulipendeza sana.Wengi wetu
tulianza kucheka.Tulicheka tukitazama chini.
63
“Hamjambo wanafunzi?” mwalimu alituamkua.
“Hatujambo. Shikamoo mwalimu?”
“Marahaba wanafunzi. Leo tuna mgeni. Hebu
tumkaribishe kisha tumruhusu atuambie anaitwa
nani.
Mvulana huyo alimtii mwalimu na kuanza
kujitambulisha. Sote tulishindwa kujizuia kucheka.
64
“Jina langu ni Kizito, alianza kuongea. Kila
mwanafunzi alicheka sana. Mbavu zangu ziliuma
kwa kicheko.
“Mnacheka nini?” Bi Upendo alituuliza kwa hasira.
Kila mmoja alinyamaza ji! Mwalimu alimwonesha
Kizito mahali pa kukaa. Alipoketi sote tulicheka
tena. Wakati wa kwenda kucheza ulifika. Sote
tulienda uwanjani. Kizito alitufuata. Alitembea
polepole kwa shida. Alikuwa mnene kupita kiasi.
Alibeba mkebe mkubwa wa chakula. Tulipoanza
kucheza, aliketi na kuanza kula.
Kizito alikula keki. Alikunywa soda akamaliza.
Alisimama akitaka kucheza. Aliporushiwa mpira,
alijaribu kuupiga. Aliteleza na kuanguka. Aliumia
mguu wake.
Hakuna mwanafunzi aliyeweza kumbeba Kizito.Bi
Upendo alikuja kumsaidia. Kizito alikuwa amelia
sana. Hakuwa ameumia sana. Alikwaruzwa
kidogo na jiwe.
Wakati wa kwenda nyumbani ulifika.Sote tulianza
kulifagia na kuliosha darasa. Kizito alipoinama,
alianguka kwa kishindo sakafuni pu!
65
Tulimzunguka na kucheka.Tulimwimbia wimbo.
Kanono! Kanono! Kanono! Kanono!
Umeshiba mno! Umeshiba mno!
Punguza unene wako! Punguza unene wako!
Unene ni hatari! Unene ni hatariiii!
Kizito alianza kulia. Hatukujali. Tuliendelea
kulisafisha darasa.Wakati wa kwenda nyumbani,
hakutoka darasani. Baadaye mjakazi alikuja
kumchukua. Aliendesha gari zuri sana. Kizito
hakutembea kwa miguu kama sisi. Alizoea
kubebwa kwa gari.
Siku iliyofuata, mama yake Kizito alikuja shuleni.
Alikuwa na hasira sana. Aliingia katika afisi ya
Bi Upendo. Alikaa huko sana. Baadaye, alikuja
darasani pamoja na mwalimu. Baada ya salamu,
Bi Upendo alimtambulisha mgeni.
“Mimi na mgeni hatuna furaha hata kidogo.
Kizito alisema kuwa mlikuwa mkimcheka. Hata
alipoumia hamkumsaidia. Ni vibaya kucheka
watu wengine. Kuanzia leo Kizito asichekwe!
Mnasikia?”
“Ndiyo mwalimu, sote tuliitikia.
66
Tulifanya mtihani. Ulikuwa mtihani wa kati ya
muhula. Kila mwanafunzi alifanya bidii. Matokeo
yalitangazwa. Lo! Kizito alikuwa nambari moja!
Sote tulimshangilia kwa kumpigia makofi. Bi
Upendo alimtuza vitabu viwili vya hadithi na
kalamu.
67
Siku moja tulienda kukimbia. Bi Upendo alisema
tuzunguke uwanjani. Kizito alianguka akikimbia.
Mwalimu alienda kumsaidia.Alikuwa akihema
68
kwa nguvu.Alipumua kwa shida.
Kizito alipelekwa hospitalini. Daktari alisema
kuwa Kizito alisumbuliwa na unene.Alihitaji kula
chakula kifaacho na kufanya mazoezi.
Kizito alirejea shuleni. Nilianza kuona tofauti.
Kizito hakubeba keki tena. Alibeba tunda moja
na pakiti ya maziwa. Wakati mwingine alibeba
muhogo au kiazi kitamu.Alianza kula vyakula vya
kiasili.
Bi Upendo alimsaidia Kizito. Alimhimiza kufanya
mazoezi. Kizito aliyapenda mazoezi. Alikimbia
mita hamsini na kurudi. Alikimbia hadi jasho
likamtoka. Kizito alipunguza uzito polepole. Sote
darasani tulishangaa.
Kizito hakuchukuliwa shuleni kwa gari tena.
Alizoea kutembea kama sisi. Alikuwa akitembea
hadi nyumbani.Alitembea asubuhi na jioni.Ulikuwa
mwendo wa kilomita tatu kwenda na kurudi.
Alifika shuleni asubuhi na mapema kila siku.
Muhula wa tatu ulifika. Mwili mnene wa Kizito
uliisha. Alikuwa mvulana tofauti. Hakuwa Kizito
tuliyemcheka. Alikuwa na nguvu nyingi. Alikuwa
mchezaji mzuri wa soka.Tabia zake zilikuwa nzuri.
69
Kizito aliingia katika timu yetu ya soka.Alionesha
uhodari mkubwa. Alimchenga kila mtu. Alifunga
mabao mengi. Wanafunzi walimshangilia.
Nilitamani kujua kucheza soka kama Kizito.
Alikubali kunifunza kandanda.
Mashindano yaliandaliwa. Timu yetu ingecheza
na timu ya gredi ya nne. Kizito alituambia kuwa
tusiogope. Mwalimu alimchagua Kizito kuwa
nahodha. Sote tulifurahia kuongozwa na Kizito.
Siku ya mashindano ilifika.Uwanja ulijaa mashabiki.
Kulikuwa na mtangazaji. Mtangazaji alikuwa
akitangaza mpira. Mechi ilianza. Sote tulishangilia.
Timu yetu ilikuwa nzuri. Ilicheza kwa bidii. Kipindi
cha kwanza kiliisha na cha pili kikaanza. Ghafla
Kizito aliupata mpira.
“Kizito…Kizito na mpira. Kizito anasonga.
Kizito anawachenga wenzake. Moja…mbili…
tatu...Kizitoo…karibu na lango…. Ana…
Gooooooooooooool! Kizito amefunga bao la
ushindi, mtangazaji alipaza sauti.
70
Sote tulishangilia. Hata walimu walirukaruka kwa
furaha. Kizito alikuwa amepiga mkwaju mzito.
Kipa alishindwa kuushika. Lilikuwa bao zuri.
Sitalisahau bao hilo la Kizito. Kizito alipongezwa
71
na kusifiwa. Alibebwa juu juu. Sote tulimwimbia
wimbo. Ulikuwa wimbo wa ushindi.
Kizito! Kizito! Kizito ni weeetu!
Kizito! Kizito! Kizito ni wetu mshindiii!
Niliamini hakuna jambo lisilowezekana. Mtu
akiwa na nia, hakuna lililo gumu. Kizito alichukia
unene.Alifanya mazoezi kwa bidii.Alikula vyakula
vizuri. Alikuwa mchezaji bora. Aliipatia timu yetu
ushindi.
72
Jibu maswali yanayofuata.
1. Kwa nini wanafunzi walikuwa wanamcheka
Kizito alipokuwa anaingia darasani na Bi
Upendo?
2. Unafikiri ni kwa nini Bi Upendo na mama yake
Kizito hawakuwa na furaha hata kidogo?
3. Bi Upendo alimtuza Kizito kwa kumpa nini?
Mbona alimtuza?
4. Wewe unapenda kucheza mchezo upi?
5. Hadithi hii inakufunza nini? Mweleze mzazi au
mlezi wako.