
3
maskini asiye na mbele wala nyuma. Katika ile hali ya
uchochole, Gambo alijipata yu miongoni mwa kundi la
vijana ambao walirandaranda ovyo mijini wakitafuta riziki
kwenye majaa ya taka. Vilevile, katika ‘siku takatifu’
alivyoiita Gambo, angekimbia kwenye mkahawa na
kununua kopo la uji katika mkahawa wa Makangati.
Hiyo ni siku ambayo angepata msamaria mwema ampe
angalau shilingi tano. Makangati, mkahawa maarufu
katika mtaa wa Rabeki, ulisifika sana hasa kwa mapishi
yake mazuri na vyakula ainati kama ‘hawhaw’ yaani
dagaa wa kukaanga, ‘ugali macho’ yaani ugali kwa mayai
na uji moto. Licha ya vyakula vingi kuwepo, vyakula
hivyo viliuzwa kwa bei nafuu sana. Hilo ndilo lililofanya
Makangati kuwameza wateja sufufu pasi na kuwatema
hadi pale walipomaliza kuhudumiwa.
Kitaka, mwanamume aliyekuwa kidurango, mnene
kwa kimo na mwenye pua iliyochongoka, alikuwa mmoja
kati ya wahudumu katika mkahawa ule ulioitwa Makangati.
Aliifanya kazi yake kwa dhati na imani kuliko wahudumu
wengine. Utendakazi wake uliongeza nguvu sumaku ya
kuwavutia wateja katika mkahawa ule.
Kila wakati Gambo alipoangukiwa na nyota ya
jaha na kupata hela, alimkuta kisadfa yule Kitaka akiwa
mhudumu wa zamu. Hivyo basi ikawa ni bahati maradufu
kwake Gambo. Kwanza Kitaka angemtilia uji mwingi zaidi
ya kipimo cha kawaida. Pia, angempa masalia ya chakula
walichokuwa wamekila wateja na kusaza.
Wawili hao wakawa wanakuza uhusiano wa karibu
uliokua na kuwa urafiki wa kupigiwa mfano. Urafiki
wa Kitaka na Gambo – mtu mzima na mtoto! Ajabu.