Dolfina
na Hadithi Nyingine
Pauline Kea
Dolfina na Hadithi Nyingine
Kimechapishwa na Queenex Publishers Limited
S.L.P 56049-00200, Nairobi, Kenya.
Simu: 0727 794 498, 0715 808 200
Baruapepe: info@queenexpublishers.co.ke
queenexbooks@gmail.com
Tovuti: www.queenexpublishers.co.ke
© Pauline Kea, 2022
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili,
kupigisha chapa, kutafsiri au kutoa kitabu hiki kwa jinsi
yoyote ile bila idhini kwa maandishi ya Queenex Publishers
Limited.
ISBN: 978-9966-141-95-8
Chapa ya kwanza 2022
1
Kijiji cha Kijani
2
Kijiji cha Kijani hapo mwanzoni kiliitwa Kijiji Kikavu. Jina hili
lilitokana na ukame wa kila mara uliokikumba kijiji hicho.Visima
vilikauka na chakula kiliadimika miaka nenda rudi. Umaskini
ulikita mizizi katika Kijiji Kikavu.Viongozi walijaribu kutafuta
suluhisho la umaskini huu bila mafanikio. Suluhu waliyoipata
ilionekana kuwa ya muda tu.Waliomba misaada ya chakula
na kuwagawia wanakijiji ukame na njaa vilipozidi. Wakati
mwingine wafadhili wao walichelewesha misaada hiyo.
Dhiki ya njaa na kiu ilizidi na kusababisha vifo vya watu
na mifugo. Wanakijiji walikonda kama ng’onda. Wengine
mbavu zao zingehesabika. Walisononeka huku wakimlilia
Mungu awaokoe.Watoto walikosa kwenda shuleni, wakabaki
nyumbani wakiyahangaikia matumbo yao. Siku ya msaada
kufika wanakijiji walirauka na kupanga foleni ili kupokea
chochote kidogo walichokuwa wameletewa. Fujo zingezuka
iwapo msaada huo haungemfikia kila mmoja wao.
Assa, nyanya yake, na Kalama walijipata wamenaswa katika
utandu huu wa umaskini.Assa alizaliwa na kukulia Kijiji Kikavu.
Maisha yake tangu utotoni yalikuwa ya taabu. Kwanza kabisa,
alifiwa na baba yake akiwa kikembe. Baba yake Assa ndiye
aliyekuwa tumaini la familia yao.Alitegemewa kwa kila kitu.
Hata Kalama alimtegemea baba yake Assa amlipie karo. Baba
yake Assa alikuwa mwalimu wa shule ya upili mjini. Kila mwisho
wa mwezi alihakikisha kuwa amewanunulia watu wake chakula
cha kutosha na aliwatumia pesa za matumizi. Maisha siku hizo
yalikuwa afueni. Baba yake Assa alifariki kwa ajali mbaya ya
barabarani. Kifo chake kiliombolezwa na wengi huko mjini na
kijijini. Mjini walilia wakisema kuwa walikuwa wamempoteza
mwalimu mzuri. Kijijini walihuzunika kwa kumpoteza mtoto
wao mwenye bidii na heshima.
3
4
“Pole sana, Mariamu. Umepoteza mboni ya jicho lako. Kufiwa
na mtoto ni jambo zito. Kifo cha Nyae kimenitia simanzi nyingi,
alisema mama mmoja rafiki ya nyanya yake Assa.
Siku ya mazishi yake shughuli zote kijijini zilisimama ili
kumsindikiza. Wanakijiji walikuwa wana sababu zote za
kumlilia. Baba Assa alikuwa ameanzisha mradi mkubwa wa
kusambaza maji hapo kijijini kwao. Alitumia mbinu nyingi
kuona kuwa amepata ufadhili wa kuchimba visima kijijini kwao.
Kabla ya kukutana na kifo chake, alikuwa tayari amechimba
visima viwili vya maji.Alipofariki visima hivyo vilipewa majina
yake kama njia ya kumkumbukia. Kimoja kiliitwa Baraka na
kingine kikaitwa Nyae. Baba yake Assa alipoaga dunia tu,
Kalama aliacha kwenda shuleni. Alianza kuichumia familia
yake. Nyanya yake Assa aliuza mbuzi wachache waliokuwa
hapo nyumbani. Alichukua mkopo kutoka kwa chama cha
kina mama.Alijumuisha pesa zote na kumnunulia mwanawe
Kalama tukutuku ili afanyie biashara ya uchukuzi. Hela
chache alizopata kila siku ndizo zilizokidhi mahitaji ya familia
yake. Pesa hizo pia zililipia mkopo. Hazikuwa hela za haja bali
zilikuwa ni pesa za kijungujiko tu!
Mama yake Assa naye alifariki Assa alipoanza kuzungumza
neno mojamoja.Aliugua ugonjwa wa msongo wa mawazo. Hii
ni hali ya kuwa na mambo mengi mazito akilini. Hakuna aliyejua
anaugua nini mwanzoni.Alipokwenda hospitalini na kupimwa,
hakupatikana na ugonjwa wowote. Alipozidiwa, alilazwa
hospitalini. Hapo ndipo ugonjwa wake ulipogunduliwa, lakini
alikuwa tayari amedhoofika kupita kiasi. Daktari alisema,Heri
kufa mwili kuliko kufa akili. Mama yake Assa amekwishajua
akili yake. Nasikitika. Lazima tuanze kushughulikia gonjwa hili la
msongo wa mawazo mapema. Limekita sana katika ulimwengu
wetu. Ni gonjwa hatari. Linaua kimyakimya. Halionekani kwa
vipimo katika maabara. Nafikiri kifo cha baba yake Assa
kimemsumbua sana mkewe.
5
Ganga ganga za mganga hazikuleta matumaini. Mama yake
Assa alikata roho baada ya siku mbili.Assa alibaki yatima.
Alilelewa na walezi wake, yaani, nyanyake na Kalama.
Assa hakudiriki kumfahamu mama yake sana.Alimjua sura
alipoerevuka. Alionyeshwa picha zake kwenye mitandao ya
kijamii.
Assa alipungukiwa na vitu vingi.Wakati mwingine hata kupata
mavazi mazuri ya kuusitiri mwili wake ilikuwa vigumu.Alitamani
vitu vingi ambavyo alihitaji kutumia shuleni pia.
“Nyanya, tafadhali ninunulie rangi za kupaka michoro yangu,
Assa alimwomba nyanya yake.
“Sina hela, mjukuu wangu. Pesa kidogo anazopata ami yako
ni za chakula. Rangi hailiwi, mjukuu wangu. Tushibe kwanza.
Mengine yatakuja kwa majaaliwa, Nyanya alimjibu Assa kwa
sauti ya huzuni.
“Sawa, Nyanya, Assa alikubali shingo upande.
Assa alikuwa na uhusiano wa karibu sana na baba yake mdogo.
Kalama naye alimtunza na kumpenda Assa kama mwanawe
wa kumzaa.Alimhimiza Assa kusoma kwa bidii kila wakati.
“Soma kwa bidii, Assa. Mimi hutamani sana kurudi shuleni.
Najua siku moja nitamaliza masomo yangu tu.
“Natia bidii ya mchwa masomoni, baba mdogo. Nataka siku
moja niendeleze mradi wa maji ambao baba yangu alianzisha.
Nataka pia niibadilishe hali ya kijiji chetu iwe bora, Assa
alimwambia Kalama.
“Hilo ni wazo zuri, Assa. Kama tungekuwa na uwezo bila
shaka tungebadilisha hali katika kijiji chetu. Nimechoshwa na
umaskini, alisema Kalama.
6
“Mwalimu wetu alituambia kuwa umaskini wetu uko kwenye
akili zetu. Alisema kuwa ukitaka kutajirika lazima ubadilishe
namna unavyowaza. Alisema kuwa ukiamini kuwa unaweza
kutajirika utatajirika.
“Alisema vizuri mwalimu wenu. Napenda anavyowashauri na
kuwatia moyo. Ila lazima ujue kuwa kuna kuamini na kutenda.
Imani bila matendo haileti mabadiliko yoyote, alisema Kalama.
“Ni kweli, baba mdogo. Lazima tufanye jambo. Sijui tufanyeje,
kwa kuwa uwezo wetu ni mdogo, alisema Assa.
“Kubadilisha mambo madogo kunaweza kusababisha
mabadiliko makubwa baadaye. Kwa mfano, nina imani kuwa
wanakijiji wakiungana na kupanda miti, tunaweza kubadilisha
mazingira yetu. Mifugo wetu watapata lishe wawe wenye afya
bora.Tukiwa na mifugo wa kutosha tutauza na hali ya uchumi
itaimarika.Wanakijiji wamepuuzilia mbali suala hili la upanzi
wa miti. Kila wakati wanatoa vijisababu. Mara wanasema
kuna ukame, mara miche haipatikani, almradi wanasema kitu
tu. Kisha miti michache iliyoko bado wanaikata na kuichoma
makaa, alielezea Kalama.
“Hata mwalimu wetu anatuhimiza kupanda miti. Miti michache
ambayo tumepanda shuleni imeyabadilisha mandhari. Sijui ni
kwa nini wanakijiji hawawezi kuona wakaiga mfano huo?”
“Wanakijiji ni wewe na mimi, usisahau hivyo.Wewe mwenyewe
umepanda miti mingapi tangu kuzaliwa? Hapa nilipo nafikiri
sijafikisha hata mitano.Tukitaka mabadiliko, tuanze sisi wenyewe.
Watu wengine wataiga, alisema Kalama.
“Kijishamba chetu ni kidogo. Miti tutapanda wapi?” aliuliza Assa.
“Si lazima upande hapa kwetu nyumbani. Unaweza ukapanda
miti hata kwenye viwanja vya umma na kando ya barabara.
7
Hakuna atakayekukataza. Ni vivuli vingapi ambavyo vimekusitiri
jua na miti yake hukuipanda wewe?” aliuliza Kalama.
“Vingi, baba mdogo. Mafundisho yako ni mazuri. Hoja yako ni
muhimu, alijibu Assa.
Assa na Kalama waliamua kuanza kubadilisha mambo
polepole. Kwanza waliamua kutafuta mbinu mpya za kutumia
ili kuboresha biashara ya tukutuku ili familia yao iwe na
mapato zaidi.
Siku moja,Assa alimwomba Kalama simu.Alisakura mtandaoni
ili apate maana ya maneno mapya. Mara aliona habari
zilizomvutia macho zimejitokeza. Alikimbia kwa Kalama na
kumwonyesha.
“Waonaje, baba mdogo? Tutajaribu?” Assa aliuliza huku
akimwonyesha ami yake picha kwenye mtandao.
“Kujaribu ni kuzuri lakini mbegu tutatoa wapi?” Kalama
alimuuliza Assa.
“Kuna miche michache shuleni. Nitamwomba mwalimu miwili,
Assa alisema.
Assa alimwomba mwalimu miche akapewa. Alisaidiana na
Kalama kuipanda vizuri katika mikebe.Walifuata hatua zote
za upanzi walizosoma kwenye mtandao.Walitayarisha mahali
pazuri pa kuweka mikebe yao nyuma ya tukutuku.Waliwekelea
mikebe kwenye funiko ndogo za ndoo ili isivuje huko nyuma
ya tukutuku. Kila siku walitia miche maji. Miche ilianza kukua
kwa kasi. Mwanzoni hakuna aliyegundua kuwa kuna miche
iliyopandwa kwenye tukutuku.Abiria waliabiri na kushuka bila
habari. Baada ya muda miche ya mkarakara ilianza kutambaa.
Ilikua kwa kasi ya ajabu. Punde si punde tukutuku nzima
ilifunikwa na matawi na majani ya mkarakara. Mara pia
8
maua yalichanua.Watu walianza kuulizana maswali walipoiona
tukutuku ya Kalama.Wengine waliona ni kama kioja.Wengi
waling’ang’ania kubebwa na tukutuku ili wajionee wenyewe
asili ya maajabu hayo ya tukutuku kumea miti.
Kalama alipata abiria wengi ajabu. Mapato yake yaliongezeka
maradufu. Abiria walisema kuwa walipendelea kuabiri
tukutuku ya Kalama kwa kuwa ilikuwa na hali ya ubaridi
wakati wa jua kali. Majani ya mkarakara yalizuia makali ya
jua kuwafikia abiria. Assa alifurahia na kuajabikia mafanikio
haya.
Madereva wale wengine walipoona hivyo, hata nao walifanya
kama Kalama. Walitafuata miche ya mikarakara na miti
mingine myepesi itambaayo wakapanda kwenye tukutuku
zao. Kituo kizima cha tukutuku kiligeuka rangi baada ya
muda. Kilionekana kijani kibichi. Tukutuku zilibeba karakara
na vitango vidogo. Watu walizipiga picha tukutuku hizi bila
kuamini.Wengine waliziweka kwenye mtandao.
Kijiji Kikavu kilianza kutia fora.Watalii kutoka mbali walifika
Kijijini hapo kutembelea kituo hicho cha tukutuku.Waliabiri
tukutuku hizo na kupigwa picha wakiwa humo ndani kwa
malipo. Hali ya uchumi ya Kijiji Kikavu ilianza kuimarika.
9
10
Viongozi wa Kijiji Kikavu walianza kupata matumaini.Walianza
tena kufanya kampeni za upanzi wa miti. Walitumia mfano
wa kituo hicho cha tukutuku kuonyesha jinsi ambavyo upanzi
wa miti yoyote ile ulivyo na manufaa. Wazee wa mtaa na
viongozi wa Nyumba Kumi waliwahimiza watu kupanda miti
popote pale walipokuwa. Miti ya kila aina ilipandwa kijijini
kwa muda mfupi. Wanakijiji walifunzwa mbinu za kisasa za
ukulima. Waliweza kutumia sehemu ndogo ya shamba na
maji kidogo kupata mavuno mengi. Viongozi wa Nyumba
Kumi walihakikisha kuwa watu wanatunza miche na mbegu
wanazopanda.Walianzisha sera mpya ya kupanda miti. Sera
hiyo ilimtaka kila mwanakijiji kupanda miti kulingana na umri
wake.Assa kwa mfano, alitakiwa kupanda miti kumi, kwa kuwa
alikuwa na miaka kumi. Hata hivyo, tayari yeye na ami yake
walikuwa wamepanda miti zaidi kuliko vile ilivyohitajika. Sera
hiyo pia ilipiga marufuku ukataji miti. Mtu alihitajika kupata
kibali maalum ili kukata mti, hata kama mti huo ulikuwa
shambani mwake.Waliokata miti ovyo walishtakiwa.
Maafisa wa kilimo walitumwa kijijini ili kuwaelimisha wanakijiji
kuhusu mbinu mwafaka za kilimo.Wakulima wengi walianzisha
kilimo-biashara. Nyanya yake Assa alianzisha kilimo cha
mboga za kienyeji. Alipanda mchicha, mabenda na kitunguu
cha majani. Wakulima wengine walipanda miti ya matunda.
Walishirikiana na kutayarisha miche spesheli ili miti yao
isitumie maji mengi kukua. Baada ya muda, Kijiji Kikavu kilianza
kubadilika. Kiligeuka na kuwa cha rangi ya kijani.
Kijiji Kikavu kilipata sura mpya.Wadudu na wanyama wadogo
wadogo ambao awali walikuwa wamehama walirudi.Vipepeo
wa rangi za kila aina waliruka na kuyapamba mandhari ya kijiji
hicho. Nyuki walionekana na kushughulika na uchumaji nekta.
Assa aliwaona nyuki hao alimwuliza nyanya yake,“Naweza
kufuga nyuki nipate asali?”
11
“Unaweza, lakini utahitaji msaada wa mtu mzima, nyanya
yake alimjibu.
“Nitasaidiwa na baba mdogo, Assa alijibu.
Assa na Kalama walizungumza na maafisa wa kilimo waliokuwa
nyanjani siku hiyo. Walipewa habari zote kuhusu ufugaji
wa kisasa wa nyuki.Waliahidiwa kupewa mizinga miwili ya
majaribio.
Mizinga ya nyuki iliwasili wikendi.Assa ana Kalama walishirikiana
kuiangika mizinga hiyo mitini. Baada ya siku mbili nyuki
walikuwa tayari wameanza kuing’ong’a mizinga.Walijua kuwa
tayari nyuki walikuwa wameanza kufanya makao mizingani.
Assa na Kalama walipovuna asali waliwauzia wanakijiji.
Watu hawakuamini kuwa kijiji chao kingeweza kuvunwa asali.
Wakulima wengi waliagiza mizinga na kuitundika ili nao wapate
asali. Kilimo cha asali kilinoga kijijini.Wakulima walivuna asali
nyingi na kuiuza mijini.Assa na Kalama waliongezea mizinga
yao. Pesa walizozipata kutokana na kilimo cha asali waliamua
kuzitumia kupanulia biashara hiyo.
Maisha yalikuwa yamebadilika sana kijijini.Watu walionekana
wenye bashasha na afya. Mashamba yalikuwa yameimarika.
Mvua pia ilianza kunyesha vizuri kwa misimu yake.Wanakijiji
waliungana na kuchimba mabwawa ya maji. Walitumia
mabwawa hayo kunyunyizia mashamba yao na kunywesha
mifugo wao.Assa na Kalama waliamua kununua mbuzi wawili
ili wafuge.
“Nimefurahi kwamba mmeamua kufuga mbuzi. Nitatumia
mbolea kutoka zizini mwao kurutubisha shamba langu, Nyanya
alisema kwa furaha. Mbuzi wa Assa na Kalama walizaana
haraka wakawa wengi. Kalama aliamua kuuza baadhi yao.
12
“Pesa nilizozipata kutokana na mauzo ya mbuzi nitaziweka
kwenye benki. Ninataka kujisajili ili nifanye mtihani wangu
kama mtahiniwa wa kibinafsi, Kalama alimwelezea nyanyake.
“Ama kweli penye nia pana njia. Uamuzi wako ni wa busara.
Ninakutakia kila la heri, mjukuu wangu, Nyanya alisema.
Siku moja, Kalama alipata wageni akiwa kwenye maegesho ya
tukutuku yake.Wageni hao walimhoji na kumdadisi.Walikuwa
wameandamana na wanahabari tajika.
“Picha hii ni yako sio?” mgeni mmoja alimuuliza.
“Ni yangu, Kalama alijibu kwa woga. Hakujua kwa nini
alikuwa anaonyeshwa picha hiyo. Picha yenyewe ilikuwa ya
miaka miwili hivi iliyopita. Alikuwa kijana mdogo. Alikuwa
ameketi ndani ya tukutuku pamoja na Assa. Kalama alihofia
kuwa wageni wale walikuwa maafisa wa polisi.Alidhani kuwa
pengine alikuwa amekosea jambo siku hizo akiwa mdogo bila
kujua.Alifikiri labda alikuwa na shtaka la kujibu lililohusiana
na picha hiyo. Wageni walipoona kuwa Kalama alikuwa
ameingiwa na wasiwasi walijitambulisha kirasmi.
“Usitie hofu, ndugu. Sisi ni maafisa wa serikali.Tunafanya kazi
katika afisi ya rais wa nchi hii. Tumekuja kwako kukuletea
habari njema. Tunataka kuchagua watu ambao wataingia
katika mchujo wa Tuzo ya Rais mwaka huu. Uliteuliwa na
mjumbe wetu mmoja. Leo tumekuja kuthibitisha kuwa upo
na pia kuchunguza baadhi ya kazi ulizofanya.Tuelezee ufanisi
wako katika mambo uliyofanyia kijiji chako, alifafanua mmoja
wa wageni hao.
Kalama aliwaelezea kila kitu.Aliwaambia kuwa ufanisi wake
ulichangiwa sana na Assa.
13
“Assa ni mpwa wangu. Ni mtoto mdogo mwerevu na mwenye
bidii. Nawaomba pia mmhoji kuhusu tuzo hii, Kalama alisema.
Wageni hao waliandamana na Kalama hadi shuleni kwa akina
Assa.Wakati wa ruhusa fupi Assa aliitwa na mwalimu wake.
Alipomwona ami yake alijua kuna jambo.Alitamani liwe jambo
zuri. Na kwa hakika lilikuwa zuri. Wageni walijitambulisha
na kumhoji. Wanahabari walifanya kazi yao ya kurekodi.
Walipomaliza waliagana naye.
Assa na Kalama walimjuza Nyanya kuwa wangetangazwa
kwenye runinga. Usiku wa siku hiyo, wote watatu walikwenda
kwa jirani yao aliyekuwa na runinga kungojea habari. Jirani
yao aliwakaribisha vizuri.Wakati wa taarifa za habari,Assa na
Kalama walionekana katika runinga wakihojiwa. Mwanahabari
alimtambulisha Assa kama mtoto bomba naye Kalama kama
kijana bomba. Wote walifurahi fika. Nyanya na jirani yao
waliwapongeza.
“Hongereni kwa kazi yenu nzuri na kwa ujasiri wenu wa
kuzungumza wakati wa mahojiano, alisema mzee huyo jirani
yao.
14
15
Mahojiano haya yalizungumziwa kijijini siku nyingi.Wanakijiji
walijivunia Assa na Kalama.Waliwatembelea walipopata fursa
ili kuwapongeza.
Gavana wao alivutiwa sana na maendeleo ya kijiji hicho. Siku
ya kuadhimisha kwa siku ya mashujaa wa nchi ilipofika, Gavana
aliamua kwenda kuisherehekea katika kijiji cha Kijiji Kikavu.
Wakati wa Gavana wa kuzungumza ulipofika, aliwaita Assa
na Kalama kwenye jukwaa. Aliwapongeza na kuwapa fursa
ya kuwasalimu watu.Walipigiwa makofi na kushangiliwa.Assa
na Kalama walipoketi Gavana alianza mazungumzo yake,
“Nina furaha ya kibogoyo kupata meno leo. Kijiji hiki kimepiga
hatua kubwa kimaendeleo. Umaskini uliokuwa umewakodolea
macho umezikwa. Nyote ni mashujaa. Kijiji chenu kimekuwa
mfano mzuri wa kuigwa na vijiji na miji mingine ya kaunti yetu.
Ninawaonea wana Kijiji Kikavu fahari kubwa. Kijiji Kikavu
si kikavu tena. Ninaomba kuanzia leo tukiite Kijiji cha Kijani.
Twataka kijiji hiki kiwe na jina lenye kuleta matumaini. Majina
yana nguvu pia.
Watu walishangilia na kukubaliana na Gavana. Kuanzia siku
hiyo, kijiji hicho kiliiitwa Kijiji cha Kijani. Baada ya sherehe hiyo
Assa na Kalama waliandamana na Gavana kwenda ikulu ya
Rais. Huko walikabidhiwa zawadi zao na kutambuliwa kama
watu wenye kuleta mchango mkubwa katika jamii.
Siku kumi baada ya sherehe hizo za mashujaa Kalama alipigiwa
simu.Alitakiwa kuwasilisha stakabadhi zake na za Assa kwenye
afisi ya masuala ya nchi za nje. Kalama aliwasilisha kila kitu.
Alifahamishwa kuwa walikuwa wameteuliwa kuwa mabalozi
wa nchi yao kwenye kongamano kuu la kimataifa la mazingira.
Walitakiwa kujitayarisha vilivyo.Assa alitunga shairi fupi kuhusu
umuhimu wa kuhifadhi mazingira ili kuwezesha maendeleo ya
kiuchumi. Mwalimu wake Kiswahili alimsaidia.Alitaka kwenda
kuliwasilisha katika kongamano hilo.
16
“Nitaliwasilisha vipi shairi hili?Watu wengi hawaelewi Kiswahili,
Assa alimuuliza mwalimu wake.
“Usitie shaka. Katika makongamano ya kimataifa kuna
wakalimali ambao watafasiri ujumbe wa shairi lako kwa
lugha yoyote ile itakayotakikana, mwalimu alimjibu Assa.
Safari ya Assa ya kwenda ng’ambo ilizungumziwa sana shuleni.
Wanafunzi wenzake walimuuliza maswali mengi.Assa alijibu
maswali ambayo aliweza. Wanafunzi wenzake walitamani
kusafiri kwa ndege kama yeye.
“Nimefurahi sana. Sikujua kuwa siku moja nitaabiri ndege.
Tena siku za kusafiri ni nzuri. Itakuwa wakati wa likizo kwa
hivyo sitakuwa na wasiwasi wa kukosa masomo, Assa alisema
alipofika nyumbani.
“Anayejitahidi hufaidi, mjukuu wangu. Umeanza kuvuna
matunda ya bidii yako, Nyanya alisema.
Siku ya kusafiri ilikuwa yenye shamrashamra nyingi. Nyanya
aliwaandalia Assa na Kalama karamu ndogo. Mcheza kwao
hutuzwa eti! Aliwaalika majirani wakala na kunywa. Jioni,
Nyanya na jirani yao mmoja aliwasindikiza Assa na Kalama
hadi mjini. Walipofika kwenye uwanja wa ndege waliagana.
Assa na Kalama waliahidi kuwa mabalozi wazuri wa mazingira
wa nchi yao.Walitarajia kusafiri kwa ndege ya usiku.
17
Kamusi Yangu
afueni nafuu
fahari kujivunia jambo zuri ambalo mtu
amelitenda
hakudiriki hakufanikiwa
kiliadimika kilikosekana kabisa
kung’ong’a kutoa sauti kama vile za nzi
wanaposhtuliwa na kuruka kutoka pale
walipo
maabara mahali pa kuchunguzia vipimo ili
ugonjwa ujulikane
maradufu mara mbili kwa idadi
mzongo fikira nyingi akilini zinazoweza
kusababisha ugonjwa
utandu hali ngumu au mbaya ya maisha ambayo
humkumba mtu asiweze kujitoa
yatima mtu aliyefiwa na wazazi
vimetusitiri vimetukinga kutokana na mambo mabaya
zilizokidhi zilizotimiza
18
Maswali
1. Kwa nini Kijiji cha Kijani kilipewa jina tofauti hapo zamani?
2. Kifo cha baba yake Assa kiliathiri vipi maisha ya familia
yake?
3. Kalama aliipata tukutuku yake kwa njia gani?
4. Assa alipata wazo la kuweka miti ya mikarakara kwenye
tukutuku wapi?
5. Kwa nini abiria walipendelea tukutuku ya Kalama?
6. Assa na familia yake walitumia mbinu gani kuboresha hali
yao ya maisha?
7. Fafanua sera mbili ambazo zilisaidia kuongezeka kwa miti
katika kijiji cha Kijani.
8. Eleza sababu zilizomfanya Assa na Kalama kuchaguliwa
kuwa mabalozi wa mazingira.
9. Umejifunza nini kutokana na hadithi hii?
19
Mazoezi
Sehemu ya A
Kusikiliza na Kuzungumza
a. Ukiwa na mzazi au mlezi wako, zungumzeni kuhusu namna
ya kukabiliana na umaskini. Maswali haya yatakuongoza:
i. Umaskini unaleta hasara gani katika jamii?
ii. Kufanya kazi kwa bidii kuna faida gani?
iii. Unaweza kuanzisha mradi gani ili ukupatie kipato?
iv. Kwa nini ni muhimu kujitafutia mapato kwa njia halali?
v. Ufisadi unaweza kusababisha vipi umaskini katika jamii?
b. Mwombe mzazi au mlezi wako akusomee kurasa zozote
tatu za hadithi hii. Mwambie akuulize maswali yoyote manne
kutokana na kurasa hizo.
c. Msomee mzazi au mlezi wako ukurasa mmoja wa hadithi
hii. Mwombe akuhesabie idadi ya maneno ambayo unaweza
kusoma kwa ufasaha kwa dakika moja. Mlezi anaweza
kuwa mtu yeyote anayekutunza.
Sehemu B
Ufahamu wa Kusoma
Jibu maswali haya.
1. Matumizi mazuri ya huduma za mtandao yaliwafaidi vipi
Assa na Kalama?
2. Kulingana na hadithi viongozi walisaidia vipi kubadilisha
maisha ya wanakijiji?
3. Je, unafikiri ni mada gani zilijadiliwa katika kongamano hilo
la mazingira la kimataifa?
4. Matumizi haya ya lugha yana maana gani kwa mujibu wa
hadithi?
a. Mboni ya jicho lake
b. Kutia bidii ya mchwa
20
Sehemu C
Matumizi ya Lugha
Soma kifungu kinachofuata. Kina nafasi 1 hadi 5.
Umepewa majibu hapo. Chagua jibu lifaalo zaidi kati
ya yale uliyopewa ili kujaza nafasi.
Watu ___1___ katika kutekeleza miradi ya maendeleo
wanaweza kunufaika na kuboresha hali zao za maisha. Ubora
___2___ maisha huondoa umaskini na kuleta utajiri wa
kiuchumi na wa kijamii. Bidii ya kila mmoja ___3___ ni muhimu
kwa kuwa atakuwa ____4___ katika ushirikiano huo. Bidii ni
nzuri kwa kuwa____5____.
1. a. waliungana b. wataungana c. wanaungana
d. wakiungana
2. a. wa b. ya c. la d. za
3. a. yetu b. chetu c. kwetu d. wetu
4. a. alichangia b. atachangia c. akichangia
d. akachangia
5. a. achanikaye kwa mpini hafi njaa
b. kinga na kinga ndipo moto huwaka
c. mtoto umleavyo ndivyo akuavyo
d. mchagua jembe si mkulima
Sehemu ya D
Kuandika
Unataka kuwahimiza wanafunzi wenzako kuanzisha mradi wa
kuvuna maji ya mvua.Andika insha ya maelezo isiyopungua
maneno 150 kuhusu mradi huo ili uwasomee darasani.
21
Mayai ya Ajabu
22
Hadithi! Hadithi! Hapo zamani za kale paliondokea Mbuni.
Mbuni aliishi mwituni na ndege wenzake kwa furaha. Mbuni
alitaga mayai yake, akayaatamia na kuyaangua. Alitotoa
vifaranga wengi wenye afya. Mbuni aliwalea vifaranga wake
hadi wakakomaa na kujisimamia. Alipoona kuwa vifaranga
wake walikuwa wanaweza kujitafutia riziki, alitaga tena mayai
kumi. Ajabu ni kuwa, wakati huu mayai yalianza kutoweka.
Kila siku Mbuni alipohesabu mayai yake aligundua kuwa yai
moja halikuwapo.
“Ni nani anayechukua mayai yangu? Lazima kuna mwizi hapa,
Mbuni alijisemea kwa huzuni.
Jitimai ya Mbuni ilizidi mayai yake yalipozidi kupungua.
Hakujua la kufanya.Alihangaika akitafuta msaada kutoka kwa
ndege wenzake.Alikwenda kwa Kanga kwanza, akamwelezea
yaliyompata.
“Pole kwa hasara uliyopata. Nilipogundua kuwa mayai yangu
yanaliwa, niliyapaka madoadoa meusi.Tangu hapo hayaliwi
tena. Nilimchanganya akili mwizi.Twende nikakusaidie kupaka
yako rangi pia, Kanga alimwambia Mbuni.
Mbuni alifurahi sana kwa kujitolea kwa Kanga.Alimwongoza
Kanga hadi alipokuwa ametagia.Walichimba mizizi ya miti na
kutengeneza rangi mseto.Walianza kupaka mayai ya Mbuni
rangi.
“Asante sana kwa kunifaa. Akufaaye kwa dhiki ndiye
rafiki.Wewe ni rafiki wa kweli, Mbuni alisema kwa furaha.
“Wewe kwangu ni kama ndugu, lazima nikufae. Undugu ni
kufaana, sio kufanana, Kanga alisema na kumuaga Mbuni.
23
24
Kanga alipoondoka tu, wingu kubwa lilianguka. Ilibidi Mbuni
ayalalie mayai ili ayakinge yasinyeshewe na kufutika rangi.
Alipoyaatamia tu, rangi yote ilifutwa na mbawa zake. Mayai
yakawa kama yalivyokuwa awali. Kesho yake Mbuni alikwenda
kutafuta chakula. Aliporudi, alishangaa kuona kuwa mayai
yake yote hayakuwapo.Alilia kwa huzuni.
Mbuni hakufa moyo.Aliamua kwenda kutafuta ushauri kwa Tai.
“Usitie shaka. Nitakusaidia. Nitakufundisha kujenga kiota.
Utatagia mayai yako juu ya mti kama mimi. Hakuna yeyote
ambaye ataweza kuyafikia. Utayaangua yote,Tai alimhakikishia
Mbuni.
“Asante sana kwa kunitia moyo, Mbuni alimshukuru Tai.
Kazi ya kujenga kiota cha Mbuni ilianza mara moja.
Mbuni alikusanya vijiti, nyasi na majani na kumpokeza Tai ili
amtengenezee kiota. Kazi ya ujenzi ilipokamilika,Tai alimwambia
Mbuni apande kwenye kiota chake. Mbuni alijaribu kupanda
mtini akashindwa.
“Siwezi kupanda mtini. Nifanyeje?” Mbuni aliuliza.
“Naona tutengeneze ngazi, Tai alisema.
Tai na Mbuni walishirikiana kutengeneza ngazi maalum ili
Mbuni aitumie. Ngazi hiyo waliitengeneza kwa kutumia mimea
itambaayo mwituni. Mbuni alitumia ngazi hiyo kupanda hadi
kwenye kiota chake. Alifurahi sana kwa kuwa alijua kuwa
tatizo lake lilikuwa limetatuliwa.Alipofika kwenye kiota chake,
alimpungia Tai mkono ili kuonyesha shukrani yake.Tai naye
pia alimpungia Mbuni mkono na kuondoka.
25
Mbuni alikikalia kiota chake ili akipashe joto.Alitarajia kuwa
wakati wowote ule angetaga yai lake la kwanza. Mbuni alisikia
Kuku akiteta kwa mbali. Aliangalia chini ya mti ili amwone
Kuku.Alipoangalia tu, aliingiwa na woga mwingi na kushikwa
na kisunzi. Mbuni alitetemeka na kutingisha kiota chake.
Kiota kilianza kudondoka. Mbuni aliingiwa na woga zaidi kila
apoangalia chini. Mwishowe aliporomoka na kuanguka chini.
Mabawa yake yalimsaidia. Hakuumia.
“Pole, Mbuni. Kwa nini umepanda juu ya mti?” Kuku alimuuliza
Mbuni.
“Nilikuwa nataka kutaga, Mbuni alijibu kwa huzuni.
“Tangu lini ukatagia juu ya tagaa? Uzito wa mwili wako
hauwezi ukakuruhusu kuishi mtini. Si kawaida wewe hutaga
mchangani?” Kuku alimuuliza Mbuni.
“Pale ninapotagia si salama.Mayai yangu yanaibwa kila
ninapotaga. Kwa muda sasa sijaangua vifaranga, Mbuni
alijibu kwa simanzi.
“Njoo twende kiamboni kwa binadamu.Atakupatia ulinzi kama
anavyonipatia mimi na vifaranga wangu, Kuku alimwambia
Mbuni.
“Asante kwa kunikaribisha huko mastakimuni kwa binadamu.
Nafikiri sasa nimepata suluhisho la kudumu kwa tatizo langu,
Mbuni alisema kwa bashasha.
Kuku na Mbuni waliandamana hadi chengoni kwa binadamu.
Binadamu aliwakaribisha vizuri.Aliwapatia mtama walipofika
wakadona. Alimtengenezea Mbuni mahali pazuri pa kuishi.
Mbuni alianza kutaga mayai. Baada ya muda aliyalalia na
kuangua vifaranga wanne. Mwanzoni binadamu alimlisha Mbuni.
Vifaranga wa Mbuni walipokua, binadamu alianza kuona ugumu
26
wa kumlisha Mbuni.Vifaranga wa Mbuni walihitaji nafaka nyingi.
Baada ya muda binadamu aliishiwa na nafaka. Mbuni alianza
kujitafutia chakula. Siku moja vifaranga wa Mbuni waliingia
shambani mwa binadamu na kula mahindi yote yaliyokuwa
yamepandwa na kuota. Binadamu alikasirika na kumfukuza
Mbuni. Mbuni na vifaranga wake walihama kwa binadamu.
Walirudi tena mwituni.
Mbuni aliendelea kutafuta msaada kwa ndege tofauti mwituni.
Alikutana na Flamingo.
“Hujambo, Flamingo? Nina shida, tafadhali nisaidie, Mbuni
alimwomba Flamingo.
“Iseme shida yako. Kama ninaweza nitakufaa, Flamingo alijibu.
“Ninawezaje kuyalinda mayai na vifaranga wangu wasiliwe?”
“Nitakufundisha kujenga kiota maalum cha matope, vijiwe,
vijiti na nyasi kando ya ziwa. Utawaficha vifaranga wako
hapo. Baadaye ukitaga mayai yako pia utayalalia hapo,
Flamingo alimwelezea Mbuni.
Mbuni alifurahi sana aliposikia hivyo.Aliandamana na Flamingo
bila ya kupoteza muda.Walipofika kando ya ziwa walianza
kazi ya ujenzi wa kiota mara moja. Walijenga kiota hicho
mchana kutwa. Jioni kiota kilikuwa kimekamilika. Mbuni aliwaita
vifaranga wake waingie kwenye kiota. Alipoingia kifaranga
mmoja tu, kiota kilijaa.
“Kiota kimejazwa na kifaranga mmoja. Umenidanganya.
Nimechoka bure, Mbuni alimlalamikia Flamingo.
27
28
“Usinilaumu. Sio makosa yangu. Sisi tumezoea kutaga na
kuangua yai moja tu. Kwa hivyo kifaranga wetu huwa mmoja
tu. Wewe kumbe una vifaranga kumi na wawili. Pole sana.
Nasikitika, siwezi kukusaidia. Nimejaribu niwezavyo, Flamingo
alisema.
Maisha ya Mbuni sasa yalikuwa magumu. Hakujua akimbilie
nani.Aliamua kuzurura mwituni ili apate mahali pa kuwaficha
vifaranga wake wasiliwe. Mbuni alifika pangoni.Alilichungulia
pango na kulichunguza vilivyo.Aliogopa kuwa pengine kulikuwa
na nyoka humo ndani.Alipohakikisha kuwa lilikuwa salama,
aliingia na vifaranga wake humo ndani.Vifaranga wa Mbuni
walianza kucheza mara tu walipoingia pangoni.Walifukuzana
na kudona wadudu wadogo wadogo humo pangoni.
“Wee!Wee! Polepole. Huku kuna wenyewe, sauti kali ilisikika.
Mbuni alitafuta kila mahali ili amwone mwenye sauti lakini
hakumwona.
“Samahani kwa kupiga kelele. Hodi huku.Wako wapi wenyewe?”
Mbuni aliuliza kwa hofu.
“Kitendawili, alisema Popo.
“Tega, alisema Mbuni.
“Miguu juu, kichwa chini. Mimi ni nani?” Popo aliuliza.
“Wewe ni Popo, Mbuni alisema huku akiangalia juu.
Aliwaona Popo wengi ajabu wamening’inia juu pangoni.
“Kwa nini mnaishi mkining’inia?” Mbuni aliwauliza.
29
“Ili adui asituone. Si wewe mwenyewe ni shahidi. Umeingia
hapa na hukujua kuwa huku kuna wenyewe. Isitoshe, hii ni njia
nzuri pia ya kutegea chakula.Wadudu na wanyama wadogo
wadogo huingia hapa kama vile ulivyoingia bila ya kutuona,
nasi huwadakia juu juu na kuwala. Hivi unavyotuona, tunategea
chamcha. Faida za kuning’inia ni kocho, zipo na nyingine
nyingi, Popo alijibu kwa kutoa maelezo marefu.
Mbuni alimwelezea Popo dhiki yake yote. Alimuuliza Popo,
“Nitafanyaje ili mayai na vifaranga wangu wawe salama?”
“Hapo kwa mayai sijui. Sisi hatutagi mayai kama nyinyi.
Sisi hutunga mimba na kuzaa watoto. Tofauti na ndege, sisi
hunyonyesha watoto wetu, Popo alimjibu Mbuni.
“Si nyinyi ni ndege? Kwa nini msitage mayai?” Mbuni aliuliza.
“Wengi hukosea wanapodhania kuwa sisi ni ndege. Sisi si ndege
bali ni wanyama wadogo, alijibu Popo.
Popo alimwambia Mbuni ajaribu kuning’inia kama wao ili
akiweza, waishi pangoni pamoja. Mbuni alijaribu, lakini kwa
sababu ya uzito wake alianguka chini pu!
Mbuni aliondoka pangoni kuelekea asikokujua kwa masikitiko
makubwa.Vifaranga wake walimfuata unyo kwa unyo kimya.
Njiani, Mbuni alikutana na Chiriku.Alikuwa anaimba nyimbo
na mashairi kwa furaha.
“Unaonekana mwenye kihoro. Una tatizo gani?” Chiriku
alimuuliza Mbuni.
Mbuni alimwelezea chiriku masaibu yake yote. Chiriku
alimwimbia Mbuni wimbo ili kumtia moyo:
30
Mbuni nakuomba usihuzunike,
Jipe moyo sana usibabaike,
Pambana vikali usitishwetishwe.
Nilimwona Nyani anayapasua,
Mayai ya kwako akiyabugia,
Pambana vikali usitishwetishwe.
Tengeza mtego umnase mwizi,
Ninakushauri mimi ni mjuzi,
Pambana vikali usitishwetishwe.
Katafute mawe kule mlimani,
Uyabingirishe yaje huku chini,
Pambana vikali usitishwetishwe.
Panga mawe hayo kwako kiotani,
Nyani akifika atayatamani,
Pambana vikali usitishwetishwe.
Nami nitakuja nitamhimiza,
Kwa tamaa yake mawe atameza,
Pambana vikali usitishwetishwe.
Mbuni aliusikiliza kwa makini wimbo wa Chiriku. Aliamua
kufanya kila aliloweza ili kuwatetea vifaranga wake na baadaye
mayai yake. Siku iliyofuata alikwenda mlimani. Huko alitafuta
mawe kumi na mawili.Alichagua mawe yale ambayo yaliviringa
vizuri na kufanana na mayai yake kama shilingi kwa ya pili.
Aliyaosha yakang’aa kama mwezi.Aliyaanika yakakauka vizuri.
Mawe yalipokauka, aliyabingirisha yakateremka yenyewe hadi
chini kwenye kiota chake.
31
32
Mbuni alipanga mawe vizuri kiotani kwake. Yalionekana
kama mayai tu. Alimwomba Konokono ayatambalie mawe
hayo. Konokono aliyamwagia mayai makamasi yake. Mayai
yalimetameta. Mbuni aliondoka na kwenda zake. Chiriku alibaki
mtini akimngoja Nyani aje, ili amhadae. Chiriku alisubiri
lakini Nyani hakuja siku hiyo. Siku ya pili, Chiriku alirudi pale
pale juu ya mti ili amngoje Nyani.
“Pengine Nyani amejua kuwa tumemtega, akatoroka, Mbuni
alimwambia Chiriku.
“Nyani hana habari kuhusu mtego huu. Najua atakuja. Subira
huvuta heri.Tungoje tu, Chiriku alimwambia Mbuni.
Nyani aliwasili saa sita mchana.Alitembea kwa madaha kama
kawaida yake.Aliyakagua mayai ya Mbuni huku akidondokwa
na mate.
“Haya mayai ni safi ajabu.Yanametameta.Tena ni makubwa.
Lazima ni matamu, Nyani alijisemea, kisha akachukua yai moja
ili alipasue. Nyani aliligongesha yai hilo kwenye mwamba wa
jiwe lakini halikupasuka.Alichukua yai la pili, tatu, nne hadi la
kumi na mbili na kujaribu kulipasua, lakini hakufua dafu. Nyani
alianza kulaani.
Chiriku kuona hivyo, alianzisha mazungumzo na Nyani.
Chiriku: (Baada ya kupepeta mbawa zake na kupiga
mluzi.) Hujambo, Nyani?
Nyani: Nina jambo. Usinipigie kelele. Nafikiria.
Chiriku: Unafikiria nini?
Nyani: Namna ya kuvunja mayai.
Chiriku: Nina wazo.
Nyani: Si uliseme! Wangoja nini?
Chriku: Yakalie mayai kwa nguvu sana, yatavunjika.
Nyani: (Akilia kwa uchungu.) Wooi! Wooi! …makalio
33
yangu. Nimeumia.
Chiriku: Pole.
Nyani: Umenidanganya. Sitaki mawazo yako tena.
Chiriku: Nina wazo la mwisho na bora zaidi.
Nyani: Liseme haraka. Tena liwe wazo la maana, ama
unyamaze nijiwazie mwenyewe.
Chiriku: (Akichekacheka.) Pia wewe huwaza?
Nyani: (Kwa ukali.) Chiriku, sitaki utani wako. Kama
huna la kusema nenda zako.
Chiriku: Badala ya kusumbuka si umeze mayai tu?
Nyani: Nitayamezaje mayai makubwa hivi?
Chiriku: (Kwa sau ya kubembeleza.) Ebu jaribu.
Hakuna lisilowezekana. Utaweza kuyameza tu.
Nyani: (Baada ya kumeza yai la kwanza kwa taabu.)
Mayai yenyewe yanateleza. Asante, umetatua
tatizo langu. Leo nitakula nishibe.
Chiriku: (Akifungia kicheko.) Karibu. Lakini usimeze yote.
Kumbuka kuwa tamaa ilimuua fisi.
Nyani aliendelea kumeza mayai. Mayai yaliteleza kwa msaada
wa makamasi ya Konokono. Nyani alijilazimisha hata aliposhiba
na kumeza mayai yote kumi na mawili, tumbo likawa kubwa
kupindukia.Alipotaka kuondoka alishindwa. Uzito wa mawe
tumboni ulimfanya kuwa mzito kama nanga. Nyani alianza
kujiburuta chini kwa makalio yake.Alitaka kuondoka haraka
iwezekanavyo. Aliogopa kuwa Mbuni angemkuta katika hali
hiyo.Alihofia kushambuliwa na Mbuni akiwa hajiwezi. Nyani
alijiburuta huku akilia kwa uchungu. Kadri alivyojiburuta ndivyo
makalio yake yalivyozidi kubambuka.Alimlaani Chiriku.
Mbuni na vifaranga wake waliangalia sinema hii wakiwa
wamejibanza kwenye kichaka.Walicheka mbavu zikawauma.
Mbuni aliamua kujitokeza mara tu Nyani alipoanza kujiburuta.
Alijidai kumfukuza Nyani. Nyani alilia kwa huzuni huku akitubu,
“Nisamehe. Sitarudia tena. Ninaumia makalio, yamebambuka.
34
Siwezi kutoroka. Mayai yako ni mazito. Ni mayai ya ajabu!”
Mbuni aliendelea kumfukuza Nyani huku akicheka.Alijua kuwa
alikuwa amemfunza adabu. Baadaye, Mbuni alimshukuru Chiriku
kwa kumsaidia kumnasa mwizi wa mayai yake. Nyani alikoma
kabisa kuiba mayai ya Mbuni.Wakati mwafaka ulipofika, Mbuni
alitaga, akayalalia na kuangua vifaranga wengine kumi na
wawili.
Nyani alijikokota hadi kwa Mganga Kunguru. Alipofika,
alimlilia Kunguru. Alielezea yote yaliyotokea. Alipewa dawa
ya kuendesha ili aweze kutoa mawe aliyomeza.Alipewa dawa
nyingine ya kupaka kidonda kwenye makalio yake.
“Siku za mwizi ni arubaini.Wizi ni mbaya!” Mganga Kunguru
alimwonya Nyani.
“Nimepata funzo na nikapata kovu la kunikumbusha maovu
yangu. Sitarudia tena. Nikimwona Mbuni nitamwomba
msamaha, Nyani alisema kwa upole.
Nyani alipopona kidonda kwenye makalio, alibaki na kovu
kubwa.Tangu wakati huo, Nyani ana ngoko kwenye makalio.
35
Kamusi Yangu
akayaatamia akayalalia mayai
amhadae amdanganye
chengoni nyumbani
jitimai huzuni kuu
kiamboni nyumbani
kihoro huzuni kubwa inayosababishwa na
kufikwa na jambo baya
kisunzi hali ya kusikia kichwa kikizunguka;
kizunguzungu
kocho nyingi sana
kujimburuta kujivurutia chini
madaha maringo
mashtakimuni mahali pa kuishi; makazi
ngoko sehemu nyekundu iliyo kama nyama
mbichi kwenye makalio ya nyani
wamejibanza wamejificha
36
Maswali
1. Ndege anapotaga mayai huyafanyia nini ili apate vifaranga?
2. Mbuni alienda kutafuta msaada kwa Kanga.
a. Kanga alimsaidia vipi?
b. Kwa nini msaada wa Kanga haukudumu?
3. Kwa nini Mbuni alianguka kutoka kwenye kiota juu ya mti?
4. Toa sababu ambazo zilimfanya binadamu kumfukuza Mbuni.
5. Flamingo hujenga viota vyao kwa kutumia nini?
6. Je, kwa nini Popo si ndege?
7. Kwa maoni yako, wizi una madhara gani?
8. Je, mazungumzo kati ya Chiriku na Mbuni yamekufunza
nini?
9. Ni neno gani ambalo msimulizi angetumia badala ya neno
kiamboni kwenye hadithi?
10. Kulingana na hadithi Nyani alipata ngoko yake vipi?
37
Mazoezi
Sehemu A
Kusikiliza na Kuzungumza
Soma mazungumzo kati ya Chriku na Nyani kwenye hadithi
kisha ujibu swali la 1 hadi la 4. Umepewa majibu manne. Chagua
jibu lifaalo zaidi kati ya yale uliyopewa.
1. Nyani alidanganyika haraka kwa kuwa:
a. alipenda kuiba.
b. alitamani mayai sana.
c. aliacha kuwaza mwenyewe.
d. alimwamini Chiriku.
2.Kwa nini Nyani alimeza mawe kwa urahisi?
a. Mawe yalikuwa matamu.
b.Alikuwa na tamaa ya fisi.
c.Aliogopa kupatikana na Mbuni.
d. Mawe yaliteleza akimeza.
3. Kama Nyani angekataa wazo la Chiriku la kumeza mayai:
a. Chiriku angeonekana mwongo.
b. Mganga Kunguru angekosa kazi.
c. Mwizi hangejulikana.
d. Nyani hangefunzwa adabu.
4. Chagua maneno ambayo yana maana sawa na nyumbani.
a. kiamboni, mastakimuni, sebuleni
b. majilisi, chengoni, kiamboni
c. mastakamuni, chengoni, kiamboni,
d. chengoni, sebuleni, kiamboni
5. Nyani ni mwenye tamaa kwa kuwa:
a. alimeza mawe haraka.
b. alimeza mawe bila woga.
c. alimeza mawe makubwa.
d. alimeza mawe yenye kamasi.
38
Sehemu B
Kusoma kwa Ufahamu
Jibu swali la 6 hadi la 10. Maswali haya yametokana
na hadithi uliyosoma. Umepewa majibu manne hapo.
Chagua jibu lifaalo zaidi kati ya yale uliyopewa.
6. Bidii ya Mbuni ilimwezesha kufaulu kwa kuwa:
a. aliweza kumkamata mwizi wa mayai.
b. alifanikiwa kuangua vifaranga kumi na wawili.
c. alijifundisha kutengeneza viota tofauti.
d. alijua kuwa Popo si ndege kama yeye.
7. Chagua jibu ambalo ni mfuatano sahihi wa matukio kwenye
hadithi uliyosoma.
i. Mbuni kwenda kwa Tai
ii. Mbuni kwenda kwa binadamu
iii. Mbuni kwenda kwa Kanga
iv. Mbuni kumwona Popo
v. Mbuni kukutana na Flamingo
a. (i), (ii), (v), (iv)(iii)
b. (iii), (i), (ii), (v), (iv)
c. (ii), (v), (iv) (iii), (i)
d. (iv), (i), (iii), (v), (ii)
8. Kulingana na hadithi, ni methali gani ambayo Kunguru
angemwambia Nyani alipolia?
a.Asiyesikia la mkuu huvunjika guu.
b.Asiyefunzwa na mamake hufunzwa na ulimwengu.
c. Mbio za sakafuni huishia ukingoni.
d. Majuto ni mjukuu, huja kinyume.
9.Wimbo wa Chiriku ulikuwa na umuhimu gani kwa Mbuni?
a. Ulimfanya Mbuni kuwa msikivu.
b. Ulimpa Mbuni ujasiri ili aweze kupambana na mwizi.
c. Ulimwelekeza Mbuni jinsi ya kumnasa mwizi.
d. Ulimliwaza Mbuni ili asiwe na majonzi.
39
10. Popo si ndege kwa kuwa:
a. ana mabawa ambayo yameshikana na mwili.
b. ananing’inia akiangalia chini.
c. ananyonyesha watoto.
d. anaishi pangoni.
Sehemu C
Matumizi ya lugha
Soma kifungu kifuatacho. Kina nafasi 11 hadi 15.
Umepewa majibu manne hapo. Chagua jibu lifaalo
zaidi kati ya yale uliyopewa.
Ndege wa porini wana umuhimu mkubwa sana _11_ binadamu.
Ndege __12___ wakulima kuvuna chakula kingi ___13__ ya
bidii yao. Ndege hupuruka kutoka kwenye mti au mmea mmoja
__14___ mwingine wakiwa wamebeba mbegu.Wanaposambaza
mbegu __15__ kilimo huimarika na mavuno kuwa mengi.
11. a. ya b. wa
c. na. d. kwa
12. a. huwezesha b. huwezekana
c. huwezeshwa d. huwezea
13. a. kwa vile b. kwa kuwa
c. kwa maana d. kwa sababu
14. a. katika b. hadi
c. kwa d. hata
15. a. hiyo b. hii
c. ile d. hizo
40
Sehemu D
Kuandika
Unataka watu wakome kuchezea viota vya ndege wa porini.
Waandikie mchezo mfupi wa kuigiza kuonyesha umuhimu wa
ndege wa porini. Mtumie rafiki yako mchezo huo ili ausome
na kukupatia maoni yake.
41
Dolfina
42
Issa na wanamazingira wenzake walifika upwani mapema.
Mwalimu wao, Bi. Heri, pia naye alirauka. Azma yao siku hiyo
ilikuwa kusafisha upwa. Zoezi hili walilifanya kila wikendi ya
kwanza ya mwezi.
“Hamjambo?” Bi. Heri aliwasalimu wanafunzi walipokutana.
“Hatujambo, mwalimu, Issa na wenzake waliitikia kwa pamoja.
“Nimefurahi kwamba mmefika hapa mapema. Bidii yetu ya
mchwa imetuzalia matunda na itazidi kuwafaidi wengi.Naomba
tuanze kazi mara moja, na leo msicheze na pomboo, Bi.Heri
aliwaambia wanafunzi wake.
Chama cha mazingira katika shule ya msingi ya Shimoni
kilikuwa kimetia fora. Sifa yao ilikuwa imevuma kote nchini.
Chini ya uongozi wa kinara wao, Issa, na mlezi wa chama
chao, Bi. Heri, wanamazingira hao walikuwa wamepata
ufanisi mkubwa. Kwanza, walikuwa wamenyakua kombe la
mashindano ya wanamazingira bora kwenye kaunti yao. Pili,
walikuwa wanashikilia taji la chama bora zaidi shuleni mwao.
Yote haya yalikuwa kwa hisani ya jitihada zao na uongozi
mzuri. Ushindi wao ulitokana na shughuli walizofanya kwa
ajili ya kuifaidi shule yao na jamii yao.
Hapo shuleni mwao kwa mfano, walikuwa wameanzisha
mradi wa ukuzaji miche. Mradi huo uliwawezesha kupanda
na kustawisha msitu mkubwa kwenye shamba la shule yao.
Uliwawezesha pia kuzirembesha bustani za shule kwa maua
ya kila aina.Walipanda miasumini na miwaridi. Miasumini
iliyapatia mazingira ya shule yao harufu nzuri na miwaridi
nayo iliyafanya mandhari ya shule yao kuvutia. Maua ya
miwaridi ya rangi kadha wa kadha pia yalivutia vipepeo.
Vipepeo hao walizidi kuyapamba mazingira hayo kwa mbawa
zao za rangi ainati.
43
“Tafadhali vaeni glavu zenu.Asiye na glavu aokote taka kwa
kuzidunga kwa kijiti,“Issa alisema huku akivaa glavu zake.
Wanamazingira hao walikuwa na glavu na ovaroli zao za kazi.
Hata hivyo, wakati mwingine wachache kati yao wangesahau
kubeba zana hizo za kazi. Ilipotokea hivyo, wangetumia mbinu
ya ufaraguzi ili waweze kuokota na kuzoa taka upwani.Wale
waliokosa glavu kwa mfano, walitafuta vijiti vyenye ncha kali
na kudungia taka.
Zoezi la kuokota taka lilianza.Taka zilikuwa zimerundikana
nyingi upwani. Nyingi kati ya taka hizi zilikuwa karatasi za
kila aina.
“Taka zimezidi hapa upwani. Nafikiri afadhali tuweke vibao
vyenye onyo hapa, Issa alimwambia Bi. Heri.
“Wataka onyo lenyewe lisemeje?” Bi. Heri alimuuliza Issa.
“Ni marufuku kutupa taka hapa!” Issa alisema kwa msisitizo.
“Nafikiri hilo ni wazo zuri, alisema Bi. Heri.
Issa na wenzake waliokota taka wakamaliza. Baada ya hapo,
walipumzika na kupunga upepo kidogo. Issa aliwashauri
wenzake watengeneze sehemu za watu kutupa taka kabla ya
kwenda nyumbani.
“Ninaomba tuwawekee watu vikapu hivi hapa karibu na upwa
ili watupe taka zao.
Watu wataona aibu kutupa taka upwani ilhali kuna mahali
mbadala pa kutupa, alieleza Issa.
“Sawa kabisa ila vikapu vyenyewe ni vyepesi. Vitapeperushwa
na upepo au visombwe na maji, alisema Tanasha huku
akikikagua kikapu kimoja.
44
45
“Ninapendekeza tuvidunge vikapu vyenyewe kwa vijiti
tulivyovitumia kuokotea taka.Vitakuwa thabiti, havitasonga
wala kuanguka, alisema Idi.
Wazo la Idi liliwavutia wengi.Wanamazingira hao walianza
kazi ya kuvipanga vikapu vyao sehemu tofauti za upwa.Vingine
waliviweka chini ya minazi na vingine kando ya miamba.
Baada ya kuvipanga, walianza kuvidunga vijiti kando kando.
Walipomaliza kazi hiyo, Issa alipendekeza watengeneze vibao
vya onyo mara moja.
“Vibao vyenyewe tutatoa wapi?” Idi aliuliza.
“Pengine tunaweza kufikiria mbinu nyingine ya kuwasilisha
ujumbe wetu, si lazima vibao. Simba akikosa nyama hula nyasi,
alisema Issa.
“Nina wazo, alisema Tanasha
“Liseme tusikie, alisema Bi. Heri.
“Napendekeza tuandike tangazo letu kwenye miamba hii ya
mawe.Tunachohitaji ni rangi ambayo haiwezi kuoshwa na maji
kwa urahisi. Nitaliandika tangazo lenyewe, Tanasha alisema.
“Kweli penye wengi hapaharibiki jambo. Nitapiga simu tuletewe
rangi na brashi mara moja ili kazi ianze, alisema Bi. Heri.
Rangi na brashi vilipoletwa,Tanasha alianza kazi mara moja.
Wenzake walimsaidia pale walipoweza ili kazi yake iwe rahisi.
Tanasha naye alitumia talanta yake ya uchoraji kuandika
maandishi yaliyosomeka na yenye kuvutia.
“Brashi imeanguka!” Tanasha alisema kwa msikitiko.
Alikuwa amebakisha maandishi machache tu amalize kazi.
Watoto walianza kuitafuta brashi kando ya mwamba mkubwa.
46
Walichakura kwenye changarawe na majani yaliyoanguka ya
mkungumanga bila mafanikio.
“Lo! Nimegusa kitu kikubwa na kiko hai!” alisema Issa kwa
sauti.
Watoto waliondoa majani ya mkungumanga kwa uangalifu.
“Ni samaki mkubwa.Amenaswa chini ya mwamba, Idi alisema.
“Haya kuweni waangalifu. Nataka tumnasue kama tunaweza.
Kama hatuwezi tutawapigia simu walinda upwa waje
watusaidie, alisema Bi. Heri.
Watoto walijaribu kumnasua pomboo huyo wakashindwa.
“Msimguse tena! Nawaita walinda upwa waje, Bi. Heri
aliamuru.
Walinda upwa waliwasili mara moja na vifaa maalum vya
kumnasulia pomboo huyo. Pomboo alikuwa chini ya mwamba.
Alikuwa amenaswa na neti kubwa. Neti hiyo ilikuwa imezunguka
mwili wote.Yaonekana alishindwa kuogelea, akasombwa na
mawimbi hadi chini ya mwamba huo.
Walinda upwa walianza kumtoa neti pomboo bila kupoteza
wakati. Watoto walisaidia kushika neti na kuivuta taratibu
walivyoshauriwa. Ilikuwa neti kubwa ajabu na yenye matundu
madogo.
47
48
Pomboo alipotolewa kwenye neti, alirudishwa kwenye maji.
“Hawezi kuogelea, alisema Issa.
“Tutamtoa. Lazima ameumia. Tutakwenda naye tumtunze
kwenye vidimbwi vyetu kwanza. Akipona na kupata nguvu
tutamrudisha hapa, mmoja wa walinda upwa alifafanua.
Walinda upwa waliwapigia wenzao simu na baada ya muda
gari maalum liliwasili. Pomboo huyo alibebwa na kutiwa
kwenye kidimbwi humo garini.Walinda upwa waliwapongeza na
kuwashukuru wanamazingira na mlezi wao, Bi. Heri, kwa kazi
waliyokuwa wanafanya.Walinda upwa waliahidi kusaidiana
na wanamazingira hao kuimarisha usafi wa upwa.
Kabla ya gari lao kung’oa nanga, Issa aliuliza,“Naweza kuja
kumtembelea pomboo kituoni kwenu? Ningependa kujua
atakavyoendelea.
“Unaweza. Umekaribishwa, bora ujitambulishe kwenye lango
kuu. Tutawaelezea walio kwenye lango yote yaliyojiri. Bila
shaka ukija watakuruhusu kuingia na wakuelekeze vilivyo,
alijibu mlinda upwa mmoja.
Watoto waliwaaga walinda upwa. Gari la walinzi lilipoondoka,
watoto waliendelea kutafuta brashi.Walipoiona, waliipangusa na
kumpaTanasha.Tanasha alimaliza kazi yake na wakaruhusiwa
kwenda nyumbani.
Kesho yake jioni, Issa aliwaomba ruhusa walezi wake ili aende
kumwona yule pomboo. Kwa kuwa kwao hakukuwa mbali na
baharini, Issa aliruhusiwa.
“Nenda ila usichelewe. Nataka uje kunisaidia kufungia mifugo.
Si unajua kazi ya uvuvi ni ngumu? Babu yako akirudi atakuwa
amechoka. Akifika nataka pia tumsaidie kupara samaki
watakaokuwa wamesalia. Sasa umekuwa mkubwa, lazima
49
utusaidie kufanya kazi kwa kadiri ya uwezo wako, alisema
nyanya yake Issa.
“Sawa, Nyanya. Nitarudi haraka. Nataka kwenda kumwona
yule pomboo tuliyemwokoa jana, Issa alimwambia nyanya
yake kisha akatoka na kwenda.
Issa alipofika kwenye lango la kituo cha walinda upwa,
alipokelewa vizuri. Aliongozwa na mmoja wa wale walinda
upwa waliokutana upwani hadi alipokuwa pomboo.
“Naona bado angali mnyonge. Hachezi kama wanavyofanya
pomboo baharini, alisema Issa.
“Ni kweli bado hana nguvu. Lazima alikuwa amenaswa kwa
muda pale tulipompata. Hata hivyo, hawezi kucheza sana
akiwa peke yake, alielezea yule mlinda upwa.
“Anakula?” Issa aliulizia.
“Anakula vizuri sana, alijibu yule mlinda upwa.
“Naweza kumpa chakula kidogo?” aliuliza Issa.
“Ndio, unaweza. Nitakuletea vipande vya samaki umpe,
alisema yule mlinda upwa.
Issa alipewa vipande vya samaki akamrushia yule pomboo
kimoja baada ya kingine. Pomboo alividaka kama mpira na
kuvila haraka haraka.
“Asante kwa kuniruhusu kumpa pomboo chakula. Inasikitisha
kwamba kiumbe huyu anateseka kwa ajili ya wavuvi haramu,
alisema Issa.
“Ni kweli usemavyo. Jambo hili linatia simanzi sana. Kiumbe
kama huyu ambaye haliwi katika utamaduni wetu hafai
50
kuteseka kwa kunaswa. Neti yenyewe ilikuwa na matundu
madogo na hairuhusiwi katika bahari yetu. Neti hiyo ni haramu
kwa kuwa inaweza kuvua samaki ambao hawajakomaa.Tendo
hilo linaweza kuhatarisha uhai baharini, alieleza mlinda upwa.
“Sasa tutafanya nini ili kupambana na maovu hayo?” aliuliza
Issa kwa huzuni.
“Wavuvi wenye nyavu zenye matundu madogo hawaruhusiwi
katika bahari yetu.Tangu hapo jana tayari tumewatia ndani
wavuvi wawili.Tutawashtaki kwa kukiuka masharti na makataa
ya uvuvi katika bahari hii.Watu wanaochafua upwa wetu pia
watachukuliwa hatua za kisheria. Hatuwezi kukubali watu
wachache warudishe juhudi zetu za utunzaji wa mazingira
nyuma, alieleza mlinda upwa huyo.
Issa aliondoka kwenda nyumbani akiwa amejawa na furaha
moyoni.Alijua kuwa jitihada zao zilikuwa zinaungwa mkono
na walinda upwa.
Issa alitembelea pomboo mara kwa mara. Kila alipofika,
aliomba kumpa pomboo chakula. Pomboo alianza kumzoea
Issa. Siku moja pomboo alimrukia Issa na kuanza kucheza
naye.Tangu siku hiyo Issa alifanya urafiki wa chanda na pete
na pomboo huyo.
“Anakupenda kweli.Akikuona anaruka kwa furaha.Anataka
mcheze tu, alisema mlinda upwa.
“Hata nami nampenda. Naomba kumpa jina, alisema Issa.
“Mpatie jina upendalo.Wataka kumwita nani?” aliuliza mlinda
upwa.
“Nitamwita Dolfina kwa kuwa uliniambia ni wa kike, alijibu
Issa.
51
“Hilo ni jina zuri sana, alisema mlinda upwa
Tangu siku hiyo Issa alimwita pomboo huyo Dolfina.
Siku ya Dolfina kurudishwa baharini ilikaribia. Mlinda
upwa mmoja alimpigia Bi. Heri simu. Alimwomba awalete
wanamazingira upwani ili waagane na Dolfina akirudi baharini.
Walinda upwa walikuwa wamependezwa na kuvutiwa na moyo
wa Issa wa kupenda kutunza mazingira.Walitaka Issa ashuhudie
rafiki yake Dolfina akirudi baharini.Waliliona hili kuwa tukio
la kipekee na la kumtia moyo Issa na wanamazingira wenzake.
Ilikuwa wikendi ya kwanza ya mwezi kama kawaida.
Wanamazingira walirauka kama ilivyokuwa ada yao.
Walipofika upwani tu, gari lililokuwa limembeba Dolfina
liliwasili. Dolfina alitolewa kwenye kidimbwi kidogo garini kwa
makini.Aliwekwa kwenye upwa wa bahari.Wimbi dogo lilikuja
na kumfunika Dolfina. Dolfina alitulia tuli. Ni kama ambaye
hakutaka kurudi baharini. Issa alikwenda na kumpapasa
Dolfina mgongoni. Dolfina alianza kuogolea taratibu akielekea
kwenye maji makuu. Chozi lilimdondoka Issa huku akimpungia
Dolfina mkono.Wanamazingira walishangilia kwa furaha. Bi.
Heri aliwapiga picha kwa simu yake ya mkononi.
“Usilie, Issa. Dolfina atakuwa salama, alisema mlinda upwa
mmoja.
“Chozi langu ni la furaha. Najua Dolfina atakuwa salama.
Anaenda kuishi na familia yake. Nafurahi kuwa tuliweza
kumwokoa Dolfina. Hata hivyo nitampeza sana, Issa alisema
hivyo huku akipangusa machozi.
52
53
Bi. Heri alituma picha alizopiga wanamazingira kwenye
mitandao ya kijamii. Mada ya ujumbe wake ilikuwa Dolfina
aokolewa, tuwalinde wanyama wa baharini na
tuyalinde mazingira yetu.Alitoa maelezo mafupi namna
wanamazingira walivyomwokoa Dolfina. Alieleza pia jinsi
Dolfina alivyotunzwa hadi akapona kisha akatuma picha
kadhaa za mwanzoni Dolfina akiwa amenaswa kwenye neti.
Alituma pia na picha za siku hiyo Dolfina akiogolea kuelekea
bahari huku wanamazingira wakimpungia mkono.
Ujumbe na picha za Bi. Heri mtandaoni ziliwavutia wengi.
Watu walitoa maoni yao kuhusu ujumbe huo, huku wakiwasifu
wanamazingira. Chama chao cha mazingira kilizidi kutia fora.
Siku moja wakati wa likizo fupi, Issa alienda baharini na babu
yake. Walirauka. Issa aliwaona pomboo wanne wakicheza
kwa mbali walipofika upwani.
“Babu, ninataka kuwa baharia nikiwa mtu mzima, Issa
alimwambia babu yake.
“Jitihada huvuta heri. Soma kwa bidii, mjukuu wangu. Mabaharia
wa siku hizi ni wasomi.Wanaendesha meli kubwa kwa kutumia
teknolojia. Ningetaka usomee uhandisi wa vyombo vya baharini.
Hapo utakuwa si baharia tu, bali mjuzi wa vyombo vyote
vieleavyo majini, Babu alimwambia Issa.
“Ninatia bidii masomoni, Babu. Ninataka kuwa baharia
aliyesomea sanyansi ya viumbe wa baharini. Nataka niweze
kufanya utafiti kuhusu namna ya kuhifadhi viumbe hao. Ninajua
ndoto yangu itatimia, Issa alijibu kwa furaha.
“Naona Bi. Heri amefanya kazi nzuri. Haya, uliniahidi kuwa
utanisindikiza tu. Hatukukubaliana kwamba utaenda baharini.
Leo hali ya anga haipendezi. Bahari imechafuka na boti zetu
nazo ni mbovu. Lolote linaweza kutokea. Unahitaji kuwa
54
mwogoleaji tajika kuingia baharini leo, Babu alisema.
“Nitacheza hapa kidogo kisha nirudi nyumbani. Nakuelewa,
Babu. Leo bahari naona imekasirika.
“Kwaheri, mjukuu wangu. Acha niende kutafuta riziki, Babu
alimuaga Issa.
Mara Issa aliona pomboo wawili wakiogolea kuelekea
alipokuwa. Alitamani sana mmoja wa pomboo hao awe
Dolfina. Pomboo walipomfikia Issa alikwenda kusimama juu
ya mwamba. Chini ya mwamba huo kulikuwa na kidimbwi
ambacho pomboo wangeogelea vizuri. Pomboo mmoja aliruka
na kumdara Issa.
“Dolfina! Dolfina!” Issa aliita kwa furaha. Dolfina aliruka na
kumdara tena Issa. Kisha alizama majini na kuzuka na kijiwe
na kukiwekelea kwenye mwamba alipokuwa amesimama Issa.
Dolfina alizama tena. Issa alichukua kijiwe kile na kukiangalia.
Kilikuwa kijiwe tu. Dolfina alizuka tena na kuwekelea susu la
kiumbe wa baharini kwenye mwamba. Lilikuwa la kupendeza.
“Asante, Dolfina, Issa alimwambia Dolfina huku akimpapasa.
Dolfina alipozama tena alizuka na kikasha kidogo kizito.
Alikiweka pale alipokuwa ameweka kijiwe na susu. Issa
alikichukua kikasha na kumpapasa tena Dolfina. Dolfina
aliendelea na mchezo wake wa kutoa vitu baharini na kuweka
kwenye mwamba.Aliweka vitu vingi, lakini kilichomvutia Issa
ni kile kikasha.
“Nitampelekea Nyanya kikasha hiki. Pengine kina kitu kizuri
ndani, Issa alijisemea moyoni.
Kikasha chenyewe kilikuwa kimeshika ukungu na kilinuka
vumba. Issa alikichukua kikasha hicho hata hivyo. Alimuaga
Dolfina na kwenda zake nyumbani.
55
“Nyanya! Nyanya!” Issa alimwita nyanya yake kwa uchangamfu
alipofika nyumbani.
“Labeka!” aliitikia Nyanya.
“Nimekutana na Dolfina. Tena amenipa zawadi. Nimeamua
kuileta nyumbani, Issa alisema huku akielekea jikoni alikokuwa
nyanya yake. Nyanya alikikagua kikasha kisha akasema,“Ni
zawadi nzuri.Tena pengine ni ya gharama sana. Iweke hapo
mezani.Tutaifungua pamoja nikimaliza kudondoa pojo.
Nyanya na Issa waliketi kibandani mbele ya nyumba yao ili
wafungue kikasha.
Hakifunguki hiki. Pengine tukivunje, Issa alisema baada ya
kujaribu kufungua.
“Hebu kilete. Nitajaribu, nikishindwa tutakivunja, alisema
Nyanya.
Nyanya alifanikiwa kukifungua kile kikasha. Kilikuwa kimejaa
dhahabu.
“Lo! Siamini. Ni vito na dhahabu, alimaka Nyanya.
“Dolfina alitoa wapi dhahabu?” Issa aliuliza nyanya yake.
“Tulipokuwa wadogo tulisimuliwa ngano ya malkia mchoyo
aliyezama baharini na dhahabu zake. Pengine dhahabu hizi
ndizo hizo kwenye ngano, Nyanya alisema huku akitabasamu.
“Tafadhali nisimulie ngano hiyo, Nyanya, Issa aliomba.
“Nitakusimulia kwa ufupi tu. Ukitaka ufafanuzi ni baadaye.
Usiniulize maswali. Sitaki kupoteza muda, nina kazi nyingi,
alisema Nyanya.
56
“Sawa, Nyanya. Najua ngano ni za jioni, si za mchana. Kwa
ufupi tu tafadhali, Issa alimsihi nyanya yake.
“Hapo zamani za kale paliondokea malkia aliyekuwa na tamaa
kama ya fisi.Alitaka vitu vyote vizuri viwe vyake.Alikuwa na
farasi wengi, marinda mengi ya hariri, vito na dhahabu nyingi.
Malkia huyo aliwafanyisha watu kazi ngumu katika himaya yake
ili wamzalishie mali nyingi.Aliwatoza watu ushuru mkubwa ili
atajirike sana.Wakati mwingine watu walikesha makondeni na
baharini ili wamchumie. Malkia huyu aliuza malighafi ya nchi
yake katika nchi za nje.Alipata umaarufu mwingi kwa kuuza
mafuta na mbao. Baada ya muda nchi yake iligeuka jangwa.
Malkia huyu aliamua kuhamia nchi jirani iliyokuwa nzuri na
yenye mandhari mazuri ya miti na maua.Alibeba vitu vyake
vyote na kuvitia kwenye melikebu kubwa. Ilisemekana alivaa
dhahabu nyingi sana siku hiyo.Watu wa nchi yake walibaki
wakilia na kusaga meno. Melikebu yake ilipong’oa nanga
haikufika mbali. Ilianza kudidimia polepole. Malkia alilia kwa
sauti. Alianza kutupa vikasha vya dhahabu ili melikebu yake
ipunguze uzito isizame. Lakini wapi?
Malkia alikuwa amechelewa. Melikebu ilizama. Mjukuu wangu,
tamaa ni mbaya. Pengine kikasha hiki ni mojawapo ya vikasha
hivyo vya malkia huyo. Hadithi yangu imekomea hapo, Nyanya
alimaliza kusimulia.
“Watu hawakumwokoa?” Issa aliuliza kwa sauti ya huruma.
“Walijaribu lakini walishindwa. Issa, nimesema sitaki maswali,
Nyanya alimwonya Issa.
“Sawa, Nyanya. Nitakuuliza jioni, baada ya chajio, Issa alisema
huku akizuia kicheko.
Babu yake alipofika nyumbani alipokelewa kwa habari njema
za kikasha cha vito na dhahabu.
57
“Kikasha hiki kitabadilisha maisha yako, Issa.Ama kweli, wema
hauozi. Ndoto yako ya kuwa baharia mwanasayansi itatimia,
Babu alisema.
Babu alikipeleka kikasha hicho kwa rafiki yake aliyekuwa
mhunzi. Rafiki yake alimaka, “Lo! Umetajirika ndugu yangu.
Dhahabu hii na vito hivi ni vya gharama ya juu.
“Si mali yangu, ni mali ya mjukuu wangu, Babu alimjibu mhunzi.
Babu alirudi nyumbani akiwa mwenye bashasha.Alimwita Issa
na Nyanya ili wajadiliane kuhusu kikasha hicho.Alimwambia
Issa aamue alichotaka kukifanyia.
“Ninataka tukiweke kikasha hiki mahali salama. Tutakuwa
tunauza dhahabu au vito vichache tukihitaji hela. Ninataka
tujenge nyumba nzuri ili niwe na mahali pazuri pa kufanyia
kazi yangu ya shuleni. Ninataka mimi na wanamazingira
wenzangu tulipiwe karo yetu tusome hadi tunapotaka. Hata
Bi. Heri akitaka kuongezea masomo yake yatagharamiwa.
Nataka Babu ununue boti kubwa ili uweze kuimarisha kazi
yako ya uvuvi. Nataka pia nikiwa na wanamazingira wenzangu
tuanzishe kampeni maalum za kutetea pomboo wasidhulumiwa.
Tutatengeneza mabango makubwa yenye picha za pomboo
na maandishi. Tutayatundika upwani ili kila mtu ajionee na
kujisomea, Issa alielezea kwa furaha.
“Matakwa yote yatatimia, mjukuu wangu. Milango yako ya
neema imefunguka, alisema Nyanya.
58
Kamusi Yangu
ainati aina tofauti tofauti
amenaswa amekwama
bashasha furaha nyingi
kikasha kijisanduku kidogo
kumdara kumshika au kumgusa kidogo
makataa makubaliano ya sheria za utumizi wa kitu
mbadala tumika badala ya kitu kingine
mhunzi mfua vyuma
nitampeza kukosa mtu au kitu kwa muda mrefu
pomboo aina ya samaki mkubwa wa baharini
uhandisi taaluma ya uundaji wa vitu, mitambo
upwa sehemu ya pwani kati ya eneo la nchi
kavu na maji yanapoishia wakati bahari
inapojaa
ushuru ada inayotozwa wananchi na serikali
vumba harufu ya samaki
zimerundikana zimejaa
59
Maswali
1. Wanamazingira walifanya nini kila wikendi ya kwanza ya
mwezi?
2. Kwa nini chama cha mazingira katika shule ya msingi ya
Shimoni kilitia fora?
3. Mlezi wa chama cha mazingira alikuwa nani?
4. Kwa nini wanamazingira waliandika ilani?
5. Eleza vile ambavyo wanamazingira walivyoweza kumwona
pomboo aliyenaswa.
6. Je, unafikiri walinda upwa wana umuhimu gani?
7. Issa aliweza vipi kufanya urafiki na Dolfina?
8. Kwa nini ni hatia kwa wavuvi kutumia neti zenye matundu
madogo wanapovua?
9. Je, hadithi hii imekufundisha nini?
10.Kama ungekuwa Issa ungefanyia nini dhahabu uliyopewa
na Dolfina?
60
Mazoezi
Sehemu ya A
Kusikiliza na Kuzungumza
1. Ukiwa na rafiki yako zungumzeni kuhusu umuhimu wa
kuhifadhi mazingira. Maswali haya yatawaongoza;
a. Ni vitu gani ambavyo vinapatikana katika mazingira
yako?
b. Unafanya mambo gani ili kuhifadhi mazingira yako?
c. Usafi wa mazingira una umuhimu gani?
d. Kupanda miti kuna faida gani?
2. Mwombe rafiki yako akusomee kurasa zozote tatu za
hadithi hii, kisha akuulize maswali yoyote matatu kutokana
na kurasa hizo.
3. Msomee rafiki yako ukurasa mmoja wa hadithi hii. Mwombe
akuhesabie maneno ambayo unaweza kusoma kwa ufasaha
kwa dakika moja. Anaweza kukurekodi ukisoma kisha
mhesabu maneno hayo pamoja.
Sehemu B
Ufahamu wa Kusoma
Jibu maswali haya ukiwa na rafiki yako.
1. Kulingana na hadithi hii ni kweli wema hauozi. Fafanua.
2. Je, unafikiri kisa cha Nyanya kina ukweli wowote?
3. Wanamazingira walionyesha ubunifu wao vipi?
4. Je, ni kwa nini tunaweza kusema kuwa Dolfina ni mnyama
mwerevu?
61
Sehemu C
Matumizi ya Lugha
Soma kifungu kinachofuata. Kina nafasi 1 hadi 5.
Umepewa majibu hapo. Chagua jibu lifaalo zaidi kati
ya yale uliyopewa ili kujaza nafasi.
Usafi wa mazingira __1___ debe kwote ulimwenguni. Mazingira
safi hutuwezesha kuishi __2__ na dhiki ya magonjwa. Mazingira
__3__ safi maji na hewa huwa safi pia. Usafi wa mazingira ni
___4___ la kila mmoja wetu. __5__.Tuungane pamoja tuyatunze
mazingira kwa faida yetu na kizazi kijacho.
1. a. unapigishwa b. unapigishiwa
c. unapigiwa d. unapigwa
2. a. pasi b. bila c. kando d. mbali
3. a. ikiwa b. yakiwa c. pakiwa d. kukiwa
4. a. deni b. kanuni c. jukumu d. zamu
5. a. Hakuna refu lisilo na ncha.
b. Ukiviona vyaelea vimeundwa.
c. Mwenye macho haambiwi tazama.
d. Kinga na kinga ndipo moto huwakapo.
Sehemu D
Kuandika
Ni siku ya mazingira ulimwenguni. Umeteuliwa kuzungumzia
umuhimu wa usafi wa mazingira darasani mwenu. Andika
insha ya maelezo isiyopungua maneno 200 kuhusu umuhimu
wa usafi wa mazingira ili uwasomee wenzako darasani.
62
Shairi
63
Maadili
Ewe mtoto Adili, karibu keti kitini,
Nakufunza maadili, yanakili akilini,
Nawe usiwe bahili, yatie mtandaoni,
Ewe mtoto Adili, karibu keti kitini.
Kwanza nasema heshima, si utumwa nakwambia,
Heshimu baba na mama, baraka utapokea,
Mwalimu akikutuma, usichelewe kimbia,
Kwanza nasema heshima, si utumwa nakwambia.
Watendee watu haki, kisha dhuluma epuka,
Kumbuka mpanda haki, huvuna haki hakika,
Haizami kamwe haki, mwisho wake huibuka,
Watendee watu haki, kisha dhuluma epuka.
Usiwabague watu, kwa rangi wala jinsia,
Hata kilema ni mtu, kumbuka hakuchagua,
Chuki isikite kwetu, ukabila nakemea,
Usiwabague watu, kwa rangi wala jinsia,
Siku zote wajibika, bidii kazini tia,
Nyumbani unapofika, upende kusaidia,
Huvuta heri hakika, jitihada ukitia,
Siku zote wajibika, bidii kazini tia.
Tamati nimeshafika, mengi mema nimesema,
Rafiki mui epuka, ukitaka usalama,
Embe likiharibika, huoza pakacha zima,
Tamati nimeshafika, mengi mema nimesema.
64
65
Kamusi Yangu
bahili mtu mchoyo
dhuluma kitendo kisicho cha haki; uonevu
isikite isiwe imara
jitihada bidii kubwa
mui mtu mwovu
pakacha kifaa cha kubebea matunda kama vile
maembe ambacho husukwa kwa makuti
ya mnazi
yanakili yaandike mahali
66
Maswali
1. Ni nani anayefundishwa katika shairi hili?
2. Taja methali ambayo imezungumziwa katika ubeti wa pili.
3. Kwa mujibu wa mshairi heshima kwa wazazi ina faida gani?
4. Ni aina gani za ubaguzi ambazo mshairi ametaja katika
ubeti wa nne?
5. Kwa nini ni vizuri kuhimiza watoto wanaoishi na ulemavu
kucheza na wenzao?
6. Kwa maoni yako, ukabila una hasara gani katika jamii?
7. Eleza maana ya methali,‘Jitihada huvuta heri’.
8. Taja maadili yote yanayozungumziwa katika hadithi.
9. Shairi hili limekufunza nini?
10. Eleza umuhimu wa kuchagua marafiki wazuri.
67
Mazoezi
1. Ukiwa na mlezi au mzazi wako zungumzeni kuhusu maadili
katika jamii. Maswali haya yatawaongoza;
a. maadili ni nini?
b. unaweza kufanya nini ili uwe mtu mwadilifu?
c. ni matendo gani yanayoifanya jamii isiwe yenye maadili?
d. ukimwona mwenzako anafanya mambo yasiyo na maadili
utamsadia vipi kuirekebisha tabia yake?
2. Mkaririe mlezi au mzazi wako shairi hili. Mwombe akurekodi
kwenye kifaa cha kidijitali. Sikilizeni shairi ulilokariri huku
mkitathmini matamshi yako ya sauti na maneno katika
shairi. Unaweza kumtumia rafiki yako rekodi hiyo, akusikilize
na kukutathmini matamshi yako.
3. Ukiwa na mlezi au mzazi wako, tengenezeni kadi za maneno
ya maadili kama vile haki, huruma, bidii, upendo, amani,
heshima, wema na umoja. Zipambeni kadi hizo kwa rangi,
maua na mapambo mbalimbali.Tundikeni kadi hizo mahali
nyumbani ili watu wajisomee na kutathmini kazi yenu.
Kuandika
Unataka kuhimiza rafiki wadumishe maadili. Andika kifungu
kifupi cha maneno kuhusu umuhimu wa maadili katika jamii
ili uwasomee.