Dana ya
Ushairi
Diwani ya mashairi mepesi
Shule za Msingi
Sirivano Ayubu
Dana ya Ushairi
Kimechapishwa na Queenex Publishers Ltd
S.L.P 56049-00200, Nairobi, Kenya.
Simu: 0727 794 498, 0715 808 200
Barua pepe: info@queenexpublishers.co.ke
queenexbooks@gmail.com
Tovu: www.queenexpublishers.co.ke
©Queenex Publishers Ltd, 2019
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili, kupigisha chapa,
kutafsiri au kukitoa kitabu hiki kwa jinsi yoyote ile bila idhini, kwa
maandishi ya Queenex Publishers Limited.
Chapa ya kwanza 2019
ISBN: 978-9966-140-18-0
Yaliyomo
A. Sehemu ya Kwanza
Maelezo ya jumla kuhusu ushairi
B. Sehemu ya Pili
Mifano ya mashairi na maswali
Wanangu ........................................................................ 1
Asante kwa viungo ......................................................... 7
Tuwe kama mwewe ........................................................ 9
Ninatamani ..................................................................... 12
Nidhamu ......................................................................... 15
Ujasiri .............................................................................. 18
Dhuluma ......................................................................... 20
Peremende ....................................................................... 22
Waadhi ............................................................................ 24
Nina ................................................................................. 26
Wa porini ni dhahabu ...................................................... 28
Kiswahili lugha tamu ...................................................... 31
Dafina .............................................................................. 33
Twaa kisomo ni lulu ....................................................... 35
Mazingira tuyalinde ......................................................... 37
Ua zuri ............................................................................. 39
Swahibuye nani? ............................................................. 42
Ng’ombe wetu wa maziwa! ............................................. 44
Gezageza ndiyo mji .......................................................... 47
Mwanangu acha woga .................................................... 50
Saba za wiki .................................................................... 52
Vijana na elimu ............................................................... 55
Mwanangu nakutakasa ................................................... 57
Kielimika wasomi ............................................................ 60
C. Sehemu ya Tatu
Tamrini ya mashairi teule ........................................ 64
Sehemu ya Kwanza
Maelezo ya jumla kuhusu ushairi
i
1. Maana ya ushairi
Ushairi ni utungo wa kisanaa unaotumia lugha
teule na ya mkato pamoja na mpangilio maalum
wa maneno badala ya kutumia lugha ya kawaida
ili kupitisha ujumbe fulani.
2. Sifa za mashairi
Mashairi huwa na mizani, vina, mishororo na beti.
Mashairi hayazingatii kanuni za kisarufi.
Mashairi hutumia lugha ya mkato na teule.
Mashairi hutumia mbinu mbalimbali za lugha.
Mashairi hufupisha au kurefusha maneno.
3. Umuhimu wa mashairi
Kuelimisha Kuburudisha
Kuliwaza Kuelekeza
Kupitisha ujumbe
fulani
Kunasihi
Kusifia mtu au kitu Kukemea
Kukuza sanaa ya lugha Kuonya
Kuhamasisha jamii Kukejeli
4. Istilahi za mashairi
Mshororo ni msitari katika ubeti.
Mizani ni idadi ya silabi katika kila mshororo.
ii
Vina ni silabi za mwisho katika kila kipande cha
ubeti.
Ubeti ni fungu la mishororo.
Mwanzo mshororo wa kwanza katika ubeti.
Mloto mshororo wa pili katika ubeti.
Mleo mshororo wa tatu katika ubeti.
Vipande sehemu ya mshororo iliyogawanywa kwa
koma (,).
Ukwapi kipande cha kwanza katika mshororo.
Utao kipande cha pili katika mshororo.
Mwandamo kipande cha tatu katika mshororo.
Ukingo kipande cha nne katika mshororo.
Kibwagizo mshororo wa mwisho
unaorudiwarudiwa katika kila ubeti.
Kimalizio/Kiishio mshororo wa mwisho katika
ubeti usiorudiwarudiwa.
Ghani - tunga kwa mfano shairi au wimbo.
Malenga - mshairi maarufu, bingwa wa kutunga
mashairi na nyimbo.
Manju - mtu ambaye ni stadi wa kutunga na kuimba
nyimbo.
Sogora - fundi wa kupiga ngoma au kucheza densi,
fundi wa kusema na kutenda jambo.
Mlumbi - msemaji hodari.
iii
Mkalimani - mtu anayetafsiri mazungumzo papo
kwa papo kutoka lugha moja hadi nyingine.
Mshairi - mtunzi wa mashairi au tenzi.
5. Aina ya mashairi
Mashairi hugawanywa katika aina mbalimbali
kutegemea idadi ya mishororo katika kila ubeti.
Aina ya ushairi Maelezo
Tathmina/Umoja Shairi lenye mshororo mmoja katika
kila ubeti.
Tathnia/Uwili Shairi lenye mishororo miwili katika
kila ubeti.
Tathlitha/Utatu Shairi lenye mishororo mitatu katika
kila ubeti.
Tarbia/Unne Shairi lenye mishororo minne katika
kila ubeti.
Mashairi mengi ni ya aina ya tarbia.
Takhmisa/Utano Shairi lenye mishororo mitano katika
kila ubeti.
Tasdisa/Usita Shairi lenye mishororo sita katika kila
ubeti.
Tasbia/Usaba Shairi lenye mishororo saba katika
kila ubeti.
Ukumi Shairi lenye mishororo kumi katika
kila ubeti.
Maudhui
Maudhui ni ujumbe au mawazo mbalimbali
yanayojitokeza katika shairi fulani. Ni mambo ambayo
mshairi huzungumzia kwa mfano; bidii, ufisadi, elimu
na mengine.
Dhamira
Dhamira ni lengo kuu la mshairi. Mtunzi wa shairi
anaweza kuwa na dhamira au lengo la kuelimisha,
kuonya au kunasihi jamii kuhusu jambo fulani.
Mtindo wa lugha au mbinu
Mtindo wa lugha ni mbinu mbalimbali ambazo mshairi
ametumia katika kutunga shairi lake. Mbinu hizi ni
kama vile; methali, tashbihi, taswira, tanakali ya sauti,
utohozi na nyingine.
iv
Sehemu ya Pili
Mifano ya mashairi na maswali
1
Wanangu
2
Wanangu nikaribie, niwape huu wosia,
Naomba mzingatie, msikose kuridhia,
Masikio nipatie, upate kuwaingia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
Namba wani iwajie, heshima kuzingatia,
Umri msijalie, kumkosea raia,
Shikamoo palilie, miguu kushikilia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
Bidii mzingatie, sadiri kutojifia,
Maisha mvumilie, vyovyote kujikazia,
Mshindwapo kubalie, keshoye tatangulia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
Malengo yawafikie, lolote kijifanyia,
Yote myaratibie, na dira kujipatia,
Shabaha mjipimie, mavuno kujivunia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
Walo wema karibie, yalo mema kuigia,
Kila mja mkidhie, ya moyo kufurahia,
Mifano wawapigie, karia hadi karia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
Dua zote mpigie, Mungu wetu jaalia,
Njia awafungulie, nyoyo zipate tulia,
Kheri awajaalie, pamoya jitakasia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
Ghafuri ziwajilie, thawabu kukumbatia,
Hali iwaangazie, na fanaka kuachia,
Tamaa jiepushie, dhunubu sijepatia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
3
Wanangu radhi niwie, ukomo nimefikia,
Naomba niaminie, ya kuwa mmesikia,
Niache nikimbilie, nafasi kuandalia,
Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha.
(Mtunzi: Mtatago Tom Nyambeka)
Maneno mapya
1. wasia: pia wosia au usia. maelezo ya kushauri.
ushauri
2. sadiri: moyo, mtima, fuadi
3. karia: kijiji
4. dua: maombi
5. ghafuri: pia ghafuru (kidini) jina ambalo hutumiwa
aghalabu na waislamu kuashiria kuwa
mwenyezi mungu ana sifa ya kusamehe.
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Ngonjera
B. Takhmisa
C. Tarbia
D. Tathlita
2. Walengwa kwenye shairi hili ni?
A. wana
B. wanafunzi
C. wajukuu
D. jamii
4
3. Vina vya ndani na vya mwisho kwenye ubeti wa tatu
ni?
A. ie, ia
B. mzingatie, kujikazia
C. nipatie, kuwaingia
D. e, a
4. Neno thawabu lililotumiwa kwenye shairi lina
maana gani?
A. adabu
B. dhahabu
C. laana
D. baraka
5. “Kokoko najikohoza, siku zangu zimekwisha”, ni
mshororo unaorudiwarudiwa katika kila mwisho wa
ubeti. Jina lake halisi ni lipi?
A. ubeti
B. vina
C. kibwagizo
D. kiingilio
5
Wakubwa kuwaheshimu, hakika huwa muhimu,
Hudhihirisha nidhamu, tunofunzwa na walimu.
Takufanya mahashumu, kifanicho adimu.
Upendwe kila sehemu, hata wako mahasimu.
Isikuwe ya misimu, hata kidogo nidhamu.
Ipe ya kwanza rakamu, leo daima dawamu.
Kumbuka kiburi sumu, sikiachie hatamu,
Takufanya siheshimu, kukaidi uzuumu.
Kamwe siwe chakaramu, ‘dunisha hata walimu,
takupaje na elimu, uweze kuwa muhimu.
Kitaka wakuheshimu, kwanza fanya yako zamu,
Ukuwe mtakadamu, bila kutoa hukumu.
Sone kavaa mademu, kamwona so binadamu,
Bora si wako hirimu, siku zote mheshimu.
Maisha tawa matamu, staha kiwa hatamu,
Hatutaimwaga damu, kwani pendo litadumu.
(Mtunzi: Ken Bogonko, Malenga wa Milimani)
Maneno mapya
1. mahashumu: enye maana
2. adimu: isiyopatikana kwa urahisi
3. mahasimu: adui
4. rakamu: nambari
5. chakaramu: utundu
6. mtakadamu: ongoza
6
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Tarbia
B. Tathmina
C. Tathnia
D. Takhmisa
2. Lipe shairi hili kichwa mwafaka.
A. Heshima
B. Bidii
C. Ushujaa
D. Ujasiri
3. Shairi hili lina beti ngapi?
A. 2
B. 8
C. 9
D. 4
4. Nini maana ya neno ‘mademu’.
A. kimada
B. kidosho
C. tambara
D. wasichana warembo
5. Mtunzi wa shairi hili anaitwaje?
A. Sogora
B. Ken Bogongo
C. Manju
D. Malenga
7
Asante kwa Viungo
Viungo niumbieni, kuyaboresha maisha,
Kutoka mwangu kichwani, ubongo kunikumbusha,
Sisahau losomeni, maswali kunipitisha,
Hata nisoyajueni, akili itanipasha,
Namshukuru Manani, kwa viungo alonipa.
Masikio ni muhimu, kwa mengi huniwezesha,
Kusikia ya mwalimu, sikio huyapitisha,
Kisha yaliyo muhimu, na mambi hutenganisha,
Akilini yakadumu, masomo nikaboresha,
Namshukuru Manani, kwa viungo alonipa.
Macho sitayaacheni, kanipa yote mawili,
Yakini huniauni, kuweza kuona mbali,
Nisomapo darasani, huwezesha kunakili,
Yalotiwa ubaoni, ‘yapeleka kwa akili,
Namshukuru Manani, kwa viungo alonipa.
8
Hakusahau mdomo, ufanyao mzo kazi,
Huvilisha vyote vimo, kuviepusha gonezi,
Hukikuza changu kimo, sinilemee zoezi,
Nifaulu kwa masomo, kufeli kuwe tukizi,
Namshukuru Manani, kwa viungo alonipa.
Kanipa nayo mikono, miwili yenye vidole,
Yenye dhima changamano, ‘dumisha wangu udole,
Vidole vyote vitano, huandika hapa pale,
Masomo yawe mswano, nikwee hadi kilele,
Namshukuru Manani, kwa viungo alonipa.
Ninayo miguu yangu, kanipa yote miwili,
Isiyohisi uchungu, kuubeba wangu mwili,
Hunitwaa wanguwangu, kwenda nakostahili,
Niweze kutoka kwangu, lama ilipo skuli,
Namshukuru Manani, kwa viungo alonipa.
(Mtunzi: Ken Bogonko, Malenga wa Milimani)
Maswali
1. Mistari katika ubeti inaitwaje?
_________________________________________
2. Shairi lenye mishororo sita katika kila ubeti linaitwaje?
_________________________________________
3. Shairi hili linaitwaje?
________________________________________
4. Mwimbaji wa shairi anaitwaje?
_________________________________________
5. Mshororo wa kwanza katika ubeti unaitwaje?
_______________________________________
9
Tuwe kama Mwewe
Huyu mwewe hushangaza, mola livyomuumbeni,
Tabiaze zapendeza, yatupasa tuigeni,
Lomuumba kamutuza, vipaji mzo maishani,
Kutwa kucha huvikuza, vimwauni aushini,
Hana budi kujikweza, kuwapiku washindani,
Mwewe yu tofauti, na wengine hafanani.
Maoziye ni makali, huweza kuona mbali,
Hata kilicho akali, takiona kiwa mbali,
Wengine hujithakili, kupaona hapo mbali,
Yetu yanastahili, ‘zoeshwa kuona mbali,
Kalisha yetu akili, kwa lishe la kule mbali,
Mwewe huyu tofauti, na wengine hafanani.
Kijapo hicho mchela, kizungukacho ja pia,
Kwake huwa ni aula, wenzake wakikimbia,
Juu enda halahala, dhoruba kifurahia,
10
Kwetu mambi masuala, cha mchela kutishia,
Hata yawe zilizala, tutatuwe kitulia,
Mwewe huyu tofauti, na wengine hafanani.
Miaka mzo mepewa, ya kuishi duniani,
Na uzee kivamiwa, tarudishwa ujanani,
Nazo nguvu tarudiwa, kuliko hata mbeleni,
Nasi sije kuishiwa, nguvu zetu za mwanzoni,
Tusiweze kulemewa, na majojo maishani,
Mwewe huyu tofauti, na wengine hafanani.
Nyamafu yeye haili, windole hutegemea,
Hapo twaona idili, kwa windaji kabobea,
Nyuni wenza kithakili, mizogani kuzengea,
Nasi tunastahili, waja kutotegemea,
Tuvisake vya asili, tuepuke kuzembea,
Mwewe huyu tofauti, na wengine hafanani.
Makindawe huwafunza, wasitegemee mama,
Kwa idili huwatunza, kwani hiyo yake dhima,
Kuruka wajue kwanza, kijifunza na kuchuma,
Walimu nao hufunza, lilo hilo toka zama,
Tusije tukajiponza, ufalani tukazama,
Mwewe huyu tofauti, na wengine hafanani.
Kichagua masahibu, na hekima huongozwa,
Na wambi hujitanibu, uzembeni ‘toingizwa,
Na wenye nia harabu, asije akapumbazwa,
Upwekewe wa kuhibu, humwepusha na kutwezwa,
Yakini yake adabu, huwa njema kuigizwa,
Mwewe huyu tofauti, na wengine hafanani.
(Mtunzi: Ken Bogonko, Malenga wa Milimani)
11
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani? Toa sababu.
_________________________________________
2. Shairi hili lina beti ngapi?
_________________________________________
3. Mshororo wa kwanza katika ubeti unaitwaje?
_________________________________________
4. Mshororo wa pili katika ubeti unaitwaje?
_________________________________________
5. Shairi lenye mshororo mmoja linaitwaje?
_________________________________________
6. Shairi lenye mishororo miwili katika kila ubeti
linaitwaje?
_________________________________________
7. Shairi lenye mishororo mitatu katika kila ubeti
linaitwaje?
_________________________________________
8. Shairi lenye mishororo minne katika kila ubeti
linaitwaje?
_________________________________________
9. Shairi lenye mishororo mitano katika kila ubeti
linaitwaje?
_________________________________________
10.Shairi lenye mishororo saba katika kila ubeti
linaitwaje?
_________________________________________
12
Ninatamani
Ninatamani maisha, maisha ya utulivu,
Ninatamani kuisha, kuisha kwa upumbavu,
Ninatamani kulisha, kulisha waso wavivu,
Ninatamani maisha, maisha yenye mkesha.
Ninatamani idhini, idhini ya kuheshimu,
Ninatamani imani, imani inayodumu,
Ninatamani udini, udini usodhulumu,
Ninatamani amana, amana kunikidhia.
Ninatamani kilaji, kilaji kinishibishe,
Ninatamani upaji, upaji uwaridhishe,
Ninatamani utaji, utaji mnivalishe,
Ninatamani nishati, nishati ya kutendea.
Ninatamani malazi, malazi yanayokifu,
Ninatamani mavazi, mavazi yalo faafu,
Ninatamani uzazi, uzazi ulo shirifu,
Ninatamani hitaji, hitaji la kimsingi.
Ninatamani jirani, jirani wa ushirika,
Ninatamani utani, utani ‘sokasirika,
Ninatamani amini, amini loaminika,
Ninatamani ‘ungwana, uungwana wa kutenda.
Ninatamani majasho, majasho yangu mwenyewe,
Ninatamani mlisho, mlisho uso kiwewe,
Ninatamani mpisho, mpisho nikubaliwe,
Ninatamani kulila, kulila jasho la kwangu.
Ninatamani heshima, heshima kwa Mkawini,
Ninatamani kupima, kupima yalo thamani,
13
Ninatamani hekima, hekima ya kuamini,
Ninatamani ujuzi, ujuzi wa kuabudu.
Ninatamani kikomo, kikomo cha amuali,
Ninatamani rihamo, rihamo iliyo ali,
Ninatamani mkomo, mkomo wa udhalili,
Ninatamani kuradhi, kuradhi ya hapa dali.
(Mtunzi: Mtatago Tom Nyambeka)
Maneno mapya
1. wavivu: wazembe
2. usodhulumu: usionyima haki
3. kilaji: chakula
4. utani: mzaha
5. thamani: gharama ya juu
Maswali
1. Dhamira kuu ya shairi hili ni?
A. Kuwa na tamaa
B. Kutamani mambo mema
C. Kutamani kufa
D. Kutamani elimu
2. Taja kitu asichotamani mwandishi
A. Maisha ya utulivu
B. Kulisha walio wavivu
C. Idhini ya kuheshimu
D. Majasho yangu
14
3. Taja kiitikio cha shairi hili
A. Ninatamani maisha, maisha yenye mkesha.
B. Ninatamani amana, amana kunikidhia.
C. Ninatamani kuradhi, kuradhi ya hapa dali.
D. Ninatamani
4. Ni anwani ipi inayofaa zaidi kwa shairi hili?
A. Ninatamani maisha
B. Ninatamani idhini
C. Ninatamani kilaji
D. Ninatamani
15
Nidhamu
Upesi makinikeni, ya nidhamu kuzinduka,
Haiuzwi mnadani, huipati kwenye duka,
Huikuti vitabuni, haiwezi kusomeka,
Heshima chombo adhimu, heshima sio utumwa.
Adabu tunu jamani, mali yasiyotekeka,
Vijijini na mijini, heshima hutambulika,
Vyaelea vitamani, kwa adabu vyaumbika,
Heshima chombo adhimu, heshima sio utumwa.
16
Usiache asilani, taadhima kuishika.
Cha muhimu aushini, ni nidhamu kusikika,
Mja sio hayawani, ukikanywa we kanyika,
Heshima chombo adhimu, heshima sio utumwa.
Chukueni usukani, enyi mlo elimika,
Wakubwa muwapisheni, ya balaa kuepuka
Chumbani si msalani, mlango unabishika,
Heshima chombo adhimu, heshima sio utumwa.
Maadili yashikeni, yasije yakaponyoka
Daima tenda hisani, mwishoni yatalipika,
Yalo mawi epukeni, shikilia ya baraka.
Heshima chombo adhimu, heshima sio utumwa.
(Mtunzi: Irene Oilipo)
Maneno mapya
1. mnadani: sehemu ya kuuzia bidhaa kwa
kitangaza bei
2. hisani: wema
3. maadili: tabia njema
4. adhimu: enye sifa, tukufu
5. daima: bila kukoma
6. mawi: mambo mabaya
17
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Tarbia
B. Utenzi
C. Tathlitha
D. Takhmisa
2. Kila mshororo una mizani mingapi?
A. kumi
B. kumi na sita
C. nane
D. nne
3. Vina katika kila ubeti mighairi ya kibwagizo vinaishia
na mizani zipi?
A. ni, ka
B. ki, vi
C. mu, mwa
D. ka, ni
4. ‘Heshima sio utumwa’ ni aina ya
A. methali
B. takriri
C. tashbihi
D. kitendawili
5. Katika ubeti wa tatu, nidhamu inatambulika
wapi?
A. vijijini pekee
B. mijini pekee
C. vijijini na mijini
D. vijijini tu bila mijini
18
Ujasiri
Simama enyi jasiri, inuka msiogope,
Maisha sasa si siri, msiwe kama mapepe
Mambo kweli ni dhahiri, ela peupe pepepe!
Maisha ni jitihada, mkumbuke ipo siku.
Mjitie vitabuni, bila ya kutetereka,
Msojua ulizeni, pasipo kutetemeka,
Hata yawe ya kigeni, ujuzi mtauteka,
Maisha ni jitihada, mkumbuke ipo siku.
Ujasiri ni dhabiti, kwa walo jitumatuma,
Ni jiti la kiberiti, kwenye msitu mzima,
We mnyonge jizatiti, kwa kudura za Karima.
Maisha ni jitihada, mkumbuke ipo siku.
Jasiri huvuna mema, isitoshe hafi moyo,
Huwa hajishiki tama, hununa kimoyomoyo,
Jaribu bila kukoma, Maulana si mchoyo,
Maisha ni jitihada, mkumbuke ipo siku.
(Mtunzi: Irene Oilipo)
Maneno mapya
1. ujasiri: kufanya jambo bila woga
2. mapepe: kutotulia wala kufanya jambo kwa
makini
3. Karima: Mungu
4. Maulana: Mungu
5. kudura: nguvu zilizo za pekee kwa Mungu
19
Maswali
1. Taja kibwagizo cha shairi hili.
A. Mkumbuke ipo siku
B. Maisha ni jitihada
C. Maisha ni jitihada, mkumbuke ipo siku
D. Ujasiri
2. Jasiri huvuna mema, isitoshe hafi moyo. Mshororo
wa kwanza ubeti wa NNE. Maneno ‘kufa moyo’ ni
aina ya?
A. methali B. tashbihi C. semi D. kitendawili
3. Mshororo wa pili katika kila ubeti huitwaje?
A. mwanzo B. mloto C. kiitikio D. mleo
4. Kina cha mwisho katika kila ubeti huitwaje?
A. utao B. ukwapi C. mwandamizi D. kipokeo
5. Katika ubeti wa kwanza, maneno yepi ambayo ni
takriri?
A. Mkumbuke ipo siku
B. Ela peupe pepepe
C. Maisha ni jitihada
D. Msiwe kama mapepe
20
Dhuluma
Watoto tunalalama, mlipo nyote sikia,
Twalia hizi dhuluma, uwi mnatufanyia,
Mnatutia kilema, tunashindwa kukimbia,
Dhuluma hizi dhuluma, kwa watoto na zikome.
Hatujakuwa wazima, kuweza kujikidhia,
Tunaraushwa mapema, migundani kuingia,
Hata ng’ombe tunakama, machungani kuingia,
Dhuluma hizi dhuluma, kwa watoto na zikome.
Ndoa hizi za mapema, mipango kutupangia,
Tu wachanga kuwa mama, ndoani tukaingia,
Hayo si malezi mema, majuto tutajutia,
Dhuluma hizi dhuluma, kwa watoto na zikome.
Kwengine kwapangwa njama, vitani tukaingia,
Tuue kama wanyama, wenzetu kwenye dunia,
Tumukosee Karima, muumba wetu Jalia,
Dhuluma hizi dhuluma, kwa watoto na zikome.
Kichwa kinaponiuma, au nijapoumia,
Wachelea kunituma, sipitali kuingia,
Mwisho kifo cha mapema, toto kuaga dunia,
Dhuluma hizi dhuluma, kwa watoto na zikome.
(Mtunzi: Malenga wa migambani Nyagemi Nyamwaro
Mabuka)
21
Maneno mapya
1. dhuluma: kunyanyasa
2. aga dunia: kufa
3. chelea: chukua muda kabla ya kufanya jambo
4. Karima: Mwenyezi Mungu
5. panga njama: kupanga kutekeleza maovu
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Takhmisa B. Tathlita C. Tarbia D. Tasdisa
2. Shairi hili lina beti ngapi?
A. 4 B. 5 C. 8 D. 16
3. Kibwagizo cha shairi hili ni kipi?
A. Dhuluma hizi dhuluma, kwa watoto na zikome.
B. Dhuluma kwa watoto.
C. Dhuluma.
D. Watoto tunalalama.
4. Mtunzi wa mashairi huitwaje?
A. manju B. sogora C. saisi D. malenga
5. Mwandishi wa shairi hili anaitwaje?
A. Nyagemi Nyamwaro Mabuka
B. Malenga
C. Mtunzi
D. Hatujaambiwa
22
Peremende
Peremende peremende,
Tamutamu peremende,
Nakupenda peremende,
Rafiki au adui?
Una nini peremende,
Meno yangu uyatende,
Ukayafanya yafunde,
Rafiki au adui?
Ukiona kwenye pande,
Meno yangu peremende,
Metoboka pandepande,
Rafiki au adui?
Yanaingia mapande,
Ya chakula peremende,
Kutafuna kunishinde,
Rafiki au adui?
U sababu peremende,
Ya kinywa changu kivunde,
Nikupende unitende,
Rafiki au adui?
Heri nende niyatunde,
Nikiyala yanilinde,
Ni matunda niyapende,
Rafiki si adui!
(Mtunzi: Malenga wa migombani Nyagemi Nyamwaro
Mabuka)
23
Maneno mapya
1. uyatende: uyafanyie ubaya
2. yafunde: yatoe harufu mbaya
3. kivunde: yaoze
4. niyatunde: niyachume kutoka mtini
5. heri: afadhali
Maswali
1. Shairi hili lina mizani mingapi katika mshororo wa
kwanza ubeti wa kwanza?
A. 4 B. 8 C. 2 D. 18
2. Shairi hili lina beti ngapi?
A. 6
B. 4
C. 8
D. 2
3. Kibwagizo cha shairi hili ni kipi?
A. Rafiki au adui
B. Peremende
C. Adui
D. Rafiki
4. Vina vya shairi hivi ni vipi?
A. ki B. au C. nde D. ngu
5. Taja jina jingine la mstari katika ushairi.
A. ubeti B. mshororo
C. ukwapi D. mwanzo
24
Waadhi
Uketi chini kitako, faidi wangu waadhi,
Utege sikio lako, za moyo haja nikidhi,
Tanyosha tabia yako, tabia yenye kuudhi,
Kwayo moyo mkunjufu, pokea wangu waadhi.
Kuwa na moyo laini, ndilo jambo la thamani,
Asonacho kumwauni, mfanyie na hisani,
Kwani ndio urazini, kuwafaa masikini,
Kwayo moyo mkunjufu, pokea wangu waadhi.
Watoto walo shuleni, kwayo bidii someni,
Walimu waheshimuni, wakifunza darasani,
Mfanyeni na makini, mtumwapo kimbieni,
Kwayo moyo mkunjufu, pokea wangu waadhi.
Nakusihi ulitende, liwalo la maadili,
La kuudhi usitende, unalotenda ujali,
Ya manufaa yatende, tena useme ya kweli,
Kwayo moyo mkunjufu, pokea wangu waadhi.
Wangu mekupa waadhi, ukifanye mja bora,
Mja bora mwenye hadhi, asiyependa papara,
Na papara zinaudhi, zasababisha uchwara,
Kwayo moyo mkunjufu, pokea wangu waadhi.
(Mtunzi: Bonnie Lubisia)
Maneno mapya
waadhi: wosia; nasaha; mawaidha
kumwauni: tendo la kumsaidia mtu
25
urazini: kuwa na akili timamu
maadili: tabia nzuri; njema
papara: hali ya kuwa na haraka na kukosa
umakinifu
uchwara: tokuwa na thamani kubwa; duni
Maswali
1. Mshororo wa tatu katika ubeti wa tatu una mizani
mingapi?
A. minane B. saba
C. kumi na sita D. kumi na mitano
2. Kipande cha pili cha mshororo huitwa?
A. Utao B. Ukwapi
C. Mloto D. Mwandamizi
3. Kulingana na shairi, waadhi ni nini?
A. tabia mbaya
B. mawaidha mazuri
C. mawaidha ya kupotosha
D. nasaha ovyo
4. Taja kibwagizo cha shairi hili.
A. Keti chini kitako, faidi wangu waadhi
B. Wangu mekupa waadhi, ukufanye mja bora
C. Na papara zinaudhi, zasababisha uchwara.
D. Nayo moyo mkunjufu, pokea wangu waadhi
5. Taja jina jingine la mstari katika ushairi.
A. Ubeti B. Mshororo
C. Ukwapi D. Mwanzo
26
Nina
‘Kushukuru wangu mama, naomba leo fahamu,
Menitenda mengi mema, umenifunza nidhamu,
Nyendo zako naandama, hadi kwangu kuhitimu,
Kisogocho natazama, nina wangu na mwandani.
Tangu kwangu kuzaliwa, mekuwa wangu rafiki,
Wakati niliuguwa, tukaenda kiliniki,
Kisha kapata afuwa, we wangu kindakindaki,
Kisogocho natazama, nina wangu na mwandani.
Huwi wa kwanza kwa kula, wasubiri sote tule,
Tukule chetu chakula, hata kuramba vidole,
Halafu waomba sala, ili twende tukalale,
Kisogocho natazama, nina wangu na mwandani.
Pokea sifa sufufu, kutoka kwangu mwanao,
Si kwamba ‘namajisifu, wewe ndiwe wangu ngao,
Yanibidi nikusifu, macheo hadi machweo,
Kisogocho natazama, nina wangu na mwandani.
Beti tano zimetimu, ya mama nimeyasema,
Mama yangu mhashamu, nitakupenda daima,
Namuomba na Rahimu, akuzidishie mema,
Kisogocho natazama, nina wangu na mwandani.
(Mtunzi: Bonnie Lubisia)
Maneno mapya
1. nina: mama
2. kindakindaki: halisi, mkamilifu
3. sifa sufufu: sifa nyingi
27
4. macheo: asubuhi jua linapochomoza
5. machweo: jua linapotua
6. rahimu: jina la mwenyezi mungu linaloonesha
rehema zake
Maswali
1. Shairi hili lina beti ngapi?
A. sita
B. tano
C. nane
D. nne
2. Mtunzi wa mashairi huitwa?
A. malenga
B. manju
C. sogora
D. malenge
3. Shairi hili linamsifia nani?
A. baba
B. baba na mama
C. mama
D. mama na watoto
4. Kibwagizo cha shairi hili kina jumla ya mizani
mingapi?
A. 8 B. 7 C. 15 D. 16
5. Kipande cha kwanza cha shairi huitwa?
A. utao B. ukwapi C. mshororo D. kina
28
Wa Porini ni Dhahabu
Wanyama wenye thamani, wa faida chungu nzima,
Twawapata msituni, pa amani na salama,
Huko kwayo ni nyikani, siwafate na hasama,
Wa porini ni dhahabu, tuwafae watufae.
Onyo kwenu majangili, lojaa ubinafsi,
Mwazua kitendawili, twawaita ibilisi,
Mwaua bila kujali, vya haramu hamkosi,
Wa porini ni dhahabu, tuwafae watufae.
29
Wanyama mnawatesa, kiwachinja pate nyama,
Tabia yazua kisa, ishara kosa hekima,
Swara hawa nawanasa, kinofua yao nyama,
Wa porini ni dhahabu, tuwafae watufae.
Kizazi hiki cha sasa, ombi langu pokeeni,
Sifanye lolote kosa, kuwafweka wa porini,
Jiepushe na makosa, kuwandama wa nyikani,
Wa porini ni dhahabu, tuwafae watufae.
Nimejawa tumaini, itakoma hi kasumba,
Tushikaneni jamani, pamoja tuvute kamba,
Wanyama tuwatunzeni, sungura, tembo na simba,
Wa porini ni dhahabu, tuwafae watufae.
(Mtunzi: Bonnie Lubisia)
Maneno mapya
1. nyikani: sehemu kubwa iliyoota nyasi na miti
iliyotawanyika hapa na pale
2. majangili: mwindaji haramu wa wanyama pori
3. nasa: shika kwa kutumia mtego
4. ibilisi: shetani
5. kasumba: mawazo mabaya; dhana potovu.
30
Maswali
1. Shairi hili lina beti ngapi?
A. tano
B. nne
C. tatu
D. sita
2. Taja kina cha kati na cha mwisho cha ubeti wa
tano.
A. li, si
B. ni, mba
C. ni, ma
D. sa, ma
3. Shairi hili ni la aina gani?
A. Tasdisa
B. Takhimisa
C. Ukumi
D. Tarbia
4. Anayeghani mashairi huitwa?
A. manju
B. malenga
C. mshairi
D. msanii
5. Kipande cha pili cha shairi huitwa?
A. ubeti
B. mshororo
C. utao
D. ukwapi
31
Kiswahili Lugha Tamu
Mabingwa hongereni, kukikuza Kiswahili,
Wa pwani na wa barani, mwakienzi Kiswahili,
Nimejawa na shukrani, nakariri nanakili,
Kiswahili lugha tamu, ni tamu kama asali.
Lugha hii ni adhimu, Kiswahili kinalipa,
Ka hukujua fahamu, ni habari ninakupa,
Lugha hii ni karimu, nakariri na kuapa,
Kiswahili lugha tamu, ni tamu kama asali.
Wajichafua mwenyewe, kiongea shelabela,
Wajipakaza mwenyewe, unuke kila pahala,
Tajidunisha mwenyewe, uweze kuitwa fala,
Kiswahili lugha tamu, tamu kama asali.
Sikiza watangazaji, sauti zao nyerezi,
Hata na waigizaji, mekita yao mizizi,
Kiswahili chafariji, usiseme hauwezi,
Kiswahili lugha tamu, tamu kama asali.
Na kikomo nimefika, nilosema ni dhahiri,
Nadhani tumegutuka, nilonena yafikiri,
Tuweze kutajirika, maisha yenye fahari,
Kiswahili lugha tamu, tamu kama asali.
(Mtunzi: Bonnie Lubisia)
32
Maneno mapya
1. mwakienzi: mwakipenda
2. adhimu: iliyo na sifa na heshima kubwa
3. shelabela: ovyo ovyo; shaghalabaghala
4. sauti nyerezi: sauti nzuri; yenye kuvutia
5. dhahiri: waziwazi
Maswali
1. Shairi hili lina mishororo mingapi katika kila ubeti?
A. mitano B. minne
C. sita D. saba
2. Shairi hili ni la aina gani?
A. Arbia B. Utatu
C. Usita D. Takhimisa
3. Mtunzi wa mashairi huitwa?
A. manju B. msanii
C. sogora D. malenga
4. Kipande cha kwanza cha mshororo huitwa?
A. mwandamizi B. utao
C. ukwapi D. mwanzo
5. Lengo la mtunzi wa shairi hili ni
A. kuidunisha lugha ya Kiswahili.
B. kuisifu lugha ya Kiswahili.
C. kuikashifu lugha ya Kiswahili.
D. kuisuta lugha ya Kiswahili.
33
Dafina
Kikao ninafungua, nikujuvye usojua,
Dafina mekuletea, Kenya sa’ tunapepea,
Sote tunafurahia, na shangwe tunapigia,
Tumeshapata dafina, mtaala wetu mpya.
Unalenga vipaji, alivyotupa Muumba,
Mfano ukimbiaji, na pia kuruka kamba,
Wawa bora mchezaji, tamashani tukiimba,
Tumeshapata dafina, mtaala wetu mpya.
Kenya katika ramani, ya ubora duniani,
Tumeyacha ya zamani, tunazama vipajini,
Tuienzi kama mboni, mtaala tupendeni,
Tumeshapata dafina, mtaala wetu mpya.
Na sote tukumbatie, mtaala wetu mpya,
Naomba tusikatae, kufaidi yalo mapya,
Kileleni tufikie, nawe uwe mtu mpya,
Tumeshapata dafina, mtaala wetu mpya.
(Mtunzi: Bonnie Lubisia)
Maneno mapya
1. tamasha: michezo ya kuigiza, nyimbo na ngoma
2. ramani: picha ya nchi inayooneshwa kwenye
karatasi
3. mboni: sehemu ya jicho iliyozungukwa na duara
nyeusi
4. mtaala: mpango wa masomo ya kiwango fulani cha
elimu
34
Maswali
1. Mbona shairi hili liitwe tarbia?
A. Lina beti nne
B. Lina mishoshoro minne katika kila ubeti
C. Lina vipande viwili
D. Lina kibwagizo
2. Mtunzi wa mashairi huitwa?
A. mshairi
B. manju
C. malenga
D. bingwa
3. Mapigo ya sauti kwenye shairi huitwa?
A. vina
B. ukwapi
C. ubeti
D. mizani
4. Kina cha kati na cha mwisho cha ubeti wa tatu ni?
A. a, a
B. ji, mba
C. ni, ni
D. e, pya
5. Mstari wa pili katika ubeti wa shairi huitwa?
A. mwanzo
B. mloto
C. mleo
D. kibwagizo
35
Twaa Kisomo ni Lulu
Paka viatu rangi, kesho siku ni ya shule,
Sione muda husongi, ukashinda kwa kelele,
Vije vitabu hupangi, fua na sare ya shule,
Twaa elimu ni lulu, jipange enda shuleni.
Umeipa muda mwingi, runinga si nzuri vile,
Vipindi vya kwake vingi, si kama vile vya kale,
Vya kileo havijengi, vinakinza ya wavyele,
Twaa elimu ni lulu, jipange enda shuleni.
Acha na maringo mengi, uwapo katika shule,
Uwe kwamba huborongi, wali kuita mchele,
Wanafunzi wako wengi, ajira ni haba vile,
Twaa elimu ni lulu, jipange enda shuleni.
Mtoto mwema hapingi, ya walimu wake wale,
Na hapasui mitungi, kukomba uji wa shule,
Jibu maswali kwa wingi, na kuswali kwa upole,
Twaa elimu ni lulu, jipange enda shuleni.
Siseme kazi ni nyingi, na kitandani ulale,
Kulala hakutujengi, hulemaza polepole,
Acha ng’ano nyinginyingi, Moliwa akutawale,
Twaa elimu ni lulu, jipange enda shuleni.
(Mtunzi: Nyagemi Nyamwaro Mabuka, Malenga wa
Migombani)
36
Maneno mapya
1. fua: sasha
2. lulu: madini ya thamani yapatikanayo ardhini
3. huborongi: kuharibu
4. haba: isiyotosha
5. ng’ano: hadithi
Maswali
1. Shairi hili lina mishororo mingapi?
A. 2 B. 4 C. 8 D.16
2. Shairi hili lina beti ngapi?
A. 8 B. 16 C. 12 D. 5
3. Kibwagizo cha shairi hili ni kipi?
A. Elimu
B. Twaa
C. Twaa elimu ni lulu, jipange enda shuleni
D. Enda shuleni
4. Vina vya kati na mwisho ni vipi?
A. ngi, le B. le, ngi
C. lu, ni D. ni, lu
5. Mtunzi wa shairi anaitwaje?
A. malenga B. nyagemi
C. migombani D. mtunzi
37
Mazingira Tuyalinde
Ya mgambo naipiga, ikafike vilimani,
Nyote mje bila woga, habari niwaambieni,
Tukalitilie njuga, jambo hili wahisani,
Mola ametuzawidi, mazingira tuyalinde.
Simameni kipembeni, uitazame dunia,
Miti imekita chini, rangiye inavutia,
Na majito mabondeni, yazidi kuchirizia,
Mola ametuzawidi, mazingira tuyalinde.
Hewa safi twapumua, sibanange kwa viwanda,
Moshi angani kupaa, na madhara kuyapanda,
Kansa wengi taugua, makao yao kitanda,
Mola ametuzawidi, mazingira tuyalinde.
Mbio sijipurukishe, kama washenzi jamani,
Chemchemi tukaushe, miti kiibwaga chini,
Mwisho wake ututishe, mabwawa kukausheni,
Mola ametuzawidi, mazingira tuyalinde.
Nayo taka viamboni, ovyoovyo sitapaze,
Karatasi za naloni, katu tusisiagize,
Tufukie mashimoni, chupa tusisipuuze,
Mola ametuzawidi, mazingira tuyalinde.
(Mtunzi: Dickson Matiabe)
Maneno mapya
1. tukalitilie njuga: tulijadili kwa undani
2. chemchemi: sehemu inayotiririsha maji kutoka
ardhini
38
3. kama washenzi: kama wasio na busara
4. imekita chini: imeota chini
5. tufukie: tufunike kwa mchanga/tuzike
6. sibanange: siharibu
7. yazidi kuchirizia: yazidi kutiririka
Maswali
1. Shairi hili lina beti ngapi?
A. nne B. halina beti C. tano D. mbili
2. Taja ugonjwa mmoja unaoweza kusababishwa na
uchafuzi wa mazingira kwa mujibu wa shairi hili.
A. Malaria B. Kansa C. Kisukari D. Kisonono
3. Ipi hapa sio njia ya kuharibu mazingira?
A. kutupa taka
B. moshi wa viwandani kupaa angani
C. kupanda miti
D. kukata miti
4. Mshairi ametumia ‘ninawaambieni’ badala ya
‘ninawaambia’. Mbinu hii huitwaje?
A. ufupishaji B. methali
C. urefushaji D. lahaja
5. Ipi hapa huthibitisha ukweli wa kauli ‘Mola
ametuzawidi’ katika shairi hili.
A. Tukijenga viwanda
B. Tuna hewa safi
C. Tunaweza kukata miti
D. Tunapokausha mabwawa
39
Ua Zuri
40
Maisha ya siku hizi, si rahisi ni magumu,
Mtu chochote hawezi, kama bado kuhitimu,
Angalitoa machozi, yalo mekundu ja damu,
Nalipenda ua zuri, ua hilo ni elimu.
Ua hilo ni elimu, vizuri linanukia,
Kesho nikawe hakimu, jamii kusaidia,
Niwe mtu maalumu, tena mwenye manufaa,
Nalipenda ua zuri, ua hilo ni elimu.
Ua hilo ni elimu, ninalopenda kwa ari,
Wengi walo na elimu, wanamiliki magari,
Nyumba wanostakimu, ni kubwa za kifahari,
Nalipenda ua zuri, babu alilonambia.
Babu alilonambia, elimu ni ufunguo,
Katika hii dunia, nitumie kama ngao,
Ndiyo njia maridhia, ilo na mafanikio,
Nalipenda ua zuri, sitowacha kulisaka.
Sitawacha kulisaka, ua langu lilo zuri,
Shuleni mie tafika, ili nitie idiri,
Jitihada nitaweka, nikaifanye dahari,
Nalipenda ua zuri, ua hilo ni elimu.
(Mtunzi: Dickson Matiabe)
41
Maneno mapya
1. mekundu ja damu: mekundu kama damu
2. mtu maalumu: mtu wa kipekee
3. nyumba wanostakimu: nyumba wanazoishi
4. njia maridhia: njia isiyokuwa na dosari/ njia
iliyonyooka
Maswali
1. Taja kichwa kingine kitakachoafiki shairi hili.
A. Elimu
B. Maisha
C. Ujana wangu
D. Dunia ni ngumu
2. ‘Mekundu ja damu’. Hii ni tamathali ipi ya usemi
iliyotumika katika shairi hili?
A. Istiara
B. Methali
C. Takriri
D. Tashbihi
3. Walio na elimu wamenufaika kivipi?
A. Wanaweza kujikimu
B. Hugonjeka kila mara
C. Wanakula hadi wanashiba
D. Hupata ua zuri
4. Taja aina ya shairi hili.
A. Kikwamba
B. Pindu
C. Takhmisa
D. Tathlitha
42
Swahibuye Nani?
Hushangaza ni wa shani, japo mdogo jamani,
Vitimbi vyenye uzani, anavienzi moyoni,
Kumtafuta machoni, maskani na mapipani,
Swahibuye nani?
Umpatapo kwa njia, mchokozi namba wani,
Mara kichwani hutua, nayo heshima hanani,
Wapenzi wake jamaa, wachafu matembezini,
Swahibuye nani?
Atuapo chakulani, vimelea huvitia,
Matumbo humlaani, tembe chungu kimezea,
Mipaka kamwe hanani, juu na chini hutua,
Swahibuye nani?
Ukiwa safi mwilini, kwako ni nduli jamaa,
Uchafu ukutiani, upitapo kwenye njia,
Hujikunyata mbioni, kofi sije kimtua,
Swahibuye nani?
Daima hakosekani, kote yeye yu’ mbioni,
Familiaye jamani, ni mchanga baharini,
Mara yupo hotelini, hata palipo wageni,
Swahibuye nani?
Swahibuye haswa nani, japo kaumba Manani,
Msiwe kimya semeni, nipate kwona machoni,
Isiyokera moyoni, tabiaye nambieni,
Swahibuye nani?
(Mtunzi: Dickson Matiabe)
43
Maneno Mapya:
1. swahibu: raki, mwandani
2. ni wa shani: ni wa ajabu/ ni wa kushangaza
3. nduli: adui
4. manani: Mungu, Mola
5. isiyokera: isiyochukiza
Maswali
1. Eleza mdudu anayerejelewa katika shairi hili.
A. mbung’o B. nzi
C. nyuki D. wembembe
2. Mdudu anayerejelewa hupenda watu wa aina gani?
A. wanaopita njiani B. wachafu kwenye njia
C. wasafi D. walio hotelini
3. Eleza dhana ‘famiaye jamani, ni mchanga baharini.
A. Ni wengi kama mchanga
B. Wanaishi baharini
C. Ni wadogo sana
D. Huwezi kuwaona
4. Anayetunga mashairi huitwaje?
A. malenga B. mkalimani
C. ngariba D. manju
5. Shairi hili ni la aina gani?
A. umoja B. utatu
C. uwili D. unne
44
Ngombe Wetu wa Maziwa!
Jina lake ni Nyausi, ng’ombe wetu wa maziwa,
Ni mnene na mweusi, shingo pana kaumbiwa,
Hula migomba na nyasi, malishoni akikuwa,
Ng’ombe wetu wa maziwa, hulisha kule bondeni.
Baba alimnunua, toka mnada wa mbali,
Sote tukafurahia, taboreka yetu hali,
Maziwa atatufaa, mengine yatufadhili,
Ng’ombe kwetu wa maziwa, hulisha kule bondeni.
45
Tumemjengea zizi, karibu na nyumba yetu,
Mumo tunamfungia, asiibwe ng’ombe wetu,
Baba humchungulia, asimle mbwa mwitu,
Ng’ombe wetu wa maziwa, hulisha kule bondeni.
Asubuhi hudamka, twende naye mabondeni,
Kule sie tukifika, humlisha kwa majani,
Mtoni humpeleka, kwa kupita vichoroni,
Ng’ombe wetu wa maziwa, hulisha kule bondeni.
Humletea mabua, toka mwetu mashambani,
Mabingobingo hutoa, kuyafikisha nyumbani,
Na kupe humwondolea, kwa dawa za madukani,
Ng’ombe wetu wa maziwa, hulisha kule bondeni.
(Mtunzi: Dickson Matiabe)
Maneno mapya
1. mabua: shina la mmea kama hindi au mtama
2. mabingobingo: nyasi ngumu zinazopandwa na
kukatwa kulisha mifugo
3. mnada: sehemu ya kuuzia vitu
4. hudamka: huamka, hurauka
5. taboreka: itaimarika vizuri
46
Maswali
1. Hili ni shairi la aina gani?
A. Tarbia
B. Takhmisa
C. Tathnia
D. Shairi huru
2. Ni kipi hapa sicho chakula ambacho ng’ombe wa
mhusika hulishwa?
A. migomba
B. mabingobingo
C. nyasi
D. mlizamu
3. Ni kwa njia gani mshairi amehakikisha ng’ombe
wao wa maziwa haibwi usiku?
A. Huenda naye bondeni
B. Humpeleka mtoni
C. Wamemjengea zizi
D. Humletea mabingobingo
4. Ipi kati ya hizi sio sifa ya ng’ombe wa mhusika?
A. Huitwa Nyausi
B. Ni mnene na mweusi
C. Alinunuliwa kutoka soko la mbali
D. Ni mkali
47
Gezageza Ndiyo Mji
Ewe Saida dadangu, mtoto wa mama yangu,
Ufunguapo kitabu, usitie nanga katu,
Siingiwe na uvivu, kaifanye kazi kuntu,
Gezageza ndiyo mji, walishanena wahenga.
Ifanye hiyo hesabu, siione ni adhabu,
Akufunzapo mwalimu, makinika dada yangu,
Mazoezi angalau, yawe ya kwako gurufu,
Gezageza ndiyo mji, walishanena wahenga.
Kiswahili si kigumu, kasome mengi mabuku,
Kiingereza kitamu, elewa yote mafungu,
Yafanye kama chingamu, masomo haya adhimu,
Gezageza ndiyo mji, walishanena wahenga.
Sayansi nayo muhimu, mazingira tafahamu,
Somo la jamii ndugu, lifanye kama motifu,
Dini nayo sisahau, itafune kama njugu,
Gezageza ndiyo mji, walishanena wahenga.
Ewe Saida dadangu, idumishe na adabu,
Yafuate maamuru, itakuwa maasumu,
Mwalimu simpe tabu, uwe mtu wa nidhamu,
Gezageza ndiyo mji, walishanena wahenga.
(Mtunzi: Daniel Siwa)
48
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Tarbia
B. Tabdila
C. Takhmisa
D. Tathlitha
2. Lipe shairi hili kichwa mwafaka kando na
ulichopewa.
A. Bidii hufaidi
B. Umuhimu wa Kiswahili
C. Faida ya masomo
D. Saida
3. Shairi hili lina beti ngapi?
A. 4 B. 5 C. 20 D. 2
4. Mzungumzaji na mzungumziwa wa utungo huu ni
nani?
A. Ndugu, dadangu
B. Saida, dadangu
C. Dadangu, Saida
D. Ndugu, Saida
5. Taja methali iliyotumika katika utungo huu wa
kishairi.
A. Gezageza ndiyo mji
B. Itafune kama njugu
C. Yawe ya kwako gufuru
D. Yafanye kama chingamu
49
6. Jambo moja kati ya haya halijatajwa katika ubeti
wa mwisho. Ni lipi?
A. Adabu
B. Kufuata sheria
C. Nidhamu
D. Kumtaabisha mwalimu
7. Mshairi anasema somo la sayansi lina umuhimu upi
katika jamii?
A. Kupita mtihani
B. Kufahamu mazingira
C. Kuifanya motifu
D. Ni muhimu
8. Taja kibwagizo katika shairi hili
A. Gezageza ndiyo mji,
B. Walishanena wahenga
C. Ewe Saida dadangu
D. Gezageza ndiyo mji, walishanena wahenga
50
Mwanangu Acha Woga
Mashujaa wa uhuru, walijawa ujasiri,
Waliimwaga damu, wakoloni ‘lipojiri,
Wakuogopa mitutu, minajili ukombozi,
Mwanangu acha uoga, utimize ndoto zako.
Tazama simba wa nyika, si mrefu njorinjori,
Si mjanja ja sungura, si mkali kama ngiri,
Ila wote huwaua, kwa sababu ni jasiri,
Mwanangu acha uoga, utimize ndoto zako.
Nanasi ni tunda tamu, lamea kati mibani,
Hukua nayo ilhamu, na utamu wa asali,
Si chachu kama limau, licha ya kua mibani,
Mwanangu acha uoga, utimize ndoto zako.
Mama Wangari Mathai, mametu aliyeishi,
Litunza maliasili, zaraa ikanawiri,
Kasumba aliiasi, akaishinda Nobeli
Mwanangu acha uoga, utimize ndoto zako.
Ya mazidadi sinayo, nimefika hitimisho,
Yafungue masikio, ondoa mfarakano,
Woga uupe mgongo, jusuru fumbua jicho,
Mwanangu acha uoga, utimize ndoto zako.
(Mtunzi: Daniel Siwa)
51
Maswali
1. Shairi hili lina mishororo mingapi katika kila ubeti?
A. mitano C. minne
B. ishirini D. miwili
2. Ni sifa ipi ambayo simba anayo inayowazidi
wanyama wengine kulingana na ubeti wa pili?
A. Mjanja ja sungura
B. Mrefu njorinjori
C. Mkali
D. jasiri
3. Ni shujaa yupi ambaye ametajwa katika shairi hili?
A. Uhuru Kenyatta
B. Simba
C. Wangari Mathai
D. Mwanangu
4. Taja isitiara iliyotumika katika shairi hili.
A. Mkali kama ngiri
B. Mrefu njorinjori
C. Kasumba aliiasi
D. Utamu wa asali
5. Ni ujumbe upi ambao mshairi anawasilisha kupitia
mfano wa nanasi?
A. Kuvumilia hali
B. Kukwepa majaribu
C. Kukua mibani
D. Kuwa na utamu
52
6. Taja methali inayoweza kutumika kueleza ujumbe
unaozumguziwa katika shairi.
A. Uzuri wa mkakasi ndani kipande cha mtu
B. Mtaka cha mvunguni sharti ainame
C. Kunguru mwoga hufukuza ubawa wake
D. Ogopa ni ngao pia
Saba za Wiki
Jumatatu, siku ya awali, shuleni,
Niamkapo, natia mabuku , mkobani,
Njiani, nakimbia niwahi, darasani,
Mimi mwanagenzi.
Jumanne, siku ya pili, shuleni,
Nawasilisha, kazi ya ziada, ofisini,
Namakinika, nazitoa nta, masikioni,
Niupate ufahamu.
Jumatano, siku ya tatu, shuleni,
Najinoa, makali yangu, vilabuni,
Nachangia, hoja nyingi, mjadalani,
Niukuze ulumbi
Alhamisi, siku ya nne, shuleni,
Awasili, mgeni wetu, ukumbini,
Atushauri, tutie bidii, maishani,
Tuondoe uvivu.
Ijumaa, siku ya tano, shuleni,
Mwalimu mkuu, atuhimiza, gwarideni,
Na jioni, nacheza soka, uwanjani,
Niikuze talanta.
53
Jumamosi, ni nyumbani, mapumzikoni,
Nawasaidia, wazazi wangu, shambani,
Na usiku, ninadurusu vitabu, mezani,
Nazidisha uwajibikaji.
Jumapili, naamkia mapema, kanisani
Twahubiriwa, kwa maandiko, Bibiliani,
Twaombewa, ili asitujaribu, shetani,
Nakuza imani.
(Mtunzi: Daniel Siwa)
Maswali
1. Kando na kichwa ulichopewa, chagua kichwa
kingine mwafaka kwa utungo huu
A. Mtoto nenda shuleni
B. Siku za juma
C. Nakuza imani
D. Nakuza ulumbi
2. Taja kibwagizo cha shairi hili
A. Niukuze
B. Saba za wiki
C. Nazidisha uwajibikaji
D. Hamna kati ya vilivyotajwa
3. Andika vina vya nje vya shairi hili.
A. /ni/, /ni/
B. /ni/
C. /si/, /ne/, /ni/
D. /ji/
54
4. Mishororo mitatu ya kwanza katika kila ubeti ina
vipande vingapi?
A. Vitatu
B. Kimoja
C. Vinne
D. Kumi
5. Mambo matatu yafuatayo yanazungumziwa na
mshairi isipokuwa jambo moja. Ni lipi?
A. Maadili
B. Uwajibikaji
C. Talanta
D. Ushauri.
55
Vijana na Elimu
Nataka kuyasemeni, vijana muyasikie,
Muyatie akilini, kisha muyazingatie,
Yaumiza mtimani, mfanyayo yaachie,
Zingatieni elimu, ya duniya mewazidi.
Mihadarati hapana, weye siye mpedozi,
Utakuwa wa kupuna, ushindwe kufanya kazi,
Uwe mtu wa vikona, na tena utiwe wizi,
Zingatieni elimu, ya duniya mewazidi.
Na la mimba huumiza, vijana nawambieni,
Masomo utakwamiza, au kifi kitiwani,
Magonjwa yatavamiza, mwisho iwe kaburini,
Zingatieni elimu, ya duniya mewazidi
Tabia mbovu acheni, nawarai sikizeni,
Muuwache na uhuni, sheria isiwahini,
Muyatie maanani, ninawasihi wendani,
Zingatieni elimu, ya duniya mewazidi.
Hadi tama kituoni, naomba yafikirie,
Tusiingie shimoni, wosia uzingatie,
Naomba sote tulani, mikosi situpatie,
Zingatieni elimu, ya duniya mewazidi.
(Mtunzi: Daniel Siwa)
56
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Tathlitha
B. Tathmina
C. Tarbia
D. Takhmisa
2. Ni jambo lipi ambalo mshairi anamkataza
mwanafunzi asifanye kulingana na shairi hili?
A. elimu
B. mihadarati
C. kifo
D. upendo
3. Kila mshororo una mizani mingapi katika kila ubeti
wa shairi hili?
A. 8 B. 16 C. 32 D. 64
4. Ni nini athari ya mimba za mapema kwa
mwanafunzi kulingana na shairi?
A. kifo
B. kuzaa
C. malezi
D. kuacha elimu
5. Taja vina vya kati na vya mwisho katika ubeti wa
nne.
A. /ni/, /ni/
B. /mu/, /di/
C. /ta/, /ni/
D. /mu/, /mu/
57
Mwanangu Nakutakasa
Mwanangu ulo basiri, kaa kitako nikwambe,
Kwedheha yalonijiri, nitangulize maambe,
Leka ‘kutowe usiri, usio tungu ya tembe,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Chekechea mafunzoni, lieleka kishupavu,
Utambazi masomoni, ukirejea mchovu,
Ukatokwa darasani, ubwabwa wa uungavu,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Nakushukuru mwanangu, hukuendea vilo viwi,
Namshukuru na Mungu, alikwepeza na wawi,
Ukanisikia tangu, hukufaza yalo mawi,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Hapa sasa waUkwea, kwa sauti kukoroma,
Vinyele vinakumea, utoto unakukoma,
Maraha yanakwandama, meIngiwa na uzima,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Hapa ninakutongowa, muwangaza ‘kuolele,
Usije ukazidiwa, ukajikwaa madole,
Ukazitumia dawa, na vichuna uwavile,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Endapo utabarizi, wakati wa likizoni,
Nakurai umaizi, kumuabudu Manani,
Ufaze na mazowezi, ya Kiswahili wivani,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
58
Kaa tini unukuu, ya dunia si matoto,
Kuwa ukuwe ukuu, ujana sio utoto,
Utukuke utukuu, wa kuume na kushoto,
Mwanangu nakutakasa, na sikuchambi adhabu.
Ni nyaka tena zaidi, Ilo mbee sekondari,
Jifaidi hufaidi, kisomo ni utajiri,
Ndo msingi tangu jadi, ya kuweza kumahiri,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Mwenendo ndia kiguu, upitapo soto poto,
Zinga uzinge nafuu, mibani palo kokoto,
Siyatapiye makuu, takusokota sokoto,
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
Nimemaliza muanga , naenda zangu salama.
Ukurasa naufunga, malezi yangu ya mana.
Ndimi mlezi malenga, kwaheri ya kuonana.
Nakutakasa mwanangu, na sikuchambi adhabu.
(Mtunzi: Phibbian Muthama, Malenga mlezi)
Maneno mapya
1. basiri: mwerevu
2. leka: acha (nikupe siri)
3. maraha: raha (ukubwa)
4. wivani: kuiva/upate kujua/uerevuke
59
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Upili C. Utatu
B. Unne D. Hakuna jibu
2. Eleza maana ya neno ‘ubwabwa’.
A. uji
B. uchafu wa shingoni
C. kamba
D. ubawa
3. Methali yenye maana sawa na usemi, ‘Nakutakasa
mwanangu, na sikuchambi adhabu’ ni ipi?
A. Mtoto umleavyo ndivyo akuavyo
B. Udongo upatilize uli maji
C. Mtoto ufuata kisogo cha ninake
D. Mtaka cha mvunguni sharti ainame.
4. Ubeti wa tisa unahimiza yafuatayo isipokuwa:
A. Upitapo soto poto
B. Mibani palo kokoto
C. Takusokota sokoto
D. Sikuchambi adabu
5. Mwimbaji wa shairi huitwaje?
A. sogora
B. malenga
C. manju
D. mshairi
60
Kielimika Wasomi
Nipo mbele kiwandani, wenu mzuri mghani,
Ndewe zenu mnipani, niweze kuwambieni,
Yanotiya tewenguni, na wingi wa taabani,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
Mtukumbuke wazazi, itakuwa ni heshima,
Katika yenu makazi, ndicho kitu muadhama,
Kizuri kielekezi, ya maisha yalo mema,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
61
Mtukumbuke wazazi, baraka walalieni,
Nawasema mumaizi, ni yake Mungu kanuni,
Msiole ni upuzi, kapuuza wasiani,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
Mtukumbuke wazazi, pindi mnapo hitimu,
Nawaamba yalo wazi, msije kunihujumu,
Ela mkipata kazi, kutulinda siwe ngumu,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
Mtukumbuke wazazi, ndio yangu aadili,
Mtuvishe na mavazi, na mengineo aali,
Fanyeni upelelezi, mtapata ni ya kweli,
Kielimika wasomi, mtukumbukeni wazazi.
Mtukumbuke wazazi, ‘pate baraka yakini,
Tupate vya kubarizi, wakati wa uzeeni,
Tung’ae sura na ngozi, enyi wetu wahisani,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
Mtukumbuke wazazi, msisahau hisani,
Enyi wa yeo wayuzi, mkasahau zamani,
Mkawa tena hamwezi, keti nasi barazani,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
Mtukumbuke wazazi, na pia mtuheshimu,
Kiwa mwona ni upuzi, mjuwe mwajihasimu,
Nakoma uzungumzi, mghani wenu adhimu,
Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
(Mtunzi: Phibbian Muthama, Malenga Mlezi)
62
Maneno Mapya
1. tewengu(ni): wasiwasi
2. msiole: msione
3. mumaizi: mtambue
4. mwajihasimu: mwajitakia uadui
Maswali
1. Shairi hili ni la aina gani?
A. Takhmisa
B. Tathlita
C. Nne
D. Hakuna jibu.
2. Taja mleo wa ubeti wa saba.
A. Mtukumbuke wazazi, msisahau hisani.
B. Enyi wa yeo wayuzi, mkasahau zamani.
C. Mkawa tena hamwezi, kuketi nasi barazani
D. Kielimika wasomi, mtukumbuke wazazi.
3. Kwa nini mtunzi ameradidi mshororo wa mwisho
katika beti zote?
A. Kwa sababu ni tarbia
B. Kwa sababu ni njonjera
C. Kwa sababu ni mloto
D. Kwa sababu ni kibwagizo.
4. Si sawa kusema kwamba:
A. Mama adekezwe
B. Mama apambwe
C. Mama apewe pesa
D. Mama apewe matibabu
63
Sehemu ya Tatu
Tamrini ya Mashairi Teule
Yametungwa na Gaceri Martha
Almaarufu Sheeri Gee
64
Nitapaa
Usione nanyamaa, udhani sitatembea,
Nasota huku nalia, udhani nimelemaa,
Haja ninajiendea, ufikiri sitapaa,
Siku yangu yawadia, ninajua nitapaa.
Usione sijafaa, eti mie ni fukara,
Chakula kwangu balaa, mapipani nachakura,
Ngozi imeshachakaa, jinsi nilivyoparara,
Jua sikati tamaa, ipo siku nitang’ara.
Usione nanyamaa, ukadhani mie juha,
Kimya kimya ninakaa, ukadhani ni fedheha,
Maongezi nakataa, udhani sina furaha,
Vyote kwangu ni hewaa, na usidhani mzaha.
Dunia Itakuhadaa
Bui wangu sikiliza, mambo ninayokwambia,
Usije ukaniliza, sipobadili tabia,
Dunia itakumeza, vibaya kikanyagia,
Pia itakupoteza, kifuata zake hadaa.
Wangapi wamejifia, tahadhari wakipewa,
Magwiji jilidhania, kumbe wao kapagawa,
Pipi walizibugia, bila wao kubaguwa,
Kote walikotembea, wamesha sahauliwa.
Dunia itakuhadaa, imejaa ubatili,
Keti chini fikiria, tumia zako akili,
Ukitaka kutembea, situmie njia mbili,
Bora moja kuchagua, na tena iliyotuli.
65
Ni vyema hapa kukoma, ujumbe nimepitisha,
Usije ukalalama, kwa mengi ninakuchosha,
Iwapoumeyasoma, basi haya yakutosha,
Rabana akupe mema, na yenye heri maisha.
Lini Tafika Kileleni
Jasho mistari lachora, mbio pumzi zatoka,
Nguo nazo matambara, zimechanwa na vichaka,
Ni hoi kama fukara, hakika mi nimechoka,
Lima hili nikwealo, kilele lini tafika?
Yameniishia maji, koo limenikauka,
Wenzi niliotaraji, wote wamenitoroka,
Hapiti hata mwindaji, mkono akanishika,
Lima hili nikwealo, kilele lini tafika.
Sauti yangu napaza, ni mwangwi tu nasikia,
Viumbe wamenyamaza, hakuna wa kuitika,
Nazidi kujihimiza, kwamba mwisho nitafika,
Lima hili nikwealo, kilele lini tafika?
Hadi nifike tamati, ndipo nitapumzika,
Katu tamaa sikati, hata vipi nikichoka,
Nazidi kujizatiti, na hatima nitafika,
Lima hili nikwealo, kilele lini tafika?
66
Buriani
Machozi yamo machoni, uchungu u mtimani,
Mawazo ya akilini, maswali mengi kinywani,
Kwa nini uhayawani, tunauliza kwa nini?
Buriani buriani, tawapeza buriani.
Litoka kwenu nyumbani, mkenda kwishi kambini,
Sio kwamba ni rahani, ni uzalendo nyoyoni,
Tukiwa usingizini, nanyi mu mapambanoni,
Buriani buriani, tawapeza buriani.
Metuacha na huzuni, na kihoro mitimani,
Daima hatuonani, ila kule aherani,
Mlazwe pema peponi, ndugu zetu kwaherini,
Buriani buriani, tawapeza buriani.
Kalamu naweka chini, niandikavyo sioni,
Machozi yalo machoni, yapofusha asilani,
Wandani tangulieni, twawaaga kwaherini,
Buriani buriani, tawapeza buriani.
67
Swagi Ndilo Dude Gani?
Nataka uliza swali, wajuao nijibuni,
Nipate jua ukweli, niridhike mtimani,
Initulie akili, nipate tena amani,
Swagi ndilo dude gani, maanake nelezeni.
Wanavaa suruali, kiuno makalioni,
Twaona zisostahili, zifaacho kuwa ndani,
Wenenda miguu mbali, ni maradhi utadhani,
Swagi ndilo dude gani, maanake nelezeni.
Kitembea hawabali, wajaa barabarani,
Hawaogopi ajali, vidude masikioni,
Yule asiyewajali, atawagonga yakini,
Swagi ndilo dude gani, maanake nelezeni,
Ni swagi ya dijitali, ukiuliza kiini,
Wacheke wakukejeli, papo hapo hadharani,
Eti u wa kule mbali, enzi za analogini,
Swagi ndilo dude gani, maanake nelezeni.
Hilo ndilo langu swali, nawasihi nijibuni,
Hawa wanadigitali, siwaelewi jamani,
Msinione jahili, mjuao nifaeni,
Swagi ndilo dude gani, maanake nelezeni.
68
Leo Huathiri Kesho
Mwenzangu tega sikio, nikuusie mwandani,
Nikupe ya mwelekeo, yakufae maishani,
Sije ukawa chambuo, la rika na majirani,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni,
Maisha mpangilio, vipago hadi peoni,
Kila kipago tukio, tofauti na mbeleni,
Sivipande mbiombio, utajikwaa doleni,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni.
Kwa mmoja mkupuo, tajipata taabani,
Fanya lako azimio, liwe kwako ni ramani,
Tazama kikanyangio, kiwa wazi lako mboni,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni.
Fanya pia dhamirio, likugande akilini,
Likupe matarajio, kuhusu ya upeoni,
Kweli nayo matokeo, ni raha iso kifani,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni.
Usiwatazame hao, walo kule upeoni,
Ukajawa tamanio, ukasahau ramani,
Sifuate mkatio, ukajuta hatimani,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni.
69
Huzijui njia zao, ndipo ukawatamani,
Kumbuka wengine wao, mepita za vichakani,
Chungua kuhusu wao, ubaki wazi kinywani,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni.
Naweka hapa kituo, japo mengi akilini,
Ni langu tumainio, umetia maanani,
Furaha yangu mwenzio, nikuufaa mwandani,
Maisha yako ya leo, huathiri ya keshoni.
Shetani au Malezi?
Naandika nasonona, raha sina mtimani,
Mwenzenu nasinasina, nimejawa na huzuni,
Nacho kisa na maana, ni wanafunzi shuleni,
Shetani kawaingia, ama malezi ndo duni?
Afya wazoroteana, mihadarati milini,
Akili nazo hawana, wamepoteza razini,
Daima ukiwaona, utajawa na imani,
Shetani kawaingia, ama malezi ndo duni?
Wenyewe wanaziona, athari zilivyo duni,
Hakunacho cha maana, humo mihadaratini,
Dhubutu nao kunena, nta zimo masikioni,
Shetani kawaingia, ama malezi ndo duni?
70
Nini mbaya na vijana, watamsikiza nani?
Ni kama wanashindana, ili watuzwe nishani,
Ole wao kwa maana, hatima ni majutoni,
Shetani kawaingia, ama malezi ndo duni?
Matokeo twayaona,kwani yako hadharani,
Akili zimejazana,matendo ya kishetani,
Wanagoma hawa wana,na kuyachoma mabweni,
Shetani kawaingia,ama malezi ndo duni?
Natamani Kale
Nikumbukapo ya zama, kihoro hunizidia,
Maisha yaliwa mema, sikujali ya dunia,
Maelekezo ya mama, ndiyo nilitegemea,
Natamani zile zama, laiti zingerudia.
Hapakuwa uhasama, baina ya familia,
Kwa usafi wa mitima, mengi tulifurahia,
Tuloneana huruma, undugu ukakolea,
Natamani zama zile, laiti zingerudia.
Suala la usalama, katu halikushtua,
Ufisadi usokoma, yakini sikuujua,
Akili yangu daima, iliwa imetulia,
Natamani zile zama, laiti zingerudia.
71
Hakukuwa kutazama, runinga saa kadhaa,
Kwa raha tulichutama, babu tukizungukia,
Mengi kwake tulisoma, yakaishi kutufaa,
Natamani zile zama, laiti zingerudia.
Vijana wenye heshima, kote kote walijaa,
Maadili walisoma, akilini kuyatia,
Wakuu waliposema, yote walizingatia,
Natamani zile zama, laiti zingerudia.
Wanafunzi walisoma, zikaridhisha tabia,
Akiili zao waama, mazuri ziliwazia,
Wazo la kuchomachoma, katu halingewajia,
Natamani zile zama, laiti zingerudia.
Tumeacha Uafrika
Baba hata naye mama, kazini wabidiika,
Hawana muda kusoma, wana wakibadilika,
Mambo yakenda mrama, wanaanza kuhangaika,
Tumeacha uafrika, mizungu yatuandama.
Twajidai tumesoma, na eti tumechanuka,
Na hivyo basi waama, tukaacha uafrika,
Kisha twaanza lalama, wanetu wamepotoka,
Tumeacha uafrika, mizungu yatuandama.
72
Vya asili tumehama, si mavazi si kupika,
Madhara yatuandama, bado hatujazinduka,
Twajitetea twasema, eti tunadijitika,
Tumeacha uafrika, mizungu yatuandama.
Ngozi yetu ile wima, imekwisha haribika,
Mafuta yetu ya zama, yameshasahaulika,
Tujipakayo yachoma, kisha ngozi zachujuka,
Tumeacha uafrika, mizungu yatuandama.
Ng’ano zetu zilikoma, zilizofaa mwafrika,
Zilimfunza heshima, mwana wa kiafrika,
Filamu ndo watazama, chwa hadi kupambazuka,
Tumeacha uafrika, mizungu yatufuata.
Babu Zishike Adabu
E babu mwenye upara, iwapi yako busara?
Hunipishi barabara, eti wataka nidara,
Huoni umeparara, na keya zako zagwara?
Nakwambia ewe babu, zishike zako adabu.
Wa jogoo wako mwendo, lanikera lako tendo,
Mbona usipite kando, kwa ule kule mkondo,
Wanuka hata uvundo, ni kama la taka rundo,
Nakwambia ewe babu, zishike zako adabu.
73
Huoni ulivyokonga, wachechema ja kinyonga,
Hata unapokanyaga, miguu wajikanyaga,
Umewahi ona kanga,ala wake kifaranga,
Nakwambia ewe babu,zishike zako adabu.
Mvi kichwa zimetanda, na ya kitoto watenda,
Ni lini itakuganda, miakayo imeenda?
Hupaswi kuwa wawinda, ya juzi juzi makinda,
Nakwambia ewe babu, zishike zako adabu.
Simile mie nipite, kamwe usinifuate,
Rika lako wafuate, upendavyo wafumbate,
Bure wadondokwa ute, kwangu hupati chochote,
Nakwambia ewe babu, zishike zako adabu.
Shika Nasaha Mwanangu
Mwanangu mwana wa mbee, jongea kwangu karibu,
Keti nikuelezee, nikuepushe aibu,
Sikubali upotee, huku nafyata ja bubu,
Nasaha si ya wazee, bali aliye karibu.
Unaouimba wimbo, mwana hauna mahadhi,
Wauimba kombo kombo, na hisia unaudhi,
Unaudhani ni chambo, kumbe haunayo hadhi,
Subiri na si kitambo, ndipo wimbe wa kuridhi.
74
Usione wasakata, udhani waimba vyema,
Usidhani kawanata, kwa midundiko ya ngoma,
Hakuna utayepata, koo likianza uma,
Raha wakishaipata, ngomayo tatia koma.
Mwanangu andaa vyema, usijitie papara,
Ulingoni kisimama, uimbe bila kukera,
Uvutie nchi nzima, toka pwani hadi bara,
Sifa zitakuandama, upae kama kipura.
Fumbo ni la muwerevu, hilo mwana walijua,
Nawe ulivyo shupavu, shaka sijakutilia,
Nimekuong’oa utovu, mtima nimeridhika,
Nenda penye utulivu, haya upate wazia.
Mama Niwie Radhi
Kosa huwa sio kosa, ila kurudia kosa,
Kuchao uliniwasa, mienendo kutakasa,
Nimejipiga msasa, nikajua nimekosa,
Mamangu niwie radhi, sikunuwia kuudhi.
Zilinipanda hasira, nikapoteza fikira,
Nikahisi nimefura, mfuro kama wa chura,
Nikaona la busara, nitende liso imara,
Mamangu niwie radhi, sikunuwia kuudhi.
75
Mamangu sikuchokoza, na sijawahi chokoza,
Mama sije nigombeza, yote nijapo kweleza,
Nilijaribu jikaza, hasira zikaniweza,
Mamangu niwie radhi, sikunuwia kuudhi.
Tuzikeni Ukabila
Masikio yategeni, kwa makini sikizeni,
Macho nayo fumbueni, ukweli wote oneni,
Vinywa vyenu fungueni, ya amani tuneneni,
Ukabila tuzikeni, kwa amani tuishini.
Twajuzwa chetu kiini, kwenye vikao vya dini,
Bibilia na kurani, tufungue tusomeni,
Toka bara hadi pwani, tu wamija tujueni,
Ukabila tuzikeni, kwa amani tuishini.
Damu yetu mishipani, inayo mija launi,
Mimi nawe mwafulani, hatutofautiani,
Chuki basi ni ya nini, yabidi tupendani,
Ukabila tuzikeni, kwa amani tuishini.
Ndugu zetu siasani, maneno yadhibitini,
Yenye busara neneni, pasiwe purukushani,
Siasa zozote duni, marufuku zipigeni,
Ukabila tuzikeni, kwa amani tuishini.
76
Kwenye yetu masikani, na tusibaguaneni,
Mazuri tutendaneni, daima tufurahini,
Kama ndugu tukaeni, kwa vyote tufaaneni,
Ukabila tuzikeni, kwa amani tuishini.
Hapa ndipo kikomoni, kalamu naweka chini,
Ndugu zangu sikieni, maneno yangu shikeni,
Amani tudumisheni, ndipo Kenya tujengeni,
Ukabila tuzikeni, kwa amani tuishini.
Mbele Ku Shwari
Naangaza kule mbali, mbali kule niendako,
Nionacho ni miali, miali ya pambazuko,
Yavutia kweli kweli, yazidisha tamaniko,
Mbele kunayo mazuri, Mola nikinge na shari.
Naona vimulimuli, vyavutia kwa miwako,
Rangi zake mbalimbali, zang’aa huku na huko,
Akili yangu i tuli, sina kamwe fadhaiko,
Mbele kunayo mazuri, Mola nikinge na shari.
Ni shwari kabisa hali, haina msukosuko,
Upepo wenye utuli, wanijaza tuliziko,
Najihisi ni kabili, siogopi niendako,
Mbele kunayo mazuri, Mola nikinge na shari.
77
Pendo Lako Mama
Natanguliza salamu, zipokee wangu mama,
Nashika hii kalamu, nandike bila kukoma,
Kwa maneno yaso gumu, ili uweze kusoma,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
Miezi tisa ulitimu, kizigo tumboni mama,
Kama mgonjwa wa pumu, kwa uzito ulihema,
Miguu kama vibomu, ulogofya kutazama,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
Siku ya uchungu tamu, uliumwa sana mama,
Ulingoja yako zamu, huku meno wayauma,
Kwako lile la muhimu, mwanao nije salama,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
Ulezi si wa msimu, ulijua hilo mama,
Penzi ulinikirimu, kunitunza hukupima,
Kwa vyovyote linikimu, bila kwesabu gharama,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
Kwangu ukawa mwalimu, na cha busara kisima,
Baya ukalishtumu, ukanijaza hekima,
Uliyonipa elimu, ndo yanipa dira mama,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
Kwangu wewe ni nujumu, kutoka kwake Karima,
Sijui kipi muhimu, nitachokulipa mama,
Hulipiki darahimu, ila nikwombee mama,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
78
Ningeandika dawamu, hadi maktaba nzima,
Lakini nayo kalamu, kuandika inakwama,
Ombi langu kwa Rahimu, akupe maisha mema,
Pendo lako kwangu mama, ni kito kilo adhimu.
Siku Mpya
Nakwita wangu azizi, niitike nakusihi,
Toka kwenye usingizi, imefika asubuhi,
Futa ya jana na juzi, yote yasiyo sahihi,
Mwandani futa machozi, siku mpya yaingia.
Siku mpya yaingia, ona jua lachomoza,
Kiza limeshaondoa, ona kunavyopendeza,
Miale isiyo doa, ona inavyoangaza,
Mwandani wangu tulia, siku mpya imekucha.
Siku mpya imekucha, jikaze wangu mwandani,
Mungu unayemcha, akujua nje na ndani,
Fahamu hajakuacha, usiyumbe kiimani,
Mwandani macho fikicha, ona leo sio jana.
Ona leo sio jana, leo siku tofauti,
Nakwomba jaribu tena, bila katu atiati,
Usife moyo ng’ang’ana, leo ndo yako bahati,
Ya juzi hata ya jana, yasikufanye mfungwa.
79
Ombi Langu
Nijapo kuwa mjinga, akili ni punguani,
Nisemayo nabananga, mwenyewe siyabaini,
Binadamu wanipinga, niyatoapo maoni,
Mola nawe nitalonga, kwako mie ni razini.
Nijapo kuwa mnyonge, siha sina mwilini,
Ulojalia ubonge, wanione mie duni,
Marafiki wanitenge, upweke uwe moyoni,
Mola wangu sinitenge, iwa mwenza na jirani.
Nijapo kuwa mkata, chochote sina sinani,
Kote kote nikipita, wanitia midomoni,
Omba omba waniita, waninyime na amani,
Sitake nikaokota, Mola wangu vya pipani.
Chuki Siipi Nafasi
Chuki nichukie mwenzi, nami pendo nikupende,
Amri ya Mwenye enzi, hata adui tupende,
Moyo siufishi ganzi, nauruhusu upende,
Chuki siipi nafasi, pake pote nimeziba.
Hata uweke viunzi, nitakwea ja mjusi,
Tenda yote ya kishenzi, sitanuna sitatusi,
Kwa chuki mi mwanagenzi, kuijua si mwepesi,
Chuki siipi nafasi, pake pote nimeziba.
80
Nisukumie majonzi, raha nitang’ang’ania,
Uso sitii kunyanzi, tabasamu napambia,
Undugu ninauenzi, na nitakuvumilia,
Chuki siipi nafasi, pake pote nimeziba.
Nani?
Nambie kama wajua, apendaye bovu nani?
Nambie nipate jua, hilo leo nibaini,
Nambie nitatulia.
Neleze ‘onaye raha, akanyangapo kinyesi,
Neleze kama si juha, aliyepoteza hisi,
Neleze bila kuhaha.
Nisimulie bayana, mwenye kupenda tambara,
Nisimulie sitakana, nitaijenga taswira,
Nisimulie kwa kina.
Nonyeshe atamaniye, kula kiporo cha jana,
Nonyeshe nijue yeye, kama raha aiona,
Nonyeshe usikimiye.
81
Polepole Mwanangu
Polepole ndio mwendo, ndivyo walinena kale,
Walinena kwa vitendo, ili tuyafuatile,
Mwanangu fata mkondo, achacho kimbelembele.
Vipi umeweka kando, ya wa zamani wavyele?
Ukaiiga mitindo, ya kina fulani wale,
Mitindo yenye uvundo, na yenye hasara tele.
Wenda wafata mdundo, mdundo wa zao lele,
Mwacheza hata na chando, bila kujali kelele,
Hatimaye ni kishindo, lele ifike kilele.
Mwanangu wala uhondo, bila kuangaza mbele,
Kisha uje na rundo, la zisotajika ndwele,
Itakupotea kondo, usalie tu na ole!
Wenenda penye utando, badala ya ukwepele,
Mwenye wajigonga nyundo, nitakwambiaje pole?
Rekebisha zako nyendo, mui ha’mbiwi kongole.
82
83