Bendera Bandia
na Hadithi Nyingine
Pauline Kea
Gredi 4
Bendera Bandia na Hadithi Nyingine
Kimechapishwa 2021 na Queenex Publishers Limited
S.L.P 56049-00200, Nairobi, Kenya.
Simu: 0727 794 498, 0715 808 200
Baruapepe: info@queenexpublishers.co.ke
queenexbooks@gmail.com
Tovuti: www.queenexpublishers.co.ke
© Pauline Kea, 2021
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili,
kupigisha chapa, kutafsiri au kutoa kitabu hiki kwa
jinsi yoyote ile bila idhini kwa maandishi ya Queenex
Publishers Limited.
ISBN: 978-9966-141-38-5
Chapa hii 2023
iii
Yaliyomo
1. Yaliyomo ..................................................................... iii
2. Tikitimaji la Ajabu ......................................................... 1
3. Bendera Bandia .......................................................... 16
4. Kisa cha Fisi Msaliti ..................................................... 29
5. Sala ya Salome na Sami .............................................. 46
1
Tikitimaji la Ajabu
2
Kobe na Sungura walikuwa marafiki wa chanda na pete.
Waliishi pamoja na kufanya mambo mengi pamoja. Kila
siku walienda mwituni kutafuta matunda, uyoga na majani
ya mimea ya aina aina. Walipofika nyumbani, waliyaosha
matunda na kuyala. Walipika uyoga na majani ya mimea na
kula. Maisha yao yalikuwa shwari hadi ukame ulipowavamia.
Mito ilikauka, misitu ilikosa matunda na majani ya mimea
yakakauka pia. Uyoga nao haukuota kamwe. Kobe na
Sungura walitaabika sana. Walikosa riziki ya kutia tumboni.
Walikonda na kukondeana kama ng’onda.
“Lazima tutafute mbinu za kukabiliana na ukame huu wa
mara kwa mara. La sivyo, tutaangamia,” Kobe alimwambia
rafiki yake.
Tufanyeje mwenzangu?” Sungura alimuuliza Kobe kwa
unyonge.
“Ninaona tuanzishe kilimo. Bora zaidi kilimo biashara.
Tupande matunda na mimea tofauti ya mboga. Tukivuna,
tutakula na mazao mengine tuyahifadhi kwa kuyakausha.
Wakati wa kiangazi tutakula mazao tuliyohifadhi. Mazao
yakiwa mengi sana tutayauza,” Kobe alimwelezea Sungura.
“Hilo ni wazo zuri sana, lakini tutalimaje bila mvua?” Sungura
aliuliza.
Tutamwomba Bwana Ndovu atuchimbie kisima cha kina
kirefu. Tutatumia maji ya kisima kunyunyizia mimea yetu
hadi mvua itakaponyesha,” Kobe alimjibu Sungura.
“Ninaona mawingu yametanda. Hata labda mvua iko karibu
kunyesha,” Sungura alisema.
3
“Iwapo kutanyesha, tutachimba bwawa kubwa la maji.
Ukame ukivamia tena tutatumia maji ya bwawa kunyunyizia
mimea yetu. Penye nia pana njia. Tutaweza, bora tuanze
tu,” Kobe alieleza.
“Hilo litakuwa wazo zuri, lakini mimi na kilimo ni kama
maji na mafuta. Hatupatani. Wewe anza mradi wako mimi
nitakutia moyo tu!” Sungura alisema na kuondoka.
Kobe alianza mradi wake wa kilimo biashara. Mwanzoni
ilikuwa kazi ngumu ya kulima na kuondoa magugu. Kisha
akatayarisha mbegu zake na kuzipanda kwenye mifuko
aliyotengeneza kwa magamba ya migomba. Baada ya
wiki chache mbegu zilichipuka na miche ikaanza kunawiri.
Kobe alinyunyizia miche yake maji kutoka kwenye kisima
alichochimbiwa na Ndovu.
Kobe alikuwa na bahati kama mtende. Miche yake ilipokomaa
na kufikia wakati wa kupandwa, mvua ilianza kunyesha.
Kobe alifurahi fika. Sungura alipopitia shambani alimwita
kwa furaha, “Njoo unisaidie rafiki yangu. Wakati wa kupanda
umewadia. Jitihada huvuta heri. Tukitia bidii tutavuna vizuri.”
“Nina shughuli nyingi sana kwa sasa. Wewe panda,
nitakusaidia kuvuna,” Sungura alimjibu Kobe na kupita
haraka.
Kobe hakufa moyo. Alijifunga kibwebwe na kuanza kazi ya
upanzi. Alipanda miche ya matunda kama vile ya michungwa,
minanasi, milimau, mitikitimaji na mimea ya mboga kama
vile karoti na vitunguu. Mimea yote ilikua na kunawiri vizuri.
Kazi ya kupalilia mimea yake ilipoanza, Kobe alimwomba
tena rafiki Sungura msaada.
4
5
“Ndugu yangu, ninakuomba unisaidie kuondoa kwekwe
shambani. Kazi imekuwa nyingi. Ninahofia kuwa siwezi peke
yangu,” Kobe alimwomba Sungura.
“Mimi ninaumwa. Siwezi kazi. Samahani sana,” Sungura
alimjibu Kobe na kutoweka.
Kobe alijipa moyo na kuendelea kuondoa magugu na kwekwe
shambani. Hatimaye baadhi ya miche yake ilianza kuchanua
na baadaye matunda yalianza kukomaa. Sungura alipitia
mara kwa mara shambani kwa Kobe kuangalia kama kuna
chakula chochote kilichokuwa tayari.
Siku moja, Kobe alifika shambani mapema. Alikuta karoti
zake zilikuwa zimeng’olewa. Mashina ya karoti yalikuwa
yametapakaa kando ya ua wa shamba lake. Hakujua
afanyeje. Hakuamini kuwa baada ya bidii yake ya mchwa
kuna mnyama ambaye angefikiria kumdhulumu.
“Hodi huku shambani,” Sungura alisema kwa sauti. Kobe
akashtuka alipomsikia Sungura.
Tangu lini ukapiga hodi ukiingia shambani?” Kobe alimuuliza
Sungura.
“Nimeona ni vizuri kuomba ruhusa ya kuingia shambani
mwako,” Sungura alisema huku akichekacheka.
“Karibu shambani basi,” Kobe alisema kwa upole.
“Ninaona wakati wa kuvuna umewadia,” Sungura alisema
kwa mshawasha.
“Umejuaje kuwa wakati wa kuvuna umefika?” Kobe alimuuliza
Sungura.
6
Sungura alicheka tu na hakumjibu. Kobe alianza kushuku
kuwa Sungura ndiye aliyekuwa ameng’oa karoti zake.
Kobe aligundua kuwa mazao shambani mwake yalikuwa
yakipungua kila uchao. Alijua kuwa lazima kulikuwa na
mwizi aliyekuwa akiyavuna kisirisiri. Ijapokuwa alimdhania
Sungura sana, hakuwa na ushahidi. Kobe alimpigia Mfalme
Simba simu ili amshtaki mwizi.
Tafuta mbinu za kumtambua mwizi. Tukimjua, askari wangu
watamtia mbaroni. Haiwezekani baadhi ya wanyama
waruhusiwe kuwanyanyasa wengine. Lazima tufanye haki,”
Simba alisema kwa simu.
Kobe alitengeneza mitego kadha wa kadha ili amkamate
mwizi. Alianza na shimo kubwa. Alichimba pale alipoona
alama za nyayo za aliyeshukiwa kuwa mwizi.
“Ninafikiria anapitia hapa. Akikanyaga majani haya ya ndizi
atatumbukia ndani,” Kobe alijisemea huku akiweka mtego.
Mtego wake haukushika kitu. Alitengeneza pia mtego wa
kengele. Alifunga uzi mwembamba kwenye kengele pale
ambapo mshukiwa wake alipitia. Usiku wa manane ulipofika,
alisikia kengele ikilia. Kobe alitoka mbio awezavyo, lakini
mwendo wake wa polepole ukamchongea. Alipofika, mwizi
tayari alikuwa ametoroka. Japo siku hiyo hakuna kilichoibwa,
mwizi hakukoma kurudi shambani.
Kobe aliweka mtego wa panya shambani mwake kisha
akaufungia kwa kamba mtini. Sungura alijua bila shaka kuwa
Kobe alikuwa anaweka mtego. Tatizo ni kuwa hangejua
mtego wenyewe ulikuwa wapi na ulikuwa wa aina gani.
7
Sungura alipofika shambani kwa Kobe, alimwona Nyani
akiruka mtini. Alimwita, “Rafiki yangu Nyani, njoo
nikuonyeshe kitu kitamu ule.”
“Shamba hilo ni la Kobe. Mimi sitaki kuvunja sheria. Ni hatia
kula vitu vya wengine bila idhini yao,” Nyani alimwambia
Sungura.
“Ruhusa ninayo. Wewe njoo tu,” Sungura alimdanganya
Nyani. Nyani alikubali na kujongea shambani.
Tuingie hapa shambani tung’oe karoti tule. Tangulia wewe,
mimi ninakufuata,” Sungura alisema.
Nyani aliingia shambani bila tahadhari. Mara mtego wa
panya uliokuwa umefukiwa mchangani ulimnasa mguuni.
Nyani alilia kwa woga na uchungu.
Sungura alicheka kwa sauti na kusema, Wajinga ndio
waliwao.”
Kisha aling’oa karoti na kula. Halafu alichagua tikitimaji
moja kubwa akalitunda na kulibeba. Nyani alibaki hapo
akilia na kulaani. Alijaribu kutoroka lakini mtego wa panya
ulikuwa umefungiwa mtini kwa kamba nyembamba ngumu.
Alirukaruka ili kujinasua. Kwa bahati mbaya alitumbukia
ndani ya lile shimo la mtego.
Kobe alipofika shambani alifurahi ghaya. Alijua kuwa alikuwa
amempata mwizi ambaye alikuwa amemhangaisha siku
nyingi.
“Ninaomba radhi ndugu Kobe. Mimi si mwizi wa karoti na
tikitimaji lako. Mwizi ni Sungura. Amenihadaa tu,” Nyani
alimweleza Kobe huku akilia na kusaga meno.
8
Kobe alitia na kutoa. Alizunguka shambani. Aliona karoti
zilikuwa zimeliwa na tikitimaji kutundwa. Alichunguza alama
za nyayo zilizokuwa shambani. Alithibitisha kweli zilikuwa
za Sungura.
9
“Ni kweli unayosema. Haiwezekani kuwa ulikula karoti na
kutunda tikitimaji ukiwa mtegoni, lakini kuwa mwangalifu
ili usidanganywe siku nyingine,” Kobe alisema huku akimtoa
Nyani mtegoni.
Nyani alimshukuru Kobe kwa kumtoa kwenye mtego huo.
Alimuahidi kuwa asingerudia kosa kama hilo tena. Nyani
alitoka hapo akichechemea na kwenda moja kwa moja hadi
kwa Simba. Alimshtaki Sungura kwa mfalme. Simba aliahidi
kumchukulia Sungura hatua.
Maarifa ya Kobe ya kutengeneza mitego yalikuwa yamefika
mwisho sasa. Kobe alianza kuwaza na kuwazua. Alijikuna
kichwa ili apate wazo la mtego mmoja zaidi tu. Alitamani
kutengeneza mtego ambao ungemnasa Sungura na asiweze
kuponyoka. Kobe aliangalia matikitimaji yake yalivyonawiri
na kukomaa. Alionekana mwenye furaha.
“Kama Sungura asingekuwa ananisumbua sasa ningekuwa
nimeanza kupeleka matikitimaji yangu sokoni. Ningepata
pesa nyingi. Ningenunua mbegu na mbolea ili nipanue kilimo
biashara changu,” Kobe alijisemea. Hapo hapo wazo lilimjia
Kobe.
“Nitatengeneza mtego wa tikitimaji. Litakuwa tikitimaji la
ajabu. Litakuwa kubwa kuliko kawaida na litametameta.
Bila shaka litamvutia Sungura kuliko mengine yote.”
Kobe alitunda tikitimaji moja kubwa. Alilitoboa na kulitoa
kila kitu ndani akala. Aliposhiba, alienda kwenye mti wa
gundi na kuchukua gundi ya kutosha. Alilipaka tikitimaji hilo
gundi kwa uangalifu mkubwa. Kisha Kobe aliingia ndani ya
tikitimaji hilo na kutulia kama maji mtungini.
10
Sungura aliingia shambani kwa Kobe akiimba. Aliangalia
huku na kule na kuendelea kuimba.
Naingia shambani, naingia, naingia,
Naingia kwa madaha, naingia naingia,
Naingia kwa kishindo, naingia, naingia.
Alipoliona lile kimaji kubwa alishtuka.
“Lo! Hili nalo ni kubwa. Tena linang’ara kama jua. Leo ni
leo asemaye kesho ni mwongo. Litanitambua. Nitalila lote,”
Sungura alijisemea kwa sauti.
Kobe mle ndani ya tikitimaji lile alicheka kimoyomoyo. Alijua
kuwa mtego wake ulikuwa umemvutia mwizi.
Sungura alilisogelea lile tikitimaji na kuligusa. Mkono wake
ulinaswa.
“Usinishike tikitimaji wewe! Nitakutunda sasa hivi,” Sungura
alisema huku akishika tikitimaji kwa mkono wake wa pili.
Mkono wa pili nao pia ulinaswa. Sungura alishtuka.
“Pole basi. Kama hutaki kuliwa leo, acha nile lile tikitimaji
jingine pale. Niache tu,” Sungura alizungumza na tikitimaji
hilo akiwa ameshikwa mikono yote miwili. Sungura aliendelea
kulizungumzia tikitimaji hilo la ajabu. Tikitimaji nalo
liliendelea kunyamaza tu.
“Ewe tikitimaji niache nisikupige teke,” Sungura alisema
huku akirusha teke. Mguu wake ulinaswa na gundi pia.
Sungura aliendelea kusema na tikitimaji huku akilipiga teke
kwa mguu wa pili. Miguu yote ilishikwa. Alibaki amenaswa
juu ya tikitimaji. Kisha tikitimaji lilianza kusonga polepole.
11
“Ewe tikitimaji la ajabu. Unaenda wapi? Nishukishe basi.
Mimi sitaki ugomvi. Niache niende zangu. Sikutaki tena,”
Sungura alisema kwa wasiwasi mkubwa.
12
Kobe alipoona kuwa amemnasa Sungura alimpigia Mfalme
Simba simu. Alimweleza yote yaliyojiri. Mfalme Simba
alifurahishwa sana na bidii, hekima na ubunifu wa Kobe.
“Pongezi Kobe kwa kuitumia akili yako vilivyo kumnasa
Sungura. Tafadhali mlete mbele ya baraza la wanyama ili
tuamue kesi yake,” Mfalme Simba alijibu simu ya Kobe.
Kobe alitembea asteaste kuelekea kwa Mfalme Simba. Njiani,
Sungura alilalama na kulia kama mtoto. Alimwomba Kobe
msamaha na kumkumbusha kuwa walikuwa marafiki wa
dhati.
Tamaa yako imekusaliti Sungura. Kama ungekuwa rafiki
wa kweli usingeniibia. Badala yake, ungenisaidia kufanya
kazi shambani,” Kobe alisema.
Walipofika kwa Mfalme Simba, tayari baraza la wanyama
lilikuwa likiwangojea. Sungura alitolewa kwenye tikitimaji la
ajabu na Nyani. Kesi ikaanza mara moja. Sungura alishtakiwa
kwa makosa mawili. Kosa la kwanza lilikuwa ni wizi shambani
mwa Kobe. Kisha, kosa la pili lilikuwa la kumdanganya Nyani
na kumtia mtegoni.
Mara tu Sungura alipobanduliwa kwenye tikitimaji la ajabu,
alipiga magoti mbele ya baraza la wanyama na kuomba
msamaha.
Baraza la wanyama lilimwamulia Sungura kesi. Alipewa
adhabu ya kumlimia na kumpandia Kobe shamba lake lote.
Sungura alimwomba Nyani msamaha. Nyani alimsamehe.
Baada ya kesi hiyo ya Sungura, Kobe alirudi shambani mwake
na kutunda matikitimaji yake apeleke sokoni. Nyani alijitolea
kumsaidia kutunda, naye Ndovu alimsaidia kubeba. Kobe
aliwashukuru kwa hisani waliyomtendea.
13
14
Kamusi Yangu
alitia na kutoa aliwaza sana
amenihadaa amenidanganya
asteaste kutembea polepole
dhati moyo wa kweli
ghaya sana
idhini ruhusa
kilimo biashara kulima ili kuyauza mazao na kupata pesa
kuchanua kutokeza kwa maua ya mmea
kujongea kwenda polepole karibu na kitu kingine
kukabiliana kupambana
kumdhulumu kumfanyia mabaya
kutoweka kwenda na kukosa kuonekana
kwekwe mmea wowote ambao umeota mahali
hautakiwi
magugu mimea isiyohitajika shambani
miche mimea michanga
mshawasha kiu ya kujua au kufanya jambo
shwari hali kuwa nzuri
tahadhari kuwa mwangalifu
ugomvi hali ya kutoelewana
ukamchongea ukamwingiza matatani
umefukiwa umefichwa ardhini
yaliyojiri yaliyotokea
15
Maswali
1. Je, Kobe alitoa wapi maji ya kunyunyizia miche yake?
2. Mtu anaweza kuhifadhi vipi maji ya mvua?
3. Taja mimea yote ambayo Kobe alipanda.
4. Ni nini maana ya ‘alikuwa na bahati kama ya mtende’?
5. Sungura alitoa sababu gani za kukosa kumsaidia Kobe?
6. Kwa nini Kobe alishuku kuwa Sungura alikuwa mwizi?
7. Taja mitego yote aliyoitengeneza Kobe.
8. Nyani alijitetea vipi aliposhikwa mtegoni?
9. Je, unafikiri kuwa adhabu ambayo Sungura alipewa ilifaa?
10. Umejifunza nini kutokana na hadithi hii?
Mazoezi
1. Ukiwa na rafiki yako:
a. Tajeni nahau zote za maadili zilizo kwenye hadithi.
b. Toeni maana ya nahau hizo za maadili.
c. Elezeni maana ya methali zilizotumika katika hadithi
hii.
2. Msomee rafiki yako ukurasa mmoja wa hadithi hii.
Mwambie akuhesabie maneno unayoweza kusoma kwa
dakika moja. Linganisha kasi yako ya usomaji na ya
mwenzako mkiwa darasani.
3. Andika insha ya maelezo kuhusu:
Jinsi ya kutunza miche
16
Bendera Bandia
17
Kengele ilipolia, wanafunzi wote walikimbia kwenye
gwaride. Sofia, Helena, Mambo na Lemayan tayari walikuwa
washafika. Walitangulia ili kuitayarisha bendera. Wakati wa
kupandisha bendera ulipowadia, kikosi hiki cha wanaskauti
kilisimama mbele ya mlingoti. Sofia ndiye aliyeibeba bendera.
Mambo, Helena na Lemayan walisimama tisti nyuma yake.
“Eeh Mungu nguvu yetu,” Lemayan alianzisha wimbo wa
taifa kwa sauti. Wanafunzi wote walimwitikia Lemayan
kwa sauti.
“Ilete baraka kwetu…”
Waliimba wimbo wa taifa huku Mambo akiipandisha bendera.
Kisha, mwalimu aliyeshika zamu alitangaza kwa sauti,
Wanaskauti wetu watatuimbia wimbo wa kuisifu bendera
yetu. Sikilizeni kwa makini ili muimbe nao tena baada ya
wao kumaliza.”
Sofia, Helena, Mambo, na Lemayan waliimba wimbo wa
kuisifu bendera kwa sauti.
Bendera yetu ya Kenya yapendeza,
Bendera yetu ina rangi nzuri,
Nyeupe, nyeusi, nyekundu, kijani,
Hizo ndizo rangi za bendera yetu.
Rangi nyeupe yatangaza amani,
Rangi nyeusi ni ya ngozi zetu,
Rangi nyekundu ni damu ya ukombozi,
Rangi ya kijani ni mashamba yetu.
Wanafunzi wote waliimba wimbo huu pamoja na kikosi hicho
cha wanaskauti. Watu walipofumukana ili kwenda darasani,
baadhi ya wanafunzi waliendelea kuimba wimbo huo kwa
sauti za chini. Wengine waliuimba vizuri na wengine vibaya.
18
Wataushika tu,” Helena alimwambia Mambo, huku
akitabasamu.
“Bila shaka wataujua. Ni wimbo mzuri sana,” Mambo alisema.
* * *
Wanaskauti hao walielekea moja kwa moja hadi kwenye
ofisi ya mwalimu wa skauti wakiwa na bendera mkononi.
Kumbe bendera ilikuwa imemwagikiwa na rangi. Baada
ya kuipandisha, ndipo wanaskauti walipoiona rangi hiyo.
Walipoingia ofisini Lemayan ndiye aliyeiweka bendera juu
ya meza. Mwalimu hakuwepo. Pengine alikuwa kwenye
ofisi kuu.
“Lo! Tutafanyaje kuondoa rangi hii kwenye bendera yetu?”
Lemayan aliuliza kwa hofu.
Tutaipangusa tu,” Helena alisema huku akimsaidia Lemayan
kuiondoa rangi kwenye bendera hiyo.
Mambo aliwekelea firimbi kwenye meza ya mwalimu, kisha
akamsaidia Helena kuipangusa bendera kwa karatasi ya
shashi iliyokuwa mezani.
“Ni bahati mbaya tu. Ajali haina kinga. Tutaiosha bendera
kabla ya kwenda nyumbani, kisha tuianike. Itakauka wikendi.
Jumatatu tutaipandisha ikiwa safi kabisa,” Sofia alisema.
Jioni baada ya mafunzo ya siku, wanaskauti hao walienda
jikoni na kumwomba mpishi wa shule sabuni kidogo na beseni.
Walichota maji mferejini. Walichanganya sabuni na maji na
kupata povu zuri. Kisha waliiloweka bendera ndani ya maji.
Walisugua bendera kwa zamu. Baada ya dakika thelathini,
wote walikuwa wamechoka. Bendera ilikuwa haitoki rangi.
Yote ilionekana rangi mchanganyiko. Ilitisha kweli.
19
20
Tufanye nini?” Lemayan aliuliza.
“Ninaonelea tumwambie mwalimu wetu wa skauti kabla
hajaenda nyumbani,” Helena alipendekeza.
“Hilo si wazo zuri. Mwalimu atafikiria kuwa hatuwezi
kuwajibika. Ninaonelea tuchange tununue bendera nyingine,”
Mambo alisema.
“Mimi siwezi kupata pesa za kuchanga,” Lemayan alisema.
“Kwa nini tusiwaite wenzetu wikendi, ili watusaidie kuchanga
pesa. Yaani tufanye harambee,” Sofia alipendekeza.
“Hilo ninaona ni wazo zuri sana,” alichangia Mambo.
Wanaskauti hao walitangazia wenzao harambee.
Waliwaomba wazazi na walezi wao simu na kuwajuza
wenzao kuhusu harambee. Waliwaandikia ujumbe mfupi.
Wengi wao hawakuwa na pesa za kutoa.
Wenzetu wanasema hawana pesa. Tutafanyaje?” Lemayan
alimuuliza Sofia.
Tuwaambie walete chochote walicho nacho. Tunaweza
kupeleka vitu watakavyoleta dukani tupewe bendera,” Sofia
alimjibu Lemayan.
* * *
Harambee ilifanyika uwanjani. Watoto wengi walihudhuria.
Wengine walielewa lengo la mkutano wao, lakini wengine
hawakujua walichohitajika kufanya. Harambee ilipoanza
watoto walichanga chochote walichokuwa nacho. Waliimba
wimbo wa harambee huku wakiweka kila walichokileta
pamoja.
21
Toa ndugu, toa dada, ulichonacho wewe,
Kutoa ndugu ni moyo, wala si utajiri.
Watoto walitoa vitu vingi: viazi vitamu, matunda, mayai,
kuku na hata sungura.
22
“Umempata wapi sungura mzuri hivi?” Mambo alimuuliza
mtoto mmoja.
“Nina mradi mdogo wa kuwafuga sungura. Nimewaomba
wazazi wangu kuchukua sungura mmoja wakakubali,” alijibu
mtoto huyo.
“Hata mimi ninataka kufuga sungura. Nakuomba baada
ya harambee hii unieleze jinsi ya kuanzisha mradi kama
wako,” Mambo alisema. Wakati huu wote, Mambo alikuwa
akiyashika manyoya mororo na meupe ya sungura huyo.
Helena alizunguka na kikapu kidogo akikusanya pesa. Baada
ya harambee kuisha, Helena alihesabu pesa walizoweza
kukusanya. Alitangaza kwa sauti. Watoto walipiga makofi
na kushangilia.
Asanteni sana kwa kuhudhuria harambee hii. Tumefanikiwa
kukusanya pesa na vitu vingi. Bila shaka sasa tutaweza
kununua bendera nyingine. Nyote ni marafiki wa dhati,”
Sofia aliwashukuru watoto wenzao.
Wanaskauti waliamua kwenda moja kwa moja hadi dukani
kununua bendera. Walipofika waliuliza bei ya bendera.
Walipoambiwa bei walishtuka sana. Pesa walizokusanya
zisingetosha. Walimpa mwenye duka vitu walivyokusanya
pia.
Mwenye duka alicheka kwa sauti na kusema, “Nampenda
sungura wenu sana. Lakini vitu vya dukani naviuza kwa pesa
taslimu. Samahani sana watoto haiwezekani biashara ya
aina hii hapa. Nawaomba mwende sokoni, muuze bidhaa
zenu, kisha mkipata pesa mje kununua bendera.”
Wanaskauti hao walimaka.
23
Tufanye nini? Hatuwezi kwenda sokoni kuuza bidhaa zetu.
Hatuna muda,” Helena alisema.
“Lazima tufanye jambo haraka, muda wenyewe unayoyoma.
Tufanye nini jamani?” Sofia aliuliza.
Tutengenezeni bendera. Nitawaelekeza,” Lemayan alisema.
Wanaskauti walikubaliana kutengeneza bendera. Walielewana
kutafuta vitu ambavyo wangehitaji haraka bila kupoteza
wakati.
Walipeleka kila kitu kwa akina Sofia. Walikaribishwa vizuri na
kazi ilianza mara moja. Walivipanga vitu vyote walivyohitaji.
Kila mmoja wao alijifunga kibwebwe kufanya awezalo.
Lemayan ndiye aliyewaelekeza. Walichukua vitambaa
vya rangi zote za bendera na kuvipanga vilivyo kisha
wakaviunganisha.
“Mambo ana kipaji cha uchoraji. Badala ya kuchora ngao,
kwa nini asichore ramani ya Kenya? Bendera yetu itakuwa na
upekee wa ajabu. Kila mtu ataipenda,” Lemayan alipendekeza.
“Ninaupenda ubunifu wako Lemayan. Ninakuunga mkono,”
Helena alisema.
Wote walikubaliana kwa kauli moja kuwa Mambo achore
ramani kwenye bendera yao. Alipomaliza, bendera hiyo
ilipendeza ajabu.
Tuipandishe bendera yetu pale mtini ili tuifanyie majaribio,”
Sofia alisema kwa furaha.
Wanaskauti waliipandisha bendera yao mtini huku wakiimba
na kucheka.
24
25
Siku ya Jumatatu ilipofika, Sofia, Mambo, Helena na
Lemayan walirauka shuleni kuliko kawaida. Walitamani
sana kuipandisha bendera waliyoitengeneza. Waliiona ya
kupendeza kuliko bendera za kawaida. Walitaka kujivunia
ubunifu wao.
“Mwalimu wetu wa skauti akiiona atatuonea fahari kubwa,”
Sofia alisema kwa sauti ya chini.
Wimbo wa taifa uliimbwa huku bendera ikipandishwa
taratibu. Mambo aliipandisha bendera polepole sana ili watu
wajionee bendera hiyo yao ya kipekee.
Walimu na wanafunzi wengine waligundua kuwa bendera
ilikuwa si ya kawaida. Walimaka. Wengi wakaonyesha hofu
yao waziwazi. Wanaskauti walishangaa kuona kuwa nyuso
za wengi hazikuonyesha hisia za furaha bali za karaha. Wao
pia waliingiwa na wasiwasi.
“Bendera bandia!” mwanafunzi mmoja alisema kwa sauti.
Baada ya shughuli zote za gwarideni kukamilika, wanaskauti
wote waliitwa ofisini kwa mwalimu mkuu.
Huko waliwapata walimu kadhaa, akiwepo pia mwalimu
wa zamu na mwalimu wao wa skauti.
Walimu hawakulifurahia wazo letu. Tufanyeje?” Lemayan
aliuliza wenzake walipokuwa wakielekea ofisini.
Tuseme ukweli. Tuwaeleze kila kitu,” Helena alijibu.
Walipoingia ofisini kwa mwalimu mkuu, walikaribishwa
kwa maswali.
“Bendera ya wanaskauti iko wapi?” mwalimu wao wa skauti
aliwauliza. Sofia alieleza kila kitu. Walimu wote walicheka
26
hadi wakachoka mbavu.
Tunaomba msamaha. Naona hamkufurahishwa na kitendo
chetu. Tulikuwa tunajaribu kutatua tatizo letu sisi wenyewe,”
Mambo alisema.
“Samahani sana. Tulidhani kuwa tulikuwa tunafanya jambo
la busara,” Helena aliongezea.
“Mwalimu wetu wa darasa alituambia kuwa tunafaa kutafuta
suluhisho ya tatizo lolote tunalokutana nalo sisi wenyewe.
Kama tumekosea, tunaomba msamaha,” Lemayan aliomba.
“Ni vizuri kutatua matatizo yenu wenyewe, lakini ni vizuri
kuomba ushauri wakati mwingine. Bendera ya taifa si
kitambaa tu ambacho kinaweza kushonwa kiholelaholela.
Bendera yetu ya taifa ina hadhi yake ambayo lazima ilindwe.
Bendera ya taifa inastahili kufanana popote pale inapopepea
nchini,” mwalimu wa skauti alifafanua.
“Nimependa ubunifu wenu. Ninapendekeza kuwa mtengeneze
bendera nyingine lakini muichore ngao. Kisha muitundike
bendera hiyo darasani mwenu ili muitumie kama nyenzo ya
kujifunzia rangi za bendera. Tutapanga na mwalimu wenu
wa darasa baadaye,” mwalimu mkuu aliongezea.
Sofia alitaka kujua maana ya ngao kwenye bendera ya taifa.
Mwalimu wake wa darasa alimwelezea, “Ngao ni ishara ya
ulinzi mkali uliowekwa kwenye mipaka yote ya nchi yetu.”
Wanaskauti hao waliwashukuru walimu wao kwa
kuwasamehe. Mwalimu wao wa skauti aliwapa bendera
nyingine mpya. Waliahidi kuilinda na kuitunza bendera hiyo.
Walitayarisha mfuko spesheli wa kuitia kila walipoishukisha
kutoka kwenye mlingoti wake.
27
Kamusi Yangu
gwaride mkusanyiko wa wanafunzi na walimu
hasa wakati wa matangazo na
kupandisha bendera
fahari kuonea fahari ni kujivunia kitu au mtu
hadhi heshima
karaha huzuni
mlingoti mti mrefu unaotumiwa kutundikia bendera
mororo yasiyokuwa magumu; laini
nyenzo vifaa vinavyotumika katika ujifunzaji na
ufunzaji darasani
ramani mchoro unaoonyesha sehemu fulani ya
nchi au nchi nzima
shashi karatasi nyepesi inayotumiwa
kupangusia uchafu. Wakati mwingine
hutumiwa chooni
tisti kusimama bila kutikisika hata kidogo
ubunifu hali ya kuweza kutengeneza kitu kwa
mara ya kwanza kabisa
waliiloweka waliitia ndani ya maji
wakachoka
mbavu wakachoka sana
walipofumukana walipotawanyika
zamu utaratibu wa kufanya jambo kwa
kupokezana
28
Maswali
1. Taja majina ya maskauti kwenye hadithi.
2. Taja maana ya rangi za bendera ya Kenya.
3. Wanaskauti walifanya nini baada ya bendera kupata
rangi?
4. Unafikiri wanaskauti walihitaji vitu gani ili kutengeneza
bendera?
5. Ni nani aliyechora ramani ya Kenya kwenye bendera?
6. Kwa nini walimu na wanafunzi walimaka bendera bandia
ilipopandishwa?
7. Wanaskauti walifanya nini walipoitwa ofisini kwa mwalimu
mkuu?
8. Ni nini maana ya ngao kwenye bendera ya Kenya?
9. Kama ungekuwa mmoja wa wanaskauti ungefanya nini
baada ya bendera kupata rangi?
10. Umejifunza nini kutokana na hadithi hii?
Mazoezi
1. Mwimbie mlezi au mzazi wako:
a. wimbo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki
b. wimbo wa Taifa la Kenya
c. wimbo wa kusifu bendera ya Kenya kwenye hadithi
2. Mwambie mlezi au mzazi wako akurekodi ukiimba nyimbo
za sehemu ya 1 ili ujisikilize na kujitathmini.
3. Zungumza kuhusu umuhimu wa bendera ya taifa ukiwa na
mlezi au mzazi wako. Andika hoja zote kuu kisha umtumie
mwalimu wako wa darasa.
29
Kisa cha Fisi Msaliti
30
Hapo zamani za kale wanyama wote walikula nyasi na
majani. Simba alikuwa mfalme wao. Wanyama wote wa
porini walimheshimu na kumtii. Naye Simba alitawala porini
kwa hekima, heshima na haki. Simba aliunda baraza la
wanyama ambalo lilimshauri kuhusu masuala ya uongozi.
Baraza hilo liliongozwa na Kobe. Wanyama wengine
walioshirikishwa kwenye baraza hilo walikuwa ni pamoja
na Kiboko, Mbwamwitu, Ngiri, Sungura, Lumbwi, Duma na
Chatu. Mara kwa mara Simba angewaita wanyama wa
baraza hilo ili wazungumzie uongozi wa porini. Baraza hili
pia ndilo lililotunga sheria na kuamua kesi zote za wanyama
wa porini.
Simba alipendwa na wanyama wote. Uongozi wake pia
ulishabikiwa na takriban wanyama wote porini.
Siku moja Simba aliwapata watoto wa Paa na Chui wakicheza.
Mtoto wa Paa alikuwa akitokwa na jasho kwa sababu ya
kukimbia sana.
“Njoo nikupanguse jasho, mtoto,” Simba alisema kwa upendo.
Mtoto wa Paa alienda kwa Simba akarambwa jasho lote.
Asante sana. Najisikia safi sana,” mtoto wa Paa alimshukuru
Simba.
Jasho lako ni tamu sana. Nina hamu ya kukulamba tena na
tena. Udugu ni kufaana sio kufanana eti,” Simba alisema
kisha akawaaga watoto wa Paa na Chui.
Simba aliendelea na tabia yake ya kuwalamba watoto jasho
wakicheza. Aligundua kuwa watoto wa Paa ndio waliokuwa
na jasho tamu zaidi. Kadri alivyoendelea kuwalamba watoto
jasho hao, ndivyo alivyozidi kujawa na hamu ya kutaka
kuwalamba zaidi.
31
32
Simba alianza kuwafuata watoto wa Paa kila walipokwenda.
Siku moja watoto wa Paa walicheza na kuumizana sana.
Walimwona Simba akipita wakamwita kwa sauti. Simba
alikwenda mbio na kuanza kuwalamba. Mmoja wao alikuwa
ameumia vibaya kwenye goti. Alivuja damu. Hata kutembea
alishindwa.
Simba alimlamba damu yote na kuimeza. Ilikuwa tamu
sana. Alitamani sana goti la mtoto wa Paa livuje zaidi ili
alilambe, lakini halikuvuja. Wazo lilimjia Simba.
“Nitamchukua mwenzenu niende naye. Nataka kwenda
kumpaka dawa kwenye kidonda hiki. Mama yenu akija
msiseme nimemchukua. Akijua ameumia atawaadhibu
kwa kumuumiza. Mwenzenu akipona nitamrudisha,” Simba
aliwaambia watoto wa Paa.
Paa aliporudi kutoka mtoni alishangaa kuona kuwa wanawe
ni watatu badala ya wanne. Alipowauliza kuhusu mtoto
mwenzao walimdanganya.
“Hatujui ameenda wapi,” walisema kwa pamoja.
Paa alianza kumtafuta mwanawe. Alimtafuta hadi akachoka.
Aliamua kwenda kwa baraza la wanyama kuripoti kisa hicho.
Alipofika alipata wanyama hao kwenye mkutano. Simba
alikuwa mwenyekiti naye Kobe alikuwa katibu kwenye
mkutano huo wa baraza la wanyama. Paa alikaribishwa
vizuri. Aliwaeleza kisa hicho cha kumpoteza mwanawe kwa
majonzi makuu. Alipomaliza kueleza machozi ya huzuni
yalimtiririka. Wanyama wote walimpa pole.
33
34
“Usilie, Bi. Paa. Mwanao atapatikana bila shaka. Nitawatuma
askari wangu, Chui na Mamba, waende kumsaka. Hata nawe
usichoke kumtafuta. Atafutaye hachoki akichoka keshapata,”
Simba alimtuliza Paa. Simba pia alijifanya kushangazwa na
kisa hicho cha mtoto wa Paa kupotea.
Mtoto wa Paa hakuonekana tena. Watoto zaidi waliendelea
kupotea. Pundamilia, Ndovu, Mbogo na Sungura pia
waliwapoteza watoto wao kwa njia ambazo hazikueleweka.
Wanyama wote hawa walipeleka habari hizo za kuhuzunisha
kwa baraza la wanyama.
“Moyo wangu ni mzito. Kuna taharuki porini. Watoto wa
wanyama wakiendelea kupotea amani itatoweka. Tufanye
nini wenzangu?” Kobe aliwauliza wanyama wenzake katika
baraza.
“Dawa ya mwizi wa watoto ni kukamatwa. Siku za mwizi
ni arubaini. Nimemwamrisha amirijeshi, Bwana Kifaru,
kutuma jeshi lake porini ili liwatafute na kuwakamata wezi
wa watoto,” Simba aliwaelezea wanyama kwenye baraza.
Alijidai kuwa mwenye simanzi kuu.
Majonzi yalitanda porini. Visa vya watoto kupotea bila
kuonekana tena viliongezeka maradufu. Wanyama na watoto
wao waliishi kwa woga. Walikonda kama ng’onda kwa kuwa
hawakula wakashiba.
Wanyama wote waliogopa kwenda kwenye pori za mbali
kulikojazana miti, majani na nyasi. Walihofia kuwa huko
ndiko kulikokuwa na adui. Walikula pamoja kwenye
kiwanja kikubwa. Hapo nyasi zilikuwa chache na majani
yalikuwa haba. Kila mnyama aling’ang’ania chochote kidogo
kilichopatikana. Maji nayo vilevile yalikwisha.
35
Mito iliyokuwa na maji mengi ilikuwa katikati ya pori kubwa.
Huku pia waliogopa kwenda. Waliumia kwa kukosa maji
hata ya kukata kiu.
36
Amirijeshi Bwana Kifaru aliwaamrisha Chui kumsaka mhalifu.
Baada ya siku mbili za kuichana pori, Chui alijionea maajabu.
Akiwa juu ya mti alimwona Simba akimlambalamba mtoto
wa Fuko. Kisha alimnyonyoa manyoya kwa meno. Halafu
alianza kumla polepole sikio, pua, mkono wa kulia, mkono
wa kushoto na mguu wa kulia.
Chui alishindwa kuvumilia. Hasira zilimpanda akamrukia
Simba huku akijisemea, “Liwalo na liwe. Nitamrarua hata
kama ni mfalme. Hawezi kuwatendea wanyama dhuluma
kama hii.”
Simba hakuamini alipokabwa koo na Chui. Walimenyana
na kubingirishana huku wakitiana kucha vibaya. Hatimaye
vita viliisha baada ya wote kupata majeraha mengi.
“Samahani sana Chui. Naomba radhi kwa tukio hili. Hapakuwa
na haja ya kupigana hivi. Nakuomba uonje nyama hii kisha
tuongee,” Simba alimshawishi Chui.
“Siwezi kula mtoto wa mnyama mwingine. Ni kama kuila
kesho yetu,” alisema Chui kwa unyonge.
“Unahitaji nguvu. Katika hali yako hii, usipokula utakufa.
Hebu jiangalie ulivyokonda hata mifupa ya mbavu zako
inahesabika. Nasema uonje tu,” Simba alizidi kumbembeleza
Chui.
Chui alinusa harufu ya kuvutia ya damu ya mtoto wa Fuko.
Njaa aliyokuwa nayo ilizidi kumtafuna tumbo. Aliunyoosha
mkono na kupokea kipande cha ini kutoka kwa Simba.
“Ni tamu sana, tena ina wororo wa ajabu. Naomba kipande
kingine,” alisema Chui kwa hamu kuu.
Simba na Chui walimla mtoto wa Fuko akaisha.
37
“Sasa umekula kiapo. Huwezi kusema uliloliona wala
kulitenda. Tutakuwa tukila nyama pamoja kuanzia leo,”
Simba alimwambia Chui.
Chui alisalimu amri. Alijua amekuwa mtumwa wa Simba.
Lazima angefanya alivyosema. Kuanzia siku hiyo Simba na
Chui walikula watoto wa wanyama pamoja. Simba na Chui
walifanya urafiki wa chanda na pete. Baada ya wiki moja
Chui alinona kama Simba.Wanyama walishangaa sana kuona
mabadiliko haya ya haraka ya Chui. Fisi alijaribu kumdadisi
Chui kuhusu alikopata chakula cha kumnonesha, lakini Chui
alikataa kutoa siri.
Fisi hakufa moyo. Alianza kumfuata Chui kila alipokwenda
kisirisiri. Siku moja Fisi aliwaona Chui na Simba kwa mbali
porini. Alinyatianyatia na kufika walipokuwa. Alijificha
nyuma ya kichaka ili achunguze waliyokuwa wakiyafanya.
Baada ya muda aliwaona wakipangusa midomo yao kwa
majani ya miti. Kisha wawili hao waliondoka hapo wakicheka
kwa furaha.
Fisi alikwenda hadi pale ambapo Simba na Chui walikuwa
wamesimama. Aliona maajabu. Kulikuwepo na kwato na
pembe za mtoto wa Swara. Mahali penyewe pia palijaa
matone ya damu. Fisi alichanganyikiwa asijue yaliyojiri.
Alijiendea zake na kuamua kuendelea kumwandama Chui.
Bidii hulipa. Bidii ya Fisi ya kumfuata Chui ilizaa matunda
hatimaye. Siku moja jioni Fisi aliwaona tena Chui na Simba
kwa mbali. Walikuwa wanakula kitu porini.
“Labda wanakula uyoga. Ngoja nikavamie ili nijue siri ya
kunona kwao,” Fisi alijisemea kimoyomoyo.
Fisi alipofika walipokuwa Simba na Chui alipigwa na butwaa.
38
“Kwa nini umepigwa na butwaa? Karibu tule, acha wasiwasi,”
Chui alimwambia Fisi. Fisi alivyo mlafi hakusita. Alianza kula
nyama ya mtoto wa Nyati kwa pupa.
“Nyama hii ni tamu sana,” Fisi alisema huku ameshika mfupa
mkubwa.
Simba, Chui na Fisi sasa walifanya usuhuba. Popote
alipokwenda Simba, pia Chui na Fisi walienda. Baada ya wiki
moja, Fisi alinona ajabu. Alianza kutembea akichechemea
kwa uzito wa mwili wake. Miguu yake ya nyuma ilionekana
mifupi kuliko ya mbele. Ilishindwa kuhimili uzito wa mapaja
yake.
Wanyama wengine walishangazwa sana na mabadiliko haya
ya Fisi ya ghafla. Alipoulizwa na wanyama wenzake kuhusu
asili ya kunona kwake alijibu huku akichekacheka, “Urefu
ni maumbile, lakini unene ni bidii ya mnyama mwenyewe.
Nendeni porini mkatafute lishe. Huko ndanindani kuna uyoga
mwingi.” Fisi alitaka kuwahadaa wanyama ili waende porini.
Huko yeye, Simba na Chui wangeweza kuwanyakua watoto
wa wanyama hao kwa urahisi.
Asubuhi moja, jua lilipokuwa linachomoza Kima aliona
vioja porini. Alikuwa juu ya mti wa vitoria kama kawaida
yake akishtaki njaa. Mara aliwaona Simba, Chui na Fisi
wakimkaba koo mtoto wa Ngiri. Mtoto huyo alilia kwa sauti
ya huruma. Aliwaomba watatu hao wamhurumie lakini
wapi! Waliendelea kumtia kucha na kumrarua. Alijaribu
kujiokoa kwa kuwadunga kwa vipembe vyake lakini hakufua
dafu. Kima aliwaza na kuwazua. Alitamani sana kumwokoa
mtoto wa Ngiri lakini alijua hakuwa na uwezo. Katika hali
hiyo ya kufisha moyo wazo lilimjia. Alichukua simu yake na
kurekodi video ya yote yaliyojiri.
39
“Huyu atakuwa mtoto wa mwisho kuliwa,” Kima alijisemea
moyoni.
Chui, Simba na Fisi walipomaliza kula, Kima naye alimaliza
kurekodi video yake. Aliitazama tena video hiyo bila kuamini
kisha akaituma kwenye mtandao wa kijamii.
Chui, Simba na Fisi waliporudi nyumbani walilakiwa na
wanyama waliokuwa na ghadhabu. Hawakuamini walipoiona
video yao ilivyosambaa mtandaoni kama moto wa kichaka
kikavu. Hata televisheni zilikuwa zinatangaza maovu yao.
Chui, Simba na Fisi kuona hivyo walijaribu kutorokea porini.
Walikimbia kadri ya uwezo wao. Simba alibahatika kutoweka
bila kuumia lakini Chui alikwaruzwa na miba akikimbia
akapata majeraha kidogo kwenye ngozi yake. Kuanzia siku
hiyo, Chui akawa na madoadoa mwilini. Fisi naye alishindwa
kukimbia kabisa kwa sababu ya kunona. Kwa bahati mbaya
alikunguwaa na kuanguka vibaya akavunjika miguu ya
nyuma ambayo tayari ilikuwa imelemewa na uzito. Wanyama
walimshika na kumpatia kichapo kibaya.
Fisi alilia na kuropokwa kila kitu. Alizisema njama zao zote
za kihuni walizokuwa wamewapangia wanyama. Alilia na
kuomba msamaha kwa niaba yake na wahuni wenzake.
Kobe aliita mkutano wa dharura wa baraza la wanyama.
Iliamuliwa kwa kauli moja kuwa Kima apewe wadhifa
wa amirijeshi. Aliahidi kuwalinda wanyama kwa
kuwatahadharisha kila alipowaona adui. Kuanzia siku
hiyo kima aliruka kutoka mti mmoja hadi mwingine porini
akiwafuata wahalifu. Kila alipowaona Chui, Simba na Fisi
angepiga kelele. Wanyama wangetoroka ili kuokoa maisha
yao.
40
41
Kobe aliamua kuwa Ndovu, Twiga, Kifaru na Chatu wateuliwe
kama walinzi wa wanyamapori. Uteuzi wao ulikaribishwa
kwa mikono miwili. Ndovu alitumia nguvu zake kupambana
na maadui. Hakuna mnyama aliyemla mwingine Ndovu
akiwa karibu.
Wanyama waliokuwa katika hatari ya kuliwa walitembea
unyo kwa unyo wakiwa na Ndovu wakati wa kulisha. Twiga
aliwafaa wanyama kwa sababu ya urefu wake. Aliweza
kuwaona maadui kutoka mbali na kuwafahamisha wanyama
mapema ili wajifiche.
Kifaru alikuwa mpiganaji hodari. Upembe wake mrefu
ungewararua adui kila walipowashambulia. Chatu
aliwalinda wanyama mitoni wakinywa maji. Simba, Chui
na Fisi walimwogopa sana Chatu. Aliwapinda wakati wote
walipotaka kuwadhuru wanyama.
Simba, Chui na Fisi walipewa onyo kubwa dhidi ya kuwala
watoto wa wanyama. Waliogopa na kukoma kabisa kula
watoto. Walijizuia pia kula mnyama aliyekuwa na mimba.
Walipotaka kula nyama, walimfukuza mnyama aliyekuwa
amekomaa.
Simba, Chui na Fisi pia walifurushwa na wanyama wenzao.
Walianza kuishi kwenye pori yao mbali na wanyama wengine.
Hii ilikuwa adhabu kubwa sana. Walijihisi wapweke na
kujawa na huzuni kwa kuwa upweke ni uvundo. Kuanzia siku
hiyo Simba, Chui na Fisi hutembea peke yao. Wanyama wale
wengine porini nao hutembea katika vikundi ili walindane.
42
Kamusi Yangu
akashtaki njaa akaanza kula chakula
alikunguwaa alijikwaa
alimnyonyoa alimtoa manyoya
alinyatianyatia alimwendea polepole ili amshike
alipigwa na
bumbuwazi alishtuka
amekula kiapo ameweka ahadi ya kutenda jambo fulani
au kutotenda
alisalimu amri alikubali
amirijeshi kiongozi mkuu
ghadhabu hasira
hakufua dafu hakufaulu
kuichana pori kukimbia
kukata kiu kunywa maji
kumdadisi kumuuliza maswali
kuropokwa kusema maneno mengi bila umakinifu
kutoweka kutoonekana tena
maradufu mara mbili ya idadi
mtumwa mtu ambaye anamilikiwa na mtu mwingine
na anayefanyishwa kazi bila malipo
njaa ilimtafuna
tumbo alihisi njaa nyingi
simanzi huzuni
taharuki hali ya wasiwasi
takribani inayokaribiana na idadi fulani
unyo kwa unyo kufuatana kwa karibu sana
urafiki wa
chanda na pete urafiki wa karibu sana
usuhuba urafiki
vitoria tunda dogo la mwituni lenye chachu
43
walikonda kama
ng’onda walikonda sana
walimenyana walipigana
yalitanda yalijaa
44
Maswali
1. Ni mnyama gani aliyekuwa mfalme porini?
2. Kwa nini Simba alipendwa na wanyama wote porini?
3. Kwa nini watoto wa Paa waliogopa kumwambia mama
yao ukweli?
4. Kwa nini wanyama wa porini walikonda?
5. Eleza jinsi ambavyo Kima aliweza kugundua uhalifu wa
Simba, Chui na Fisi.
6. Unafikiri nini kilichotokea kabla ya Fisi kuona kwato na
pembe za mtoto wa Swara?
7. Taja:
a. wanyama wote waliosimuliwa kwenye hadithi.
b. wanyama wa porini watano wakubwa zaidi hapa nchini.
8. Je, kwa mujibu wa hadithi hii kwa nini wanyama wengine
hula nyama?
9. Taja wanyama walao:
a. nyasi
b. nyama
c. matunda
d. majani
e. mchanganyiko wa nyama, matunda na majani
10. Hadithi hii imekufunza nini?
Mazoezi
1. Kaa ukitazamana ana kwa ana na rafiki yako. Zungumzeni
kuhusu wanyama wa porini.
Maswali yafuatayo yatawaongoza:
a. Wanyama wa porini wana faida gani kwa binadamu?
b. Wanyama wa porini wana haki gani?
c. Kwa nini ni muhimu kuwalinda wanyama wa porini?
d. Wawindaji haramu wanastahili kupewa adhabu gani?
e. Unaweza kumshauri vipi mkulima ambaye mazao
45
yake yameliwa na kima?
2. Msimulie rafiki yako hadithi uliyosoma kwa maneno yako
mwenyewe. Tumia ishara za uso, mikono na mabega
kujielezea. Unaweza kujirekodi ukisimulia kisha umtumie
mwalimu wako rekodi hiyo akutathmini. Kisha:
a. tajeni visawe vya maneno haya:
i. lumbwi
ii. mbogo
iii. usuhuba
iv. ghadhabu
v. haba
b. tambueni methali zilizotumika kwenye hadithi hii.
3. Chora wanyama watano wa porini uwapendao kisha
uwapake rangi.
4. Andika hadithi yoyote kuhusu wanyama wa porini kwenye
chombo cha kidijitali. Mtumie mwenzako kwa njia ya
mtandao akutathmini.
46
Sala ya Salome na Sami
47
48
Salome na Sami walipiga magoti waombe kabla ya kulala.
Walikubaliana kusali kwa zamu. Kila mmoja wao alikuwa
na sala zake alizotaka kusema. Sami alianza yeye kusali
kwa sauti,
“Mungu nakuomba uwe dira yetu maishani. Tupe nasaha.
Tuwezeshe kutega sikio ili tukiitwa tuitike. Tukitumwa
twende mbio. Tupe uvumilivu na nia ya kupenda kutenda
mema. Tujalie moyo wa bidii masomoni na kazini. Wajalie
wazazi na walezi wetu nguvu za kufanya kazi ili waweze
kuyatimiza mahitaji yetu. Naomba ewe Mungu uwawezeshe
wazazi wangu kuninunulia kipakatalishi. Amina!”
Naye Salome aliomba,
“Mungu Mwenyezi tunakuomba utukumbushe siku zote
kuwasaidia wenzetu. Tuishi nao kwa upendo na amani.
Nakuomba ewe Mungu wetu utusaidie tuwe watoto watiifu
na wenye heshima. Tuepushe na shari na utupe heri. Wajalie
wazazi wangu uwezo wa kuninunulia baiskeli. Amina!”
Salome na Sami walisikia wazazi wao wakipiga makofi
baada ya kumaliza kusali. Kumbe walizisikia sala za Salome
na Sami. Siku mbili baada ya sala zao, Sami aliletewa
kipakatalishi kipya. Salome naye aliletewa baiskeli mpya.
Sala zao zilikuwa zimejibiwa. Salome na Sami walifurahi
na kumshukuru Mungu na wazazi wao.
49
Kamusi Yangu
amani hali ya kutokuwapo vita na machafuko; salama
dira kifaa kinachoonyesha pande nne kuu za
dunia. Huwa kama mwongozo kwa msafiri wa
safari ya mbali
heshima tabia njema; adabu
nasaha ushauri ambao mtu hupewa ili aweze kuishi vizuri
nia kusudio la kufanya jambo; lengo
shari jambo baya
upendo hali ya kuvutia moyoni na mtu au kitu
uvumilivu hali ya kuvumilia mambo magumu
50
Maswali
1. Sami alimwomba Mungu nini?
2. Weka alama ya kwenye jibu sahihi.
Kutega sikio kunamaanisha nini? __________________
a. Kusikiliza maneno ambayo hayakuhusu.
b. Kusikiliza kwa makini.
c. Kusikiliza maneno muhimu peke yake.
d. Kusikiliza kwa sikio moja.
3. Salome alimwomba Mungu nini?
4. Kwa nini ni muhimu kutia bidii maishani?
5. Sala za Salome na Sami zilijibiwa vipi?
6. Umejifunza nini kutokana na hadithi hii?
Mazoezi
1. Ukiwa na rafiki yako:
a. Msomee hadithi hii huku akurekodi kwenye kifaa
cha kidijitali kama vile simu ya mkononi.
b. Sikilizeni rekodi hiyo huku ukihesabu idadi ya
maneno ambayo unaweza kusoma kwa dakika moja
kwa usahihi.
2. Paka rangi maneno haya heshima, shule, huruma, utiifu,
amani, heri, shari, masomo, mema, moyo kwenye mraba
huu.
h u r u m a
e m e m a m
s h u l e a
h e r i z n
i s h a r i
m a s o m o
a m o y o k
u t i i f u