Akili ni Mali
na Hadithi Nyingine
Pauline Kea
Akili ni Mali na Hadithi Nyingine
Kimechapishwa na Queenex Publishers Limited
S.L.P 56049-00200, Nairobi, Kenya.
Simu: 0727 794 498, 0715 808 200
Baruapepe: info@queenexpublishers.co.ke
queenexbooks@gmail.com
Tovuti: www.queenexpublishers.co.ke
© Pauline Kea, 2022
Haki zote zimehifadhiwa. Hairuhusiwi kuiga, kunakili,
kupigisha chapa, kutafsiri au kutoa kitabu hiki kwa jinsi
yoyote ile bila idhini kwa maandishi ya Queenex Publishers
Limited.
ISBN: 978-9966-141-96-5
Chapa ya kwanza 2022
Mganga Sungura
1
2
Hapo zamani za kale Sungura alikuwa mganga tajika. Sungura
alisifika kwa ujuzi wake wa tiba za kiasili. Kila uchao wanyama
walifurika kwake ili kupimwa na kupewa dawa za kienyeji. Sifa
sufufu za Sungura zilienea kama moto wa kichaka kikavu.
Alifanya utafiti wa kina maabarani mwake ili kuvumbua dawa
mpya na faafu zaidi.Alichanganya dawa kutokana na majani,
mabaka na mizizi ya miti na kupata dawa zenye nguvu za
ajabu. Magonjwa yaliyowashinda madaktari na waganga
wenzake yeye aliyatibu mara moja. Huduma za mtandao
zilimfaa sana Sungura. Mara nyingi angesakura mtandaoni ili
kupata maarifa zaidi kuhusu tiba hizo za kiasili.
Sungura aliheshimiwa sana na wanyama wenzake. Mfalme
Simba pia alizitambua jitihada za Sungura na kumpa madaraka
katika utawala wake. Sungura alipewa wadhifa wa Waziri
wa Afya. Cheo hiki kilimwafiki Sungura. Alizidi kuwatumikia
wanyama wenzake kwa moyo mkunjufu.
Sungura alizidisha bidii ya kazi akazidi kufanikiwa.Wasemao
husema, ukijitahidi utafaidi.Aliamua kupanua mawanda yake
ya tiba kwa kufungua hospitali zaidi.Alichukua mkopo mkubwa
wa benki ili kuitimiza ndoto hii yake.
“Nimemaliza kujenga hospitali zangu. Najua wateja watafurika,
Sungura alimwambia Mfalme Simba siku moja.
“Ombi letu ni kuwa kusiwe na wagonjwa.Tumefanya kampeni
nyingi kuhusu namna ya kuzuia magonjwa na pia wanyama
wengi wamepokea chanjo. Ninafikiri hospitali zako zitapata
mgonjwa mmoja mmoja tu, Mfalme Simba alimwambia
Sungura.
Sungura alishtuka alipokumbushwa ukweli huo. Baada ya
kutafakari kauli za Simba, aligundua kuwa zilikuwa na ukweli
mwingi. Sungura aliwaza na kuwazua, “Nahitaji kufanya
mikakati ili hospitali zangu zipate wateja. Nahitaji hela za
3
kulipia mikopo yangu, Sungura alijisemea.
Sungura aliamua kutumia mbinu yoyote ile ili apate wateja.
“Nitatengeneza mabango ili kutangaza biashara zangu,
Sungura alijisemea huku akitengeneza mabango ya kuvutia.
Mabango yake yalionyesha wanyama wanaotoka kwenye
hospitali zake wakiwa wenye tabasamu.
Jitihada hizi za Sungura hazikufua dafu.Wanyama walipendezwa
na mabango yake lakini hawakuenda hospitalini.
“Kwa nini wanyama hawaendi hospitalini kwangu hata baada
ya kuwawekea mabango?” Sungura alimuuliza Waziri wa
Sheria, Bwana Kobe.
“Mabango yanayozitangaza hospitali zako yanavutia kweli.
Wanyama wanayasifu, ila hawawezi kwenda hospitali kama
hawajaugua, Kobe alimjibu Sungura kwa tabasamu.
“Asante sana, Bwana Kobe. Umenikumbusha kitu, alisema
Sungura kwa furaha.
“Nimekukumbusha nini, mwenzangu?” Kobe alimuuliza Sungura.
“Kuwa katika utamaduni wetu tiba na imani hazifai
kutenganishwa, alisema Sungura kisha akaangua kicheko.
“Maana yake?” aliuliza Kobe.
“Ina maana kuwa nitapata wateja, Sungura alisema na
kumuaga Kobe harakaharaka.
Sungura alikwenda kutengeneza mabango tofauti. Mabango
yake yalilenga imani za wanyama zaidi kuliko magonjwa.
Alilipamba jiji lao kwa mabango yake. Siku iliyofuata wagonjwa
walianza kumiminika kwenye hospitali zake.
4
5
Sungura aliwahudumia wagonjwa wake halahala kwa kuwa
walikuwa wengi kupita kiasi. Aliwahadaa kuwa matatizo
yao yangekoma baada ya muda. Aliwatoza ada kubwa na
kuwaitisha vitu vya aina aina. Sungura alikwenda kwenye benki
na kulipa mkopo wake.Alibaki na pesa nyingi zisizohesabika.
Namna alivyozidi kupata pesa ndivyo alivyozidisha tamaa.
Sungura alibuni mbinu nyingine nyingi za kujipatia pesa.Alipanua
shamba lake na kuwa mkulima aliyesifika. Alipanda mboga
na matunda. Aliyauza mazao yake sokoni na kujipatia pesa
zaidi.Wanyama walioshindwa kulipa ada baada ya kugangwa
walimfanyia Sungura kazi shambani mwake. Sungura alianza
kuwatumikisha wanyama wenzake.
Sungura aliona kuwa bado alihitaji wateja zaidi.Alimtafuta Fisi
ili amsaidie kwenye njama nyingine ya kuongezea wanunuzi
wa huduma zake.
“Fisi, naomba msaada wako. Nitakulipa. Unahitaji tu kufuata
maelekezo ambayo nitakupa, Sungura alimwambia Fisi.
Fisi alishawishika haraka. Sungura alimpaka Fisi asali mwili
wote. Kisha alifungulia nyuki waliokuwa kwenye mzinga. Nyuki
hao walimganda Fisi mwilini.
“Haya, shika pikipiki hii. Nenda nayo sokoni. Wanyama
wakikuuliza sema uliiba pikipiki na nyuki wakakuganda. Nataka
ukifika ulie kwa sauti ili wanyama waje kushuhudia uganga
wangu. Nimesema na Ngiri ili aje kudai kuwa ulimwibia pikipiki
akaja kwangu nimgange. Mimi nitakuja baadaye kidogo ili
nikutoe nyuki mwilini na nimpe Ngiri pikipiki.Tutateka imani
ya wanyama wengi na watazidi kuja kwangu ili niwagange.
Wajinga ndio waliwao eti!” Sungura aliifafanua njama yake.
Sungura alipofika sokoni alipokelewa kama mfalme.Wanahabari
walikuwa wamekongamana tayari kumhoji. Fisi naye alilia
kama mtoto mdogo.Alijidai kuwa nyuki walikuwa wamemvamia.
6
Aliendelea kushikilia pikipiki ambayo ilikuwa inang’ong’wa
na nyuki. Alijidai kuwa alikuwa ameganda kwenye pikipiki.
Wanyama waliziajabikia sarakasi hizi.Wengi walipiga picha
tukio hili na kuliweka mitandaoni.
Fisi alianza kumwomba Sungura msamaha.
“Mganga Sungura, ninakuomba unisamehe. Nakuomba
uniondolee dhiki hii. Sitaiba tena, Fisi alisema huku akibubujikwa
na machozi.
“Nimekusamehe. Nitakutoa nyuki hawa. Nataka uwe funzo kwa
wezi wote. Nataka pia watu wafahamu kuwa mimi si daktari
tu, bali pia mganga wa waganga anayeweza kuagua kila kitu!”
alisema Sungura kwa ukakamavu.Wanyama walishangilia na
kumpigia Sungura makofi.
Ngiri alifika akihema kama alivyokubaliana na Sungura.
“Sijui nikulipe nini, Mganga Sungura.Asante kwa ajili ya dawa
uliyonipa. Mwizi amepatikana.Ama kweli, hakuna mfano wako.
Wewe ni zaidi ya mganga. Ni mganguzi hasa!” alisema Ngiri
huku akimpigia Sungura magoti.
Sungura alifurahi sana kwa kuwa mipango yake ilikuwa
imeenda kama alivyopanga.Alijua kuwa wateja wake wangezidi
kuongezeka kwa kuwa alikuwa amewadhihirishia kuwa
angeweza kuwafanyia hata miujiza.
Sungura aliendelea kuwatapeli wanyama hata zaidi.Alicheza na
imani na itikadi za wanyama.Wakati mwingine alitumia vitisho
ili wanyama wamtafute na kumwomba awape huduma. Siku
moja Sungura alitangaza kuwa ugonjwa mbaya ungewavamia
wanyama.Aliwataka wanyama wote waende kwake kupata
chanjo. Aliwatoza ada kubwa kwa kuwadunga sindano za
maji ya chumvi. Nyani alishindwa kulipia huduma za Sungura.
7
Alipewa adhabu ya kifungo na kulima shamba la Sungura.
Nyani alishindwa kuvumilia akatoroka na kwenda kwa mfalme
kushtaki.
“Mfalme, nimekuja kwako kulalamikia dhuluma za Sungura.
Anatutoza ada kubwa kupita kiasi.Anatutapeli.
“Tunahitaji ushahidi wa kutosha ili tumpeleke Sungura
mahakamani.Wanyama wengi wamelalamika lakini hawana
ushahidi, Simba alijibu kwa huzuni.
Sungura aliitwa na Mfalme Simba ili kuulizwa kuhusu madai
ya Nyani. Alimtupia Mfalme Simba mikono kwa kiburi huku
akisema,“Kama umeshindwa kutawala, sema. Mimi ninaweza
kuongoza wanyama. Sasa nina wafuasi wa kutosha. Nikiomba
kura nitapata.Tena nina pesa za kutosha za kufanya kampeni.
“Ama kweli kikulacho ki nguoni mwako.Wewe waziri wangu
unataka kuipindua serikali yangu? Naona unatangaza vita.
Uko tayari kupambana?”
“Aliye na macho haambiwi tazama. Nimekuwa nikiweka
mikakati yangu. Naendelea kuiboresha tu, Sungura alijibu
kwa ukakamavu.
Sungura alitoka kwa Mfalme Simba na kuelekea moja kwa
hadi kwenye ofisi za wasajili wa vituo vya habari.Alisajili kituo
chake cha habari kilichoitwa Imani TV. Kituo chake kilianza
matangazo mara moja. Alitangaza dawa na hospitali zake.
Alionyesha pia miujiza yake ya uongo akiponya wanyama
kwenye kituo hicho.Alipata wafuasi wengi mno.Aliwahimiza
wafuasi wake wamtumie maombi yao pamoja na pesa ili
awaombee wapone. Wafuasi wake walitii kikondoo. Aliuza
pia maji ya baraka kwenye chupa ya nusu lita kwa bei ghali
sana. Wafuasi wake walinunua maji hayo kwa wingi. Utajiri
wa Sungura haukuwa na mfano.Alikuwa amefanikiwa kutumia
8
imani na itikadi za wanyama kujipatia chochote alichotaka.
Sungura aliwafanya wanyama kuamini kuwa wangepona kwa
kugusa gauni lake tu! Sungura alijihisi kama mungu mdogo.
Siku moja Sungura alitangaza janga la njaa kupitia kwenye
kituo chake cha televisheni.Aliwaambia wanyama kuwa kama
wangetaka kunyeshe, basi hawakuwa na budi kumwabudu yeye.
Simba aliposikia tangazo hili alifadhaika sana.Aliita mkutano
wa dharura wa mawaziri wake. Hakumwalika Sungura.
“Ndugu zangu, Sungura anataka kuipindua serikali yetu.
Amewahadaa wanyama na kuwateka fikra. Amewafanya
kuamini kuwa mimi ni adui yao.Amewadanganya kuwa mimi ni
mchawi wa kupindukia.Wanyama hawataki tena niwe mfalme
wao. Sijui nifanyeje, Simba aliwaelezea wenzake kwa huzuni.
“Nina wazo. Nataka tumwekee Sungura mtego ili tuthibitishe
kuwa ni mwongo. NamwombaWaziri Nyati atangaze kwenye
kituo cha televisheni ya kitaifa kuwa amempoteza mwanawe.
Kisha aende kwa Sungura kuomba huduma. Nitatangulia
kwenda pangoni kwa Sungura ili nijifiche na kuchukua video
wakati wa mazungumzo yao. Nitajifanya kuwa jiwe kubwa.
Nitakaa kando ya mawe ambayo Sungura hukalia akifanya
uganga wake, Kobe alieleza kwa utaratibu.
“Hilo ni wazo zuri, Bwana Kobe. Naipenda hekima yako.
Nataka tuiweke rekodi hiyo kwenye mitandao ili tumuumbue
Sungura akome tabia yake ya kuwahangaisha wanyama.
Lazima tumkomeshe tapeli huyu, Nyati alisema.
Nyati alitoka mkutanoni na kwenda moja kwa moja hadi
kwenye kituo cha televisheni. Huko alitangaza kupotea kwa
mwanawe kitindamimba. Sungura alipozipata habari hizi
alifurahi sana.Alitaka kuitumia fursa hiyo kumkosanisha Nyati
na Simba.Alimpigia Nyati simu mara moja.Alimwalika Nyati
kwake ili amgangue. Nyati naye alijidai kuwa alihitaji msaada
9
wa Sungura kwa dharura.Alikwenda mara moja alipoalikwa.
Aliandamana na mkewe. Kobe naye alitangulia kwa Sungura
kama walivyokuwa wamepanga. Alijibanza kando ya mawe
ambayo Sungura alipenda kukalia akifanya uganga wake.
Alitayarisha simu yake ili arekodi video ya yote ambayo
yangejiri kati ya Sungura na Nyati.
Nyati alipowasili alimpata Sungura tayari amevalia maleba
yake ya uganga. Alitisha kuliko ibilisi. Usoni alivaa barakoa
yenye meno na macho ya kutisha kwelikweli. Mwilini alivaa
kabuti iliyoshonwa kwa vipande vya ngozi za chui, chatu na
twiga. Kabuti lake alilipamba kwa mabawa makubwa ya ndege.
Kichwani alivaa taji la dhahabu ambalo lilikuwa limerembeshwa
kwa manyoya ya tausi.
Kobe alianza kazi yake ya kurekodi video punde tu Nyati
na mkewe walipowasili. Nyati na mke wake walipokelewa
na Sungura, kwa kishindo. Hawakutarajia mambo yawe
yalivyokuwa kwa hivyo walijawa na hofu. Hawakuamini kuona
Sungura akiwa mkali kama simba na mchafu kama fuko.
“We’! Hapa hapana haraka! Vulia viatu huko nje!” alisema
Mganga Sungura kwa sauti ya juu na ya kutisha.
10
11
Nyati na mke wake waligeuka na kutoka pangoni.
“We! We! Mtaikasirisha mizimu. Rudini kinyumenyume.Vile
mlivyoingia. Hakuna cha kugeuka. Mizimu haionyeshwi mgongo.
Naona hamzifahamu itikadi zetu. Leo nitawafunza!”
Nyati na mkewe walivua viatu na kuingia pangoni polepole
kama konokono. Humo ndani, Sungura aliwavisha magauni
meusi kama makaa na kuwafunga viunoni mishipi miekundu
kama damu.
“Haya, semeni shida zenu.Wewe! Wewe! Ni nani aliyekuambia
kuwa hapa wanawake wana ruhusa ya kuvaa suruali ndefu?
Nenda!Tokomea kabisa!” Sungura alimkaripia na kumfukuza
mkewe Nyati.
Mke wa Nyati alitoka nje na kujikunyatia kando ya mlango
wa pango kama kifaranga aliyenyeshewa. Kobe aliendelea
kurekodi mazungumzo ya Sungura na Nyati kwa rununu yake
huku akifungia kicheko.
“Nawe, mbona una wasiwasi kama kuku mgeni? Ni yepi
yaliyokuleta hapa?” Sungura alimuuliza Nyati kwa bezo.
“Nimepata msiba, yaani tumepata msiba, mimi na mke wangu.
Tumempoteza kitindamimba wetu.Tunafikiri kuna mnyama…”
Hakumaliza maelezo Sungura akarukia, “Bila shaka yupo
mnyama na ndio maana mko hapa.
“Ndio, daktari, alisema Nyati.
“Daktari ni nani? Eeh! Tangu lini nikawa daktari? Naitwa
mganguzi. Nyumba hii ina masharti eti! Usinibandike majina
ovyoovyo. Wewe uliye huko nje ninakuona. Ingia!” Sungura
alimwita mke wa Nyati.
12
Mkewe Nyati aliingia pangoni kwa woga kama kunguru.
“Shika leso. Jifunge.Tamaduni zetu lazima ziheshimiwe hapa.
Mwanamke ni gauni, si hivi viguo vyenu vya kuwabana
mnavyovaa siku hizi. Mwawatatiza mafundi wa nguo nyie,
alisema Sungura kisha akaangua kicheko kikubwa.
Ganga ganga za mganga ziliendelea huku Kobe akiendelea
kunasa sauti na kuchukua video kisirisiri. Sungura aliwazunguka
Nyati na mke wake huku akirukaruka kama kiroboto na
kuropokwa na maneno mengi kama chiriku.
Hatimaye alisema haya huku akichungulia nyungu, “Kuna
mnyama. Nimemwona. Huyu hapa. Mnyama mwenyewe si mrefu
kama twiga, si mwembamba kama sindano lakini ni mnafiki
kama panya.Anawawinda.Anataka kuwaangamiza ninyi na
kizazi chenu.Adui ni Mfalme Simba, lakini amedunda. Mganguzi
atamfunza adabu. Nitamkomesha! Nitaipindua serikali yake!”
Sungura aliwapatia Nyati na mke wake orodha ya vitu
ambavyo alitaka wamletee kama ada yake ili awatibu.
“Nataka kuku mweusi kama mpingo, jogoo mweupe kama
pamba na tausi maridadi kama kipepeo. Leteni vitu hivi baada
ya siku mbili niwatolee kisirani hiki. Niwape mtoto wenu.
Mkoba wangu nao mjue hautabaki bure, wataka pesa.Wewe!
Usije tena na hivyo viguo vyako.Wazee wamekasirika. Haya,
nendeni!” Sungura alisema huku akiwafukuza Nyati na mke
wake.
“Asante sana, mganguzi, Nyati na mkewe walisema kwa
pamoja. Walichomoka kama risasi na kwenda zao huku
wakicheka kama fisi. Kobe naye alitoka mafichoni taratibu kama
kinyonga na kuwafuata Nyati na mkewe.Wote waliandamana
hadi kwa Mfalme Simba.Walipofika walimchezea Simba video
ambayo Kobe alikuwa amerekodi. Simba alighadhibika fika.
13
“Sasa mmejionea wenyewe unafiki wa Sungura?” Mfalme
Simba aliuliza.
Kobe alimwomba Mfalme Simba awe na subira ili waweze
kumkamata Sungura.Waliamua kuandamana wanyama wengi
kwenda kwa Sungura baada ya siku mbili. Simba, kitindamimba
wa Nyati na wanyama wengine wangejibanza pembeni.
Siku hiyo ya siku, Nyati, mkewe, mtoto wao kitindamimba, Kobe,
Simba na wanyama wengine walikwenda kwa Sungura. Nyati
na mke wake walibeba ada waliyotakiwa kupeleka. Simba na
kitindamimba wa Nyati na wanyama wengine walijificha karibu
na pango la Sungura. Kobe alinyatianyatia na kujificha mahali
pake pa kawaida, huku akirekodi vituko hivyo vya Sungura.
“Haya. Karibuni. Nilijua mtarudi. Mtoto wenu huyu hapa.
Nipatieni vitu vyangu kwanza kisha niwape mwana wenu.
Mtieni kamba mguuni. Akipotea tena itawagharimu zaidi,
Sungura alisema kwa ukali.
Nyati na mkewe walimpatia Sungura vitu vyote alivyowatuma
kumletea. Sungura aliwakabidhi Nyati na mkewe mtoto bandia.
Kwa mbali alionekana mtoto wa Nyati lakini hakuwa na
kwato.Alikuwa na kucha ndefu badala yake.
Ghafla bin vuu, Simba, kitindamimba wa Nyati na wanyama
wengine walilizingira pango. Sungura alianza kubabaika.
Alitafuta mbinu za kutoroka akakosa. Chui alisimama tisti
kwenye mlango wa pango la Sungura.
Simba alinguruma hadi pango la Sungura likatetemeka. Sungura
alianza kulia kwa woga. Nyani alivua haraka ngozi na pembe
za Nyati ambazo alikuwa amevishwa na Sungura na kupiga
magoti aombe msamaha. Sungura kuona hivyo pia naye alipiga
magoti kuomba msamaha.
14
15
“Natubu. Naomba radhi kwenu na wanyama wote niliowakosea.
Tamaa ilinitawala. Msinidhuru, Sunguru alibubujikwa na
maneno na machozi kwa wakati mmoja.
“Una tamaa kama fisi wewe! Leo ulimwengu utazigundua
hadaa zako. Tutakuanika mtandaoni. Mrongo wewe. Mtoto
wetu kitindamimba huyu hapa, Nyati alimwambia Sungura.
“Hatuwezi kuchukua sheria mikononi. Tutafuata sheria.
Tutakufungulia mashtaka ili ufikishwe mahakamani. Chui, mtie
mhalifu pingu, Mfalme Simba alisema kwa hasira.
Nyani kuona hivyo alirukia tawi la mti na kutoweka.Tangu siku
hiyo Nyani alianza kuishi juu ya miti akichelea kukamatwa.
Hiyo ikawa adhabu tosha kwa Nyani. Sungura naye alitiwa
mbaroni. Alishtakiwa kwa makosa mengi lakini la kwanza
lilikuwa la jinai. Sungura alitakiwa kueleza kwa kina namna
alivyoweza kupata ngozi za wanyama ili atengenezee kabuti
lake.
“Sheria za nchi hii haziruhusu kamwe matumizi ya ngozi za
wanyama. Ili kupata ngozi ya mnyama yeyote lazima umuue.
Wewe ni muuaji!” Kobe alisema siku ya hukumu ya Sungura.
Sungura alitaka kukana makosa yake lakini akachezewa
video iliyorekodiwa.Wanyama wengi pia walijitokeza kutoa
ushuhuda wa namna walitapeliwa na Sungura. Fisi alijitokeza
na kuomba msamaha kwa kukubali kutumiwa vibaya na
Sungura.Wanyama walimsamehe alipoahidi kuwa angebadili
mienendo yake.
“Umeshtakiwa kwa kosa la kuwadhuru ndege na kutumia
manyoya yao bila idhini, Mfalme Simba aliongezea.
16
“Makosa yote hayo, pamoja na kosa la kuwahadaa wanyama
wenzako yanakupatia kifungo cha miaka mingi na kazi ngumu
gerezani, Kobe alitoa hukumu.
Siku hiyo, Mfalme Simba alitangaza sheria mpya zilizonuia
kuwakinga wanyama dhidi ya matapeli wa tiba,“Natangaza
kuwa kuanzia leo, daktari, mganga, muuguzi na yeyote yule
anayetaka kutoa huduma za tiba lazima apewe kibali maalum
na serikali.Tumeweka viwango thabiti ambavyo sharti vifuatwe
na wanyama wote kwenye tasnia ya uuguzi.Afya bora ni haki
ya kila mnyama na kuanzia leo serikali yangu itawapatia bima
kwa bei nafuu ili gharama ya matibabu ipungue.
Wanyama waliokuwa kortini siku hiyo walifurahi sana.Walijua
kuwa walikuwa wamefunguliwa pingu za itikadi za kidini na
za kijamii walizotiwa na Sungura. Kituo cha televisheni cha
Imani TV na Chama cha Imani vilifungwa mara moja.Wanyama
walirejelea maisha yao ya kawaida chini ya uongozi wa Mfalme
Simba.Waliishi kwa raha mustarehe.
17
Kamusi Yangu
akichelea akisita kufanya jambo fulani kwa
kuogopa matokeo mabaya
alifadhaika alibabaika
alijibanza alijificha nyuma au kando ya kitu
alimkaripia alimkemea
bezo dharau
bubujikwa tokwa na machozi au maneno kwa wingi
au ghafla
ghadhabika alikasirika sana
itikadi mkusanyiko wa imani zinashikiliwa na
watu fulani
maleba mavazi maalum yanayovaliwa na msanii
anapokuwa anafanya maonyesho
mizimu roho za wale waliofariki
sufufu nyingi mno au tele sana
tisti kusimama imara bila kuyumbayumba
18
Maswali
1. Sungura alitoa wapi maarifa kuhusu tiba za kiasili?
2. Kwa nini Sungura aliteuliwa kuwa Waziri wa Afya?
3. Toa sababu ambayo ilifanya hospitali za Sungura zisipate
wateja hapo mwanzoni.
4. Sungura alitumia ujanja gani kuhakikisha kuwa alipata
wateja katika hospitali zake?
5. Je, ni kwa nini Fisi hakuumwa na nyuki waliomnata mwilini?
6. Sungura alikuwa ameweka mikakati gani ili kupindua serikali
ya Simba?
7. Wanyama waliweza kudhihirisha vipi kuwa Sungura ni
tapeli?
8. Eleza namna ambavyo Sungura alipanga kumtapeli Nyati.
9. Umejifunza nini kutokana na hadithi hii?
10.Je, unafikiri sheria ya kutoa kibali maalum kwa wahudumu
wote wa tiba ingesaidia wanyama vipi?
19
Mazoezi
Sehemu ya A
Kusikiliza na Kuzungumza
a. Ukiwa na rafiki yako, zungumzeni kuhusu namna ya kudhibiti
itikadi za dini na za kijamii katika mazingira yenu. Maswali
haya yatakuongoza:
i. Je, ni itikadi gani za dini zinazopatikana katika mazingira
yenu?
ii. Ni itikadi gani katika utamaduni wenu zenye faida kwa
wanajamii?
iii. Ni mila gani katika mazingira yenu ambazo husababisha
hasara kwa wanajamii?
iv. Serikali hutumia mbinu gani kubadilisha mila na desturi
duni katika jamii?
b. Mwombe rafiki yako akusomee kurasa zozote tatu za hadithi
hii. Mwambie akuulize maswali yoyote manne kutokana na
kurasa hizo.
c. Msomee rafiki yako ukurasa mmoja wa hadithi hii. Mwombe
akuhesabie idadi ya maneno ambayo unaweza kusoma kwa
ufasaha kwa dakika moja. Rafiki anaweza kuwa mwanafunzi
mwenzako darasani.
Sehemu B
Ufahamu wa Kusoma
Jibu maswali haya.
1. Eleza jinsi ambavyo Mganga Sungura alibadilika na kuwa
tapeli.
2. Ni nini maana ya ‘kikulacho ki nguoni mwako’ kwa mujibu
wa hadithi hii?
3. Je, unafikiri Sungura alifanya kazi gani gerezani?
4. Taja tashbihi nne za tabia zilizotumika katika hadithi hii.
20
Sehemu C
Matumizi ya Lugha
Soma kifungu kinachofuata. Kina nafasi 1 hadi 5.
Umepewa majibu hapo. Chagua jibu lifaalo zaidi kati
ya yale uliyopewa ili kujaza nafasi.
Ni marufuku ___1___ maleba kwa kutumia ngozi ___2___
wanyama pori wakati wa sherehe za kitamaduni. Mtu yeyote
ambaye ___3___ na ngozi ya mnyama wa pori hana budi
kushtakiwa. Wanyamapori ___4___ haki ya kuishi huru. Ni
kinyume na sheria za nchi ___5__ pia kufuga mnyamapori
pasipo na kibali maalum. Ni muhimu tuwalinde na kuwahifadhi
wanyamapori ili tufaidike.
1. a. kutengenezana b. kutengenezeka
c. kutengeza d. kutengezwa
2. a. ya b. za
c. la d. wa
3. a. anayepatwa b. anayepatiwa
c. hupatiana d. hupatikana
4. a. yana b. ana c. wana d. una
5. a. chetu b. yetu c. letu d. wetu
Sehemu ya D
Kuandika
Umegundua kuwa kuna watoto katika mazingira yako
wanaofanya kazi ngumu kwa sababu ya mila zao.Andika insha
ya masimulizi isiyopungua maneno 150 kuonyesha hasara ya
kuwafanyisha watoto kazi ngumu. Msomee rafiki yako insha
yako ili akupe maoni yake.
21
Akili ni Mali
22
Bi. Faraja aliingia darasani akiwa amevaa tabasamu usoni.
Wanafunzi walijua kuwa kuna jambo zuri alilotaka kuwajuza.
“Nimewaletea habari njema, alisema na kutabasamu zaidi.
“Wizara ya viwanda imetangaza shindano. Wizara hiyo
inawataka wanafunzi wote wa Gredi ya Tano katika kaunti hii
kushiriki. Shindano hili ni la kipekee. Kila mwanafunzi atakuwa
mshindi iwapo atashiriki.Wizara imewaomba walimu wa Gredi
ya Tano kuwahimiza wanafunzi kushiriki katika shindano hili
kwa kikoa, Bi. Faraja alitua.
“Shindano ni la nini, mwalimu?” Gelo aliuliza akiwa ameinua
mkono.
“Kaunti inataka kuwekeza kwenye sekta ya viwanda. Imeamua
kutumia wanafunzi kupata pendekezo la mradi ambao
wanaweza kuuwekezea. Jukumu lako kama mwanafunzi ni
kuungana na wenzako wasiozidi wanne na kuandaa pendekezo
la mradi wenu. Pendekezo lenu litahitaji kielelezo kidogo.
Utahitaji pia maelezo ya kuonyesha jinsi ambavyo mradi wenu
utaweza kuwafaidi vijana iwapo utatekelezwa katika kaunti
yetu, Bi. Faraja aliendelea kufafanua.
“Kielelezo kinahitaji malighafi. Je, tutatoa wapi vitu vya
kutumia ili kutayarisha vielelezo vyetu?” Sela aliuliza.
“Hilo ni swali zuri sana na pia suala nyeti katika mfumo huu
wetu wa elimu. Wizara ya viwanda imehimiza na kusisitiza
kuwa malighafi ya kutayarisha kielelezo cha miradi yenu
yatoke katika mazingira yenu.Yaani, vitu mtakavyotumia viwe
ni vile vinavyopatikana katika mazingira yenu bila kununua.
Mfano mzuri ni karatasi ambazo zimekwisha kutumiwa ambazo
zinaweza kurudishwa tena mitamboni na kuunda bidhaa
mpya tofauti tofauti. Wizara imetoa onyo kali kwa yeyote
atakayetumia shindano hili kumgharimu mzazi. Sitaki kusikia
23
kuwa mmewaambia wazazi wenu wawanunulie vitu vya kutumia
katika mradi wenu.Akili ni mali.Tumieni akili na ubunifu wenu.
Wizara inataka kulea kizazi cha watu ambao watajitegemea
kiuchumi katika siku za usoni. Inataka muanze kufikiria namna
ya kuanzisha viwanda na kuviendeleza mkiwa wadogo. Mazoea
ni tabia. Tunasema ‘samaki hukunjwa akiwa mbichi’ eti!” Bi.
Faraja alielezea zaidi.
“Asante mwalimu kwa maelezo hayo. Mimi nafikiria
kupendekeza mradi wa kutumia mabaki ya maganda ya
matunda ili kutengeneza mbolea. Maganda hayo yanapatikana
katika soko letu bila malipo.Tukitumia maganda hayo tutakuwa
tunatengeneza mbolea na kusafisha soko kwa wakati mmoja,
Sela alisema kwa bashasha.
“Hilo ni wazo zuri, Sela. Najua mtaliboresha wazo hilo katika
kikundi chenu ili kielelezo chenu kifane. Narudia kuwa kila
mwanafunzi atakayeshiriki katika shindano hili ni mshindi na
atatuzwa kwa kushiriki.Wizara imesema kuwa itatuza jitihada.
Nawaomba mshirikiane katika makundi yenu ili kila mtu atoe
mchango wake, Bi. Faraja alisema.
“Je, tumepewa muda gani wa kutayarisha kielelezo hicho?”
Gelo aliuliza.
“Mwezi mzima. Maelezo zaidi yako kwenye tovuti ya wizara
hiyo mtandaoni. Nitawapeleka kwenye maabara yetu ya
tarakilishi ili mjisomee maelezo wenyewe. Haya, mnaweza
kujadiliana kuhusu mapendekezo ya miradi yenu, Bi. Faraja
aliwaambia wanafunzi.
Wanafunzi walijigawa katika makundi na kuanza majadialiano
mara moja. Kila mwanafunzi alipata kundi isipokuwa Fadhila,
aliyeishia kuzunguka na kitimaguru chake darasani. Kila
kundi lilimkataa.
24
25
“Kwa nini huna kundi, Fadhila? Si ujiunge na kundi la kina Sela.
Naona ni watatu, alipendekeza Bi. Faraja.
Fadhila alipokaribia kundi la Sela hakuamini aliyoambiwa,
“Tumetosha. Hatutaki mtu mwingine. Mradi wetu utahitaji
matumizi ya viungo vya mwili. Hatutaki usumbuke, tafuta kundi
jingine, alisema Sela huku akimtupia Fadhila mkono.
“Lakini nitawafaa kwa mawazo. Naomba nijiunge nanyi.
Nitafanya kazi yoyote mtakayonipatia. Mwalimu amesema…”
Fadhila alijaribu kujieleza kwa unyenyekevu.
“Amesema nini? Huwezi kujilazimisha katika kundi letu. Mwalimu
mwenyewe alisema kuwa tujichagulie makundi wenyewe.
Acha kudanganya.Tutakuhitaji wakati wa kundi la Hisabati
na Kiswahili kwa kuwa wewe ni gwiji, lakini hapa hutatufaa.
Tafadhali tuelewe, Sela alimwambia Fadhila kwa ukakamavu.
Wakati wa mapumziko ya mchana Fadhila alikaa pembeni peke
yake.Aliwaza kuhusu matukio ya darasani siku hiyo. Hakuamini
namna ambavyo wanafunzi wenzake walivyomtema
alipowahitaji.
“Hata Gelo hakutaka nijiunge na kundi lao! Ama kweli marafiki
wanafiki ni hatari sana, Fadhila alijisemea huku akidondokwa
na machozi.
Bi. Faraja aligundua kuwa Fadhila alikuwa akilia. Alikwenda
mara moja kumdadisi,“Una nini Fadhila? Unaumwa?”
“Sina neno. Siumwi, mwalimu, Fadhila alisema huku akifuta
machozi haraka.
“Kama kuna jambo linalokusumbua usisite kuniambia, Bi.
Faraja alisema.
26
“Sina kundi. Wenzangu darasani hawanitaki. Wanasema
sitaweza kuwafaa kwenye mradi, Fadhila alisema huku akilia
kwikwikwi.
“Usitie shaka, Fadhila. Pangusa machozi. Kama nilivyosema
akili ni mali. Mradi huu unahitaji akili zaidi ya nguvu za mwili.
Wazia mradi wako peke yako. Nitakuelekeza ili nawe uweze
kushiriki, Bi. Faraja alimwelezea Fadhilla kwa makini.
Kuanzia siku hiyo, Fadhila alipata nguvu mpya. Hakikisho la
Bi. Faraja kuwa angemwelekeza lilimtia moyo. Hakujihusisha
tena na miradi ya wenzake darasani bali aliwazia mradi wake.
“Mwalimu, nimepata wazo la mradi wangu. Nafikiria kuwa
matumizi ya magamba na matawi ya ndizi kutengenezea
vikapu, magunia na karatasi ni wazo zuri, alisema Fadhila
kwa ujasiri.
“Hilo ni wazo zito sana. Manufaa ya mradi huo ni makubwa na
mengi.Tukipata malighafi mbadala ya kutengenezea karatasi
tutaokoa miti na kuimarisha mazingira yetu. Naona uanze mara
moja kufanya utafiti zaidi na kutayarisha kielelezo chako, Bi.
Faraja alisema kwa furaha.
“Naomba uniruhusu kutumia tarakilishi kwenye maabara
kufanya utafiti zaidi, Fadhila alimsihi Bi. Faraja.
“Bila shaka una ruhusa. Wakati wa jioni nitakuwa huko
maabarani. Njoo usakure na kupata maarifa zaidi. Naipenda
hekima yako ya kuutumia mtandao ili kujinufaisha. Inasikitisha
jinsi ambavyo watoto wengi wanavyotumia mtandao
kujizubaisha tu. Tunahitaji pia wavumbuzi si tu watumizi wa
huduma za mtandaoni, Bi. Faraja alisema.
Kauli za Bi. Faraja zilimpa Fadhila matumaini. Alianza mradi
wake mara moja. Aliandika yote aliyotaka kuwasilisha kwa
27
kuyapiga chapa kwenye tarakilishi.Wasilisho lake lilipendeza
ajabu baada ya kulitia picha.
“Sasa kazi iliyobaki ni ya kuandaa kielelezo halisi. Nahitaji
kinu na mchi, magamba na matawi ya ndizi, gundi, mti wa
kukandia chapati, Fadhila alijisemea.
Alasiri ya siku hiyo mwanafunzi mpya aliwasili hapo darasani.
“Tumepata mgeni ambaye kuanzia leo atakuwa mwenzetu.
Nawaomba tumkaribishe kwa makofi kisha aseme jina lake.
Baadaye tumwelezee kuhusu yale tuliyojifunza darasani
na tumwalike kwenye mradi wetu unaoendelea, Bi.Faraja
alitangaza.
“Asante mwalimu kwa makaribisho. Ninaitwa Bela, Bela
alijitambulisha kwa ukakamavu.Alipewa muda wa kuangalia
miradi ya makundi tofauti na kuchagua kundi la kujiunga nalo.
Baada ya siku mbili, Bela alimsalimu Fadhila na kumwomba
ajiunge naye kwenye mradi. Fadhila hakuamini.Alishtuka sana.
“Makundi yote yalinikataa ndio maana nafanya mradi peke
yangu. Siamini kuwa unataka kujiunga nami, Fadhila alisema
kwa mshangao.
“Kwanza nimeipenda tabia yako. Una uvumilivu, umakinifu na
ujasiri. Pili, katika shule niliyotoka wanafunzi hawabaguani kwa
misingi yoyote ile. Mwalimu wetu alituambia kuwa ulemavu
wa mwili si hoja. Alisema kuwa yule ambaye anawabagua
walemavu wa mwili yeye mwenyewe ni mlemavu wa akili,
Bela alisema na kucheka.
“Kweli kabisa!” Fadhila alisema na kuangua kicheko.
“Mwalimu wetu wa darasa huko alitufunza kuwa kila mtu
ana haki ya kuhusiana na wengine.Tatu, nimeupenda mradi
wako. Ni mradi ambao unaweza kufanywa katika mazingira
28
yetu bila gharama yoyote. Mradi wenyewe uliupata vipi?” Bela
alimuuliza fadhila.
“Bi. Faraja alituambia kuwa akili ni mali. Ni kweli kabisa.
Nilijiuliza ni kwa nini tutumie ukonge kutengeneza magunia,
vikapu na nyuzi za kujengea na tusiweze kutumia migomba?
Kisha niliingia mtandaoni na kugundua kuwa pia kwa kutumia
magamba na matawi ya ndizi tunaweza hata kutengeneza
karatasi, Fadhila alisema kwa tabasamu.
“Tutafanya nini hasa ili tuweze kutengeneza bidhaa zetu za
kielelezo cha mradi?” Bela aliuliza.
“Kwa ajili ya mahitaji ya kielelezo chetu tutatumia magamba
ya ndizi. Baada ya ndizi kuvunwa, yaani kukatwa, mti wa ndizi
hubakia ukiwa mzima. Magamba yake huwa bado ni mabichi.
Tutakata magamba hayo katika vipande tunavyotaka kisha
tuyatie ndani ya kinu. Tutayaponda magamba hayo kwa
mchi. Tunaweza kuongezea gundi aina yoyote ile tukitaka.
Magamba yakilainika tutayaweka kwenye meza. Hapo mezani
tutatandaza kwa kutumia mti wa kukandia chapati ili yanyooke.
Yakikauka tayari tutakuwa na malighafi ya kutengenezea
bidhaa mbalimbali kwa magamba ya ndizi. Mradi huu ukiwa
kiwandani haya yote yatafanyika kwa urahisi zaidi kwa kutumia
mitambo, Fadhila alijieleza kwa ufasaha.
29
30
Wanafunzi walifanya kazi zao kwa bidii. Kila kikundi kilionekana
kufanikiwa katika mradi wake. Bi. Faraja alipendezwa sana
na jitihada za wanafunzi wake.Aliwaambia,“Jitihada huvuta
heri. Nawahongera kwa hatua ambazo tayari mmepiga katika
miradi yenu.
Fadhila na Bela walipata kile walichohitaji bila usumbufu
wowote. Migomba ilikuwa imetapakaa kila mahali katika
kaunti yao. Ndizi zilikuwa ndicho chakula chao cha kila siku.
Hawakwenda mbali kutafuta magamba ya ndizi. Hapo shuleni
palikuwa na ndizi za kutosha na zilipokomaa na kukatwa tu,
walipata malighafi ya mradi wao.
Siku ya vielelezo vya miradi kukaguliwa ilikuwa imekaribia.
Kila kundi lilikuwa na matumaini makubwa kupata tuzo yao.
Wanafunzi walisikika wakibashiri tuzo yenyewe.
“Pengine tutapewa vitabu vya hadithi, alisema Gelo.
“Hata pengine tutaletewa sare za michezo, alisema Sela.
“Nafikiri tupewa vipakatalishi, Bela alisema.
“Nilisema kila mtu ni mshindi na atapata kitu. Chochote
utakachopewa pokea kwa moyo mkunjufu. Jambo muhimu ni
kuwa mtajifunza jambo kutokana na mradi huu, Bi. Faraja
aliwakumbusha wanafunzi wake.
Siku hiyo ya siku ilisubiriwa na wanafunzi kwa hamu na ghamu.
Kila kikundi kilikuwa kimekamilisha kielelezo cha mradi wao.
Wanafunzi wote walivaa sare safi. Walionekana nadhifu
kweli. Kila kikundi kilitakiwa kuwasilisha maelezo ya mradi
mbele ya wakaguzi. Baadaye wangewaonyesha wakaguzi
hao kielelezo chenyewe.Vikundi tofauti vilichagua njia tofauti
za kuwasilisha maelezo yao. Sela na kikundi chake walichora
chati kuelezea hatua za kutengeneza mbolea kwa kutumia
31
maganda ya matunda. Gelo na kikundi chake waliigiza namna
ya kutumia chupa za plastiki kujengea kuta za nyumba. Fadhila
ana Bela walitumia projekta kuelezea mradi ambao walikuwa
wanapendekeza. Walionyesha picha na video walizochukua
kwa ruhusa ya mwalimu wao kuanzia mwanzo wa mradi
hadi mwisho.Wakaguzi walipendezwa sana na wasilisho lao.
Wanafunzi wa Gredi ya Tano waliongozwa na Bi. Faraja na
kuandamana hadi kwenye vielelezo vya miradi yao. Kila kundi
lilisimama kando ya mradi wao.Waliwaelezea wakaguzi wazo
la mradi wao hatua kwa hatua.
Wakati wa maswali ulifika na kila mtu akawa huru kuuliza.
“Nimeupenda mradi wenu wa kutengeneza karatasi na bidhaa
nyingine kwa kutumia magamba ya ndizi. Je, iwapo wizara yetu
itateua mradi wenu na kuwekeza mnafikiri vijana wa kaunti
hii watanufaika vipi?” aliuliza mkaguzi mmoja.
Fadhila aliinua mkono mara moja na kujibu.
“Asante sana kwa swali hilo. Kwanza kabisa vijana watapata
ajira. Pili, mradi huu utawahimiza vijana kurudi mashambani
ili walime na kupanda ndizi zaida. Mwalimu wetu alituambia
kuwa mtu akionja asali hutaka kuchonga mzinga. Bora tu
vijana waonje faida za mradi wenyewe.
Fadhila alipigiwa makofi na kila mtu.
“Mwalimu wenu amewafunza mambo mazuri. Je, mwenzako
naye analo la kusema?” aliuliza mkaguzi mwingine.
“Asante sana. Mradi wetu utafanya chakula kuongezeka katika
kaunti yetu. Kama tunavyojua kaunti yetu tayari inaongoza
kwa ukulima wa ndizi. Huwezi kupata magamba ya ndizi kabla
ya kukata mkungu uliokomaa. Bila shaka mauzo ya ndizi katika
kaunti yetu yataongezeka na kuimarisha uchumi wetu, Bela
32
alielezea kwa utaratibu.
Bela pia naye alipigiwa makofi na kushangiliwa na wakaguzi,
walimu na wanafunzi wenzake.
Zamu ya kikundi cha Sela ya kuulizwa maswali ilifika.
“Mradi wenu wavutia ili nina swali moja tu. Je, mnafikiri tutapata
wapi chupa za kutosha za kujengea nyumba zote katika kaunti
yetu?” mkaguzi mmoja aliwauliza kina Sela.
Sela na kundi lake walinyamaza kimya kama maji mtungini.
“Pia nami nina swali.Tunanuia kupiga marufuku matumizi ya
chupa za plastiki katika kaunti yetu. Je, mradi wenu utaweza
kuendelea baada ya hapo?” mkaguzi mwingine aliuliza. Kundi
zima lilinyamaza.
Kundi la Gelo liliulizwa swali moja. Gelo alilijibu bila kumakinika.
“Je, unafikiri maganda ya matunda yanaweza kutengeneza
mbolea ya kutosha ya kukidhi mahitaji ya wakulima katika
kaunti hii?”
“Sina hakika. Lakini nafikiri kila mtu akiongeza idadi ya
matunda anayokula kila siku tutaweza, Gelo alipojibu kila
mtu aliangua kicheko.
Wakaguzi waliondoka na kuahidi kuwasiliana na mwalimu
kuhusu zawadi za makundi yote. Bi. Faraja aliwapongeza
Fadhila na Bela kwa ukakamavu wao wa kujibu maswali.
Alisema, “Nawaonea fahari kubwa, Fadhila na Bela. Heko!
Mmedhihirisha kuwa mlikuwa mmefanya utafiti wa kutosha
kuhusu mradi wenu.
Siku moja asubuhi, kabla ya masomo kuanza, Bi. Faraja aliwaita
Fadhila na Bela ofisini mwake. Bela alimsaidia Fadhila kusukuma
33
kitimaguru chake hadi huko ofisini. Walipofika walipewa
habari njema, “Nina furaha isiyo na kifani. Hongera kwenu.
Mradi wenu umechaguliwa na mwekezaji mmoja wa kaunti
yetu. Kwa usaidizi wa wizara ya viwanda atafungua kiwanda
cha kutengeneza karatasi na bidhaa nyinginezo kwa kutumia
magamba na matawi ya ndizi.Ameomba tumtumie wasilisho
lenu kwa njia ya kidijitali ili alidadisi zaidi. Ameomba pia
mkikubaliwa na wazazi au walezi wenu wakiridhia, niwapeleke
mkahojiwe kwenye kituo cha televisheni ya kitaifa.
Habari za kuteuliwa kwa mradi wa Fadhila ana Bela zilisambaa
haraka shuleni na kwingineko. Baada ya siku chache watoto
hawa pia walianza kuzungumziwa kwenye mitandao ya kijamii.
Ijapokuwa picha zao hazikuwepo tayari watu wengi walikuwa
wamefahamishwa kuwa Fadhila alikuwa na ulemavu wa miguu.
Baadhi ya kauli mitandaoni zilikuwa hivi;
‘Ulemavu si hoja. Mungu ambariki mtoto huyo azidi kuifaa
jamii yetu’
‘Mtoto huyu anahitaji kufanyiwa uchunguzi. Pengine miguu
yake bado inaweza kutembea. Wadau, tumeni picha tuzione.
Teknolojia ya tiba imepiga hatua. Palipo na nia pana njia.
Madaktari mko wapi?’
Siku ya kwenda kwenye kituo cha habari ilisubiriwa na wengi
kwa hisia mseto. Kuna wale waliofurahia kuwa wangewaona
Fadhila na Bela. Kuna wengine waliotaka kujigamba kwamba
wanawafahamu Fadhila na Bela.Wanafunzi wa Gredi yaTano
waliona fahari kubwa kwamba wenzao wangeonekana kwenye
runinga.Almradi kila mmoja wao angefurahi kuwaona watoto
hao kwenye kiwambo cha runinga.
Hayawi hayawi huwa. Siku ilifika. Fadhila na Bela walifika
studioni na kuhojiwa. Bi. Faraja pia alihojiwa. Mahojiano
yalipokamilika mwekezaji aliyependezwa na mradi wa Fadhila
34
na Bela naye alikaribishwa studioni.Aliwapongeza wanafunzi
hao na kuwahimiza kuendelea na bidii katika kubuni na
kuvumbua maarifa ambayo yataifaidi jamii yao.
“Nawapa hongera zangu, Fadhila na Bela. Mradi mliowasilisha
utawezesha maendeleo endelevu. Utafaidi vizazi vingi
vijavyo katika jimbo letu. Nimemletea Fadhila zawadi ya kiti
cha kisasa cha kutembelea. Kiti hiki ni cha kieletroniki na
hatahitaji kutumia nguvu kujisukuma au kusukumwa na mtu
mwingine. Kiti hiki pia kinakuja na kipakatalishi chake ambacho
unaweza kukitenganisha ukitaka. Nawe Bela nimekuletea
kipakatalishi. Sasa mnataweza kufanya utafiti mtandaoni kwa
wepesi. Tafadhali tumieni vifaa hivi kwa njia nzuri ili viwape
faida. Tumieni vifaa hivi wakati ufaao kwa mwongozo wa
mwalimu au wazazi na walezi wenu. Kampuni yangu imejitolea
pia kugharamia uchunguzi wa hali ya Fadhila. Iwapo Fadhila
anaweza kupata matibabu na kurudia hali ya kawaida itakuwa
fahari yangu kugharamia kila kitu, alitangaza mwekezaji
akiwa kwenye runinga.
Fadhila na Bela walibubujikwa na machozi ya furaha. Hata
mwanahabari alikuwa akiwahoji macho yake yalitona mchozi
akayapangusa.
35
36
Wakaguzi wa miradi walirudi shuleni baada ya wiki moja
kuwapelekea watoto zawadi zao.Walileta vitabu vya hadithi,
tarakilishi, mipira ya kuchezea na miche ya kupanda.Wanafunzi
walifurahia zawadi zao na kuwashukuru wageni wao.Walikariri
mashairi waliyokuwa wametayarisha kwa msaada wa Bi.
Faraja.
“Nimefurahishwa na mashairi yenu kuhusu uwekezaji na utunzaji
wa mazingira. Huwezi kutenganisha masuala haya mawili. Ili
jimbo letu lipate ufanisi tunahitaji kuhakikisha kuwa uwekezaji
hasa kwa njia ya viwanda huyachafui mazingira yetu. Upanzi
wa miti, utunzaji wa vianzo vya mito ni jukumu la kila mmoja
wetu. Napendekeza kuwa ule mradi wa kufanya maganda
ya matunda mbolea utiliwe mkazo kama njia mojawapo ya
utunzaji wa mazingira. Mradi wa kutumia chupa za plastiki
kujengea pia ni mbinu nyingine ya kuhakikisha kuwa chupa
hizi hazitupwi ovyoovyo na kuharibu mazingira. Napendekeza
ufundi huo utumike hasa kwenye majengo kama vile ya vibanda
vya kuku na sungura. Ikumbukeni kauli ya mwalimu wenu kuwa
akili ni mali, alihutubia mmoja wa wakaguzi.Watu walimpigia
makofi kama ishara ya kukubaliana naye.
Hotuba ilipokwisha, Gelo na Sela walimwita Fadhila kando.
Fadhila alikwenda mara moja kwa msaada wa kiti chake kipya.
“Tunaomba utusamehe, Fadhila. Tulikubagua, alisema Gelo
kwa upole.
“Tusamehe, hatutarudia.Ahadi ni deni, tumekuahidi.Tunaomba
tuwe marafiki zako tena.Tufanye miradi pamoja na tucheze
nawe, Sela alisema huku akilengwalengwa na machozi.
“Niliwasamehe zamani. Bi. Faraja alisema kosa ni kurudia
kosa, alisema Fadhila.
“Asante!” Gelo na Sela walisema kwa pamoja huku wakimpa
Fadhila mkono kama ishara ya mapatano.
37
Kamusi Yangu
kikoa kufanya kazi au mambo kwa pamoja
sekta sehemu ya kitu kilichogawanywa
malighafi kitu chochote ambacho kinatumika
katika utengezaji wa bidhaa
kielelezo mfano
kumgharimu kumfanya mtu atoe pesa fulani za
kununua kitu
tovuti mkusanyiko wa kurasa zilizoandikwa
kwa lugha mbalimbali za tarakilishi
ambazo kwa pamoja hujumuika katika
kutoa habari au maelezo kuhusu jambo
fulani
gwiji mtu hodari katika kufanya jambo fulani
walivyomtema walivyomkana
wanafiki watu ambao si wakweli; wasioaminika
alimsihi alimwomba
kinu na mchi ni vifaa vya kiasili vinavyotumiwa kwa
pamoja kupondea nafaka kama vile
mahindi
wakibashiri wakisema kitakachofanyika katika siku
za usoni
wakiridhia wakikubali
wadau wahusika katika shughuli fulani
maendeleo
endelevu ni ukuaji wa viwango vya ufanisi wa
binadamu na uboreshaji wa maisha bila
kuathiri mazingira
38
Maswali
1. Bi. Faraja aliwaletea wanafunzi habari gani?
2. Wanafunzi walipaswa kupata malighafi ya kielelezo cha
mradi wao wapi?
3. Toa sababu ambazo ziliwafanya wanafunzi kutomkaribisha
Fadhila kwenye vikundi vyao.
4. Mradi wa Sela ulikuwa na upungufu upi?
5. Je, ni kwa nini mradi wa Gelo haungeweza kuwasaidia
vijana kuwa na maendeleo endelevu?
6. Mradi wa Fadhila na Bela ungesaidia vipi uchumi wa jimbo
lao?
7. Zawadi ambazo wanafunzi walipewa zilikuwa na manufaa
gani kwao?
8. Je, kwa nini ni muhimu kwa wawekezaji kuwazia suala la
usafi wa mazingira kila wanapoanzisha miradi kwenye
viwanda?
9. Umejifunza nini kutokana na hadithi hii?
10.Je, msamaha una umuhimu gani kwa wanajamii?
39
Mazoezi
Sehemu ya A
Kusikiliza na Kuzungumza
a. Ukiwa na rafiki yako, zungumzeni kuhusu namna ambavyo
mnaweza kuwekeza. Maswali haya yatawaongoza:
i. Je, ni mradi gani ambao mnaweza kuanzisha ili
kuwekeza?
ii. Mnaweza kupanua mradi huo wenu kwa njia gani?
iii. Mnaweza kutumia mbinu gani kuwaalika wawekezaji
kujiunga nanyi katika mradi wenu?
b. Uwekezaji wenu utaifaidi vipi jamii yenu?
c. Mwombe rafiki yako akusomee kurasa zozote tatu za hadithi
hii. Mwambie akuulize maswali yoyote manne kutokana na
kurasa hizo.
d. Msomee rafiki yako ukurasa mmoja wa hadithi hii. Mwombe
akuhesabie idadi ya maneno ambayo unaweza kusoma kwa
ufasaha kwa dakika moja. Rafiki anaweza kuwa mwenzako
darasani.
Sehemu B
Ufahamu wa Kusoma
Jibu maswali haya.
1. Eleza jinsi ambavyo unaweza kutengeneza karatasi kwa
magamba ya ndizi kwa mujibu wa hadithi.
2. Kwa nini Bela alipendelea kufanya kazi na Fadhila?
3. Pendekeza mambo ambayo Bi. Faraja anaweza kufanya ili
kukomesha ubaguzi miongoni mwa wanafunzi wake.
4. Eleza maana ya methali zote zilizotumiwa kwenye hadithi.
40
Sehemu C
Matumizi ya Lugha
Ni jambo __1__ busara kuwekeza. Mtu anaweza kuwekeza
akiwa peke yake au __2__ na wenzake katika __3__cha watu.
Watu wengine huwekeza kwa kuanzisha miradi ya kibiashara
ambayo huwaletea faida. Ijapokuwa panda __4__ za dunia ni
nyingi ni vyema kutafuta mtaji na kuwekeza. __5__. Ni muhimu
kuhangaika tukitafuata riziki.
1. a. ya b. wa
c. la d. za
2. a. akaunga b. akaungisha
c. akaungika d. akaungana
3. a. kikosi b. kikundi
c. kilinge d. kikoa
4. a. shuka b. nenda
c. rudi d. kwea
5. a. Mgaagaa na upwa hali wali mkavu
b.Aliye juu mngoje chini
c. Mwenye shibe hamjui mwenye njaa
d. Ukiona vyaelea jua vimeundwa
Sehemu ya D
Kuandika
Unataka kuanzisha mradi wa kufuga sungura ili ujipatie
mapato.Andika baruapepe kwa rafiki yako isiyozidi maneno
150 ukimwomba ajiunge nawe kwenye mradi huo. Msomee
rafiki yako insha yako ili akupe maoni yake.
41
Tamara Tamashani
42
Tamara alijitayarisha vilivyo kwa ajili ya tamasha ya muziki.
Kila siku alifanya mazoezi akiwa nyumbani na pia shuleni.
“Jitihada huvuta heri. Shairi lako litafana bila shaka. Nimekusikia
ukilikariri kutoka huko nje. Umelishika kweli, mama yake
Tamara alimwambia kwa furaha.
“Hata nami nimeisikia sauti iliyo kama ya ninga nikiwa huko
barazani. Shairi lenyewe ni zuri na mwenye kulikariri naye
amelimudu kweli. Nafikiri unaweza kulikariri hata ndotoni.
Bila shaka utanyakua ushindi. Nakutakia kila la heri siku hiyo
ya tamasha, alisema baba yake Tamara kwa tabasamu kuu.
“Asanteni sana. Najitahidi ili nifaidi. Ijapokuwa mwalimu wetu
alituambia kuwa kila mshiriki ni mshindi kwenye tamasha
hiyo, nataka niwe bora zaidi. Nataka kuikuza talanta yangu
ya usanii wa jukwaani, alisema Tamara kwa bashasha.
Shuleni, mwalimu wake, Bwana Jasiri, alimwelekeza na
kumhimiza Tamara kila uchao.
“Kombe la ushindi kwenye kitengo hiki cha shairi la kujitungia
ni lako. Unakariri shairi hili kwa kuzingatia ishara mwafaka za
mwili na uso. Umekuwa malenga haswa. Kinolewacho kumbe
hupata, Bwana Jasiri alimwambia Tamara siku moja baada
ya mazoezi yake ya kukariri shairi.
“Nikipata kombe halitakuwa langu bali letu. Ushindi utakuwa
wetu sote. Mimi, nyinyi walimu na wanafunzi wenzangu.
Nyote mmenishika mkono na kunitia shime tangu tamasha
hii kutangazwa.Asanteni sana, Tamara alisema kwa upole.
“Ushindi ni wetu sote kwa hakika ila umetuwakilisha vilivyo
kuanzia mwanzo wa tamasha hii.Tia bidii zaidi ili uchaguliwe
kuipeperusha bendera yetu kwenye kiwango cha Jumuiya ya
Afrika Mashariki, alisema Bwana Jasiri.
43
Tamara aliufuata ushauri wa wote waliomwelekeza.Alilikariri
shairi lake kwa ufundi mkubwa. Kila aliyemsikiliza alimwambia
kuwa angefanikiwa.
“Asiyekubali kushindwa si mshindani. Hata nisiposhinda kombe
hili, bado nitakuwa nimeafikia lengo langu.Azma yangu hasa
ilikuwa ni kuunoa uwezo wangu wa kutunga na kulikariri,
Tamara angesema.
Siku iliyosubiriwa na wengi ilifika.Tamara na wenzake walifika
mapema ili kushiriki kwenye tamasha hilo.Walisafiri kwa basi
la shule yao. Shule yao ilikuwa imewasajili washiriki katika
vitengo tofauti vya tamasha hiyo.
Zamu ya Tamara kupanda jukwaani iliwadia. Alipanda kwa
kishindo.Alisindikizwa na wenzake kwa vigelegele na nderemo.
Alianza wasilisho lake,“Wakaguzi, wageni waalikwa, walimu
na wanafunzi wenzangu. Mbele yenu ni mwanafunzi wa shule
ya msingi ya …”Tamara alisita ghafla.Alikauka kama sanamu.
Watu walishangaa.Wanafunzi wenzake walimaka. Hawakuamini
kuwa Tamara alikuwa amenyamaza kama ambaye alikuwa
amezimwa kwa swichi. Mwalimu wake, Bwana Jasiri, alitingisha
kichwa kwa masikitiko.
Tamara alianza kububujikwa na machozi. Baadhi ya wanafunzi
wa shule yake pia walianza kulia kilio cha chini kwa chini.
Tamara alijaribu kufungua kinywa lakini hakuweza kusema
lolote la maana. Aligugumiza tu.
44
45
“Sa…sama…ha…” alisema huku akilia jukwaani.
Mwalimu wake, Bwana Jasiri, alisimama na kumwangalia
Tamara na kumpa ishara ambayo alizoea kumpa wakati wa
mazoezi. Tamara aligutuka kama ambaye ametoka kwenye
ruya mbaya. Alipangusa machozi na kuanza kutokwa na
maneno kama chiriku.
“Samahani sana kwa hilo. Samahani sana kwa kuwapotezea
muda. Najua ratiba yenu imepangwa kwa kuhesabiwa dakika.
Nawaomba niwaelezee sababu za kusita kwangu. Nawaomba
niseme ukweli. Nimemwona mwalimu wangu wa utotoni
kwenye hadhira hii. Bi.Azuri alinifunza kuanzia Gredi ya Kwanza
hadi Gredi ya Tatu kabla wazazi wangu kupata uhamisho nami
nikabadilisha shule. Nimekumbuka kauli zake ‘sema ukweli
ukuweke huru’.Asante sana, Bi.Azuri. Kauli zako hizo zimenilea
na kuniokoa kila mara ninapokumbana na hali hii. Mwalimu
wangu, Bwana Jasiri, asante. Mafunzo yako wakati wa mazoezi
yangu ya kukariri shairi hili yananiwezesha sasa kuikabili
hadhira hii. Uliniambia nisiangalie watu nyusoni mwao iwapo
nafikiri woga umeniingia. Nilipopanda jukwaani sikuwa na
woga wowote.Aliye na kovu usidhani kapona.Woga umeniingia
nilipomwona mwanafunzi mwenzangu aliyenitesa sana kwa
ajili ya hali yangu ya kimaumbile. Kesi Mtoro, nisamehe kwa
kuyazungumzia haya hapa hadharani.
Nilizaliwa na mdomo uliopinda. Huo haukuwa ugonjwa wa
kunywewa dawa lakini ni hali iliyohitaji tiba kwa njia ya
upasuaji.Watoto na wanafunzi wengine walinicheka kwa kuwa
nilisema vibaya. Walimu walijaribu wawezavyo kuwakanya
na hata wakati mwingine kuwaadhibu ili wasinitese.Walimu
wangu waliweza tu kunilinda nikiwa darasani au karibu nao.
Nikiwa uwanjani watoto wangenichokoza ili niseme wacheke.
Kwa sababu ya hilo niliishia kubaki kivyangu ili nisisumbuliwe.
Nakumbuka kwa uzito wa moyo kisa kimoja kilichotokea
46
siku moja. Kisa hicho kilinitisha sana. Sikumwambia mtu
yeyote siku hiyo. Nimeamua kukisema ili nijiweke huru. Mtoro
alinitesa sana siku hiyo.Tulikuwa wa kwanza kuingia darasani.
Tulimwona jongoo akitambalia ukutani. Lazima aliingia kupitia
kwenye dirisha. Mtoro alimchukua jongoo huyo kwa rula yake.
Alifungua begi langu na kumtia jongoo huyo humo ndani huku
akicheka. Nilishtuka kama ambaye nilikuwa nimekutana na
ibilisi mwenyewe. Nilitamani kumwomba asiniadhibu bila ya
kosa lakini kinywa kilinisaliti. Nilishinda nimejikunyata siku
nzima. Bi.Azuri aliponidadisi sikusema kitu.
Tangu siku hiyo nilishikwa na kigugumizi nisichokilalia wala
kukiamkia. Tuseme nilikumbwa na ugonjwa wa kisaikolojia.
Sikufungua begi langu la shule siku hiyo. Sikulibeba begi langu
la shule siku hiyo saa za kwenda nyumbani. Sijaliona tangu
siku hiyo. Je, Mtoro, ulilichukua begi langu? Nilipofika nyumbani
singeweza kusema kitu. Mama na baba walipogundua kuwa
sina begi langu waliniuliza. Nilisema baadaye kuwa lilikuwa
limepotea. Nafikiri hawakutaka kunisumbua. Walitambua
kuwa tayari hali yangu ilikuwa imeyafanya maisha yangu
kuwa magumu.Walininunulia tena kila kitu. Leo nilipomwona
Mtoro moyo wangu umeshtuka. Wazazi wangu na walimu
wangu, akiwemo Bi. Azuri walifanya mipango nikafanyiwa
upasuaji na kurekebishwa mdomo wangu wa juu. Leo nasema
vizuri bila tatizo. Asante tena, Bi. Azuri. Una moyo mzuri
ajabu. Wewe kwangu ni zaidi ya mwalimu, ni mlezi haswa.
Nilipomwona Mtoro leo kwenye hadhira moyo umenipapa.
Kumbe ijapokuwa tatizo la kimaumbile lilipona, bado naugua
kisaikolojia. Kama Bwana Jasiri hangesimama na kunipa ishara
singeweza kuendelea.Asante sana, Bwana Jasiri.
Leo nimesema ukweli. Nimejiweka huru. Natumai kuwa
nitapona ugonjwa huo wa kisaikolojia. Mtoro nimekusamehe
hata kama hujaniomba msamaha.Asanteni kwa kunisikiliza,
Tamara alimaliza kusema na kupangusa machozi ambayo
47
yalikuwa yanabubujika kama maji kwenye mfereji. Alishuka
kutoka kwenye jukwaani na kuelekea walikokuwa wameketi
wanafunzi wenzake. Huko walimkaribisha kama shujaa.
Masimulizi ya Tamara yaligusa nyoyo za wengi. Wakaguzi
walikubaliana kwa kauli moja kuwa Tamara alikariri shairi
alilokuwa ametunga kwa ajili ya tamasha hiyo.Tamara alirudi
tena jukwaani akishangiliwa na kila mtu, hata wakaguzi.
Alilikariri shairi lake kwa ujasiri mkubwa.Alitamka kila neno
kwa ufasaha. Mahadhi yake yalipendeza.
Kumbukumbu naandika, uwele nahadithia,
Miaka hadi mikaka, itasomwa historia,
Korona ililipuka, ikatingika dunia,
Makubwa yalitufika, hivi nayasimulia.
Korona ni jinamizi, janga lisilo mithili,
Halisikii mizizi, dawa na kinga ya mwili,
Huingia kama mwizi, kwa fujo bila kibali,
Kisha hukita mizizi, na kuzidisha makali.
Ilianza na uvumi, fununu na vijineno,
Watu walichonga ndimi, kueneza minong’ono,
Sikuyaamini mimi, yaliposemwa maneno,
Visa vilifika kumi, tukaonyeshwa mifano.
Walifunga mipakani, viwanja na bandarini,
Tulisalia nyumbani, hakuna kwenda shuleni,
Masomo mtandaoni, kazi ni mtandaoni,
Jirani hawaonani, hujambo hawapeani.
Tulivaa barakoa, kwa tabu tulipumua,
Ikawa kubwa hatia, kieuzi kususia,
Mikono tulisugua, sabuni tulitumia,
Virusi tuliviua, korona ilipungua.
48
49
Ukishikwa shikamana, mbinu nyingi tulibuni,
Tukawa twagoteana, mikono na miguuni,
Hatungekaribiana, tuingiapo garini,
Umbali kuwekeana, ikawa ndiyo kanuni.
Halafu madaktari, walifanya uvumbuzi,
Tulisikia habari, wamepata utatuzi,
Chanjo ilileta heri, kudhibiti jinamizi,
Walituepusha shari, asante kwa wauguzi.
Tamara alipomaliza kulikariri shairi watu wote walisimama.
Alipigiwa makofi na kushangiliwa kwa ajili ya uzuri wa wasilisho
lake. Mtoro alitoka mbio alikokuwa ameketi na kwenda
jukwaani. Alimpigia Tamara magoti na kumlilia kama mtoto
mdogo. Hakusema kitu.
“Nimekusamehe, Mtoro, alisema Tamara kwa tabasamu.
“Asante. Naomba tena na tena msamaha. Kosa nililokufanyia
ni kubwa sana. Halistahili msamaha. Limenikosesha amani
kwa muda mrefu. Begi lako bado ningali nalo kwetu. Naomba
kutafuta mbinu za kukurudishia. Kuanzia leo nitawaelimisha
wenzangu wasifanye kosa kama nililofanya. Mtu hachagui kuwa
kilema wala mgonjwa. Ni vibaya kuwatesa au kuwatenga watu
ambao tayari wanapambana na hali ngumu za kimaumbile au
wanaougua, alisema Mtoro kwa unyenyekevu.
Tamara alitangazwa mshindi miongoni mwa washindi wengine
mwishoni mwa tamasha hiyo. Kila mtu aliridhika na matokeo
hayo. Mmoja wa wakaguzi alikuwa na haya ya kusema kuhusu
kisa cha Tamara,“Nafurahi kuwa Tamara ametangazwa moja
wa washindi wa tamasha hii. Akiwa na wenzake nina imani
kuwa atatuwakilisha vyema katika kiwango cha jumuiya.
Tamara ni mfano mzuri wa watu ambao wameweza kujitolea
na kuzungumzia hali zao za kisaikolojia, na kujikomboa.Watu
wengine hufundika hali na magonjwa ya kisaikolojia nyoyoni
50
na kuishia kuathirika bila mtu yeyote kujua. Natoa wito kwa
watu wote hapa ambao wanahisi wana matatizo yoyote ya
kisaikolojia wajitokeze ili wasaidiwe. Magonjwa ya kisaikolojia
wakati mwingi hayana dalili zinazobainika wazi. Mgonjwa
huweza kupata msaada pale tu anapojitolea kuelezea hali
yake bila woga. Semeni ukweli ili muwe huru.
Watu wote walisimama na kumpigia makofi.
Siku ya washindi kwenda kwenye tamasha ya jumuiya ilifika.
Tamara alisindikizwa hadi shuleni na wazazi wake.Waliagana
na safari ikaanza.Walifika kwenye uwanja wa ndege mapema
ili wakutane na wanafunzi kutoka shule nyingine. Tamara
alifurahi sana kuona ndege zikipaa na kutua kwa karibu sana.
Hakuamini kuwa siku hiyo pia naye angeabiri ndege.Alikuwa
amezoea tu kuimbia ndege zikipita angani akiwa na wenzake
walipokuwa wakicheza katika uwanja wa shule.
Tamara alikuwa na mchanganyiko wa hisia walipoitwa ili
kuingia kwenye ndege. Alitamani sana kuabiri ndege, lakini
ndani kwa ndani alikuwa na woga. Alijipiga moyo konde na
kujiambia,“Sema ukweli utakuweka huru.
Mara hiyo hiyo alimkaribia mwalimu wake na kumwambia,
“Mwalimu, ninaogopa kupaa angani kwa ndege. Sijui nifanyeje.
51
52
“Mara yangu ya kwanza kupaa kwa ndege niliogopa sana.
Nilikuwa kama wewe tu, lakini usitie shaka.Tutakapoingia ndani
ya ndege tutapewa maelezo kuhusu safari yetu. Maelezo hayo
yatapunguza idadi ya maswali mengi ambayo yanaisumbua
akili yako. Maelezo hayo ambayo yanahusu usalama wetu
tukiwa safarini, yatapunguza taharuki na woga. Kama una
swali unaweza kuuliza na utajibiwa mara moja. Usikubali woga
ukuhini raha inayokungojea ya kusafiri kwa ndege. Nina hakika
utaipenda safari hii na kuikumbuka siku zote za maisha yako,
Bwana Jasiri alimweleza Tamara.
“Asante, mwalimu.Woga wangu umenitoka, alisema Tamara
kwa tabasamu.
53
Kamusi Yangu
aligugumiza alisema kwa kukatakata maneno.
barakoa kitambaa cha nguo ambacho watu
hujifunika mdomoni na puani ili kuzuia
kuambukizwa ugonjwa kupitia kwenye
hewa wanayopumua
chanjo dawa inayotolewa kwa ajili ya
kukinga watu kutokana na magonjwa ya
kuambukiza
hufundika huweka moyoni bila kuzungumzia
imewasajili imewaandikisha
jinamizi ndoto ya kutisha
kanuni sheria ambazo zimewekwa ili watu
wafuate
kieuzi dawa ya kunawia mkono ili kuangamiza
virusi
kilimsaliti kilikataa kumtii
kugoteana kusalimiana kwa kukutanisha mikono
ikiwa imekunja ngumi
kumbukumbu maandishi yanayoelezea mambo
ambayo yalitokea zamani
kususia kukataa kufanya jambo
malenga mtu ambaye ni hodari wa kutunga na
kuimba mashairi
mikaka miaka mingi iliyopita
minong’ono habari ambazo hazina uhakika
mithili mfano
ninga ndege mwenye kuimba kwa sauti ya
kuvutia
ruya ndoto
taharuki hali ya kutojua kitakachotokea baadaye
54
Maswali
1. Mshairi anaandika kumbukumbu kuhusu nini?
2. Kwa nini korona inafananishwa na jinamizi katika ubeti
wa pili wa shairi?
3. Unafikiri ni kwa nini mshairi hakuamini aliposikia korona
ikizungumziwa?
4. Taja mambo ambayo yalitendeka baada ya korona
kuvamia kwa mujibu wa ubeti wa nne.
5. Watu walijikinga vipi dhidi ya korona kwa mujibu wa ubeti
wa tano?
6. Eleza jinsi ambavyo watu walisalimiana wakati wa korona.
7. Ni uvumbuzi gani ambao ulisaidia kudhibiti korona?
8. Je, kwa nini ni hatari kwa watoto kutumia vieuzi bila
kuelekezwa na watu wazima?
9. Unafikiri korona ilikuwa na athari gani kwa wanajamii?
10.Taja njia ambazo unafikiri zilitumiwa kufunza mtandaoni
wakati wa korona?
55
Mazoezi
Sehemu ya A
Kusikiliza na Kuzungumza
1. a. Ukiwa na rafiki yako zungumzeni kuhusu ugonjwa wa
korona. Maswali haya yatawaongoza:
i. Dalili za korona ni zipi?
ii. Watu wanaweza kujikinga vipi wasiambukizwe korona?
iii. Chanjo ina umuhimu gani kwa wanajamii?
iv. Ugonjwa kama korona unaweza kuathiri vipi uchumi
wa nchi?
b. Ugonjwa wa kisaikolojia una athari gani za kiafya
kwa wanajamii?
2. Mkaririe rafiki yako shairi hili. Mwombe akurekodi
kwenye kifaa cha kidijitali. Sikilizeni shairi ulilokariri huku
mkitathmini matamshi yako ya sauti na maneno katika
shairi. Unaweza kumtumia mwalimu wako rekodi hiyo,
akusikilize na kuyatathimini matamshi yako.
3. Ukiwa na rafiki yako tungeni ubeti mmoja wa shairi.
Msomee mzazi au mlezi wako ubeti huo ili akupe maoni
yake.
Sehemu B
Ufahamu wa Kusoma
Jibu maswali haya.
1. Eleza jinsi ambavyo kusema ukweli kulimwokoa Tamara.
2. Bi.Azuri ana moyo wa utu. Eleza.
3. Pendekeza mambo ambayo walimu na wanafunzi wanaweza
kufanya ili kuwalinda kisaikolojia wanafunzi wenye dosari
za kimaumbile wakiwa shuleni.
4. Eleza maana za methali zote zilizotumiwa kwenye kisa.
Sehemu C
Matumizi ya Lugha
Ugonjwa __1__ kisaikolojia ni hatari sana kwa kuwa dalili
zake __2__ wazi.Wagonjwa wengine mara nyingi hawaonyeshi
ishara zozote za ugonjwa __3__ hadi pale wanapozidiwa.
Wengine huonyesha dalili ambazo zinahusiana na magonjwa
mengine ya kuambukiza. Mgonjwa __4__ sana na kufanyiwa
uchunguzi ndipo tatizo linapoweza kugunduliwa. Ni muhimu
kutafuta huduma za tiba kila tunapougua ili tupate suluhisho
ya maradhi. ___5___.
1. a. ya b. wa
c. la d. za
2. a. haionekani b. halionekani
c. hazionekani d. havionekani
3. a. huo b. hiyo
c. hizo d. hizi
4. a. anapozidia b. anapozidi
c. anapozidisha d. anapozidiwa
5. a. Ganga ganga za mganga huleta matumaini
b.Atafutaye hachoki, akichoka keshapata
c. Jitihada huvuta heri
d. Penye nia pana njia
Sehemu ya D
Kuandika
Darasani mwenu kuna mwanafunzi ambaye hapendi kucheza
na wenzake. Umegundua kuwa ana tatizo la kisaikolojia.
Andika insha ya maelezo isiyopungua maneno 150 kuhusu
jinsi ambavyo unaweza kumsaidia. Msomee rafiki yako insha
yako ili akupe maoni yake.
56